Ratili

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa sarafu ya Uingereza, angalia makala ya Pauni (sarafu)

Ratili (kutoka Kiarabu رطل ratl; pia: pauni kutoka Kiingereza pound) ni jina la kizio cha uzito wa takriban nusu kilogramu.[1] Wakati wa ukoloni chini ya mfumo wa vipimo rasmi vya Uingereza wakati ule pound ilikuwa kipimo rasmi kilicholingana na gramu 454. Kifupi chake kilikuwa £ au lb kutoka Kilatini libra.

Tangu kuenea kwa vipimo vya SI ratili imetazamiwa kama jina la takriban gramu 454.

Asili ya ratili[hariri | hariri chanzo]

Ratili pia ni kati ya vipimo asilia vya Kiswahili. Kihistoria, ilikuwa kipimo cha uzito cha takriban nusu kilogramu au gramu 400-500.

Ratili ilipokewa kutoka vipimo vya Kiarabu رطل ratl, iliyotumiwa kwa jina hili katika sehemu nyingi za nchi za Kiislamu. Lakini uzito wa ratl ulikuwa tofauti kati ya nchi, majimbo na miji, kuanzia gramu 340 hadi zaidi ya kilogramu 2. Ratili ya Uswahilini ililingana zaidi na ratl jinsi ilivyotumiwa Uarabuni katika eneo la Makka iliyokuwa kidogo juu ya gramu 400.[2]

Ratili kama kipimo cha kihandisi na biashara[hariri | hariri chanzo]

Hadi leo "ratili" inatumiwa pale ambako matini za kiingereza zinatafsiriwa zinazotumia pound.

  • pau za reli zinatofautishwa mara nyingi kwa kutaja uzito kwa urefu na katika mfumo wa vipimo vya Uingereza ni "pound per yard" na kwa Kiswahili "ratili"[3]. Hapo ratili inalingana na pound ya Kiingereza ambayo ni gramu 453.59237.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Kamusi ya Kiswahili Sanifu (toleo la 4). Dar es Salaam: TUKI. 2019. uk. 520. ISBN 978 019 574616 7. 
  2. Makala "Makayil" katika The Encyclopedia of Islam, Leiden 1991, Vol VI, MAHK—MID
  3. linganisha taarifa kwenye tovuti ya TRL Archived 8 Septemba 2018 at the Wayback Machine. "kazi ya kutandika reli nzito ratili 80 imekamilika", habari ya 25 Machi 2017, iliangaliwa Aprili 2017