Montenegro

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Montenegro
Ramani ya Montenegro

Montenegro (yaani Mlima mweusi kwa lugha ya Kiitalia; kwa Kimontenegro: Црна Гора au Crna Gora) ni nchi ndogo ya Ulaya kwenye rasi ya Balkani.

Ina pwani ya Mediteranea na inapakana na Albania, Kosovo, Kroatia, Serbia, Bosnia na Herzegovina na Masedonia.

Mji mkuu ni Podgorica

Nchi ni mwanachama wa Umoja wa Mataifa na inatarajia kujiunga na Umoja wa Ulaya.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Tangu karne za kati maeneo ya Montenegro yalikaliwa na watu ambao walitumia lahaja ya lugha ya Kiserbokroatia na kufuata Ukristo wa Kiorthodoksi.

Katika eneo lenye milima mingi makabila yao yalifaulu kutunza kiwango cha uhuru chini ya himaya mbalimbali.

Tangu mwaka 1500 Milki ya Osmani ilivamia sehemu kubwa ya Balkani yaani nchi za Ulaya kusini-mashariki. Lakini Waosmani walishindwa kutawala mabonde ya Montenegro.

Makabila yake yaliunganika chini ya maaskofu wa Cetinje walioshika nafasi kama viongozi wa kiroho na wa kisiasa hadi karne ya 19 wakitumia cheo cha "Vladika". Jinsi ilivyo kwa maaskofu wa Kiorthodoksi hawakuruhusiwa kuoa, hivyo ilikuwa kawaida ya kwamba mpwa wa askofu mtawala aliandaliwa kumfuata na kuwa vladika mpya.

Baada ya kupata msaada wa kidiplomasia kutoka Urusi, sultani wa Milki ya Osmani alipaswa kutambua uhuru wa Montenegro.

Mwaka 1851 askofu na vladika Danilo II aliamua kuoa akajiuzulu cheo chake cha Kikanisa na kuendelea kutawala kama mtemi wa Montenegro.

Nikola I alikuwa mtemi kuanzia mwaka 1860. Wakati wake uhuru wa Montenegro ulitambuliwa na mataifa ya Ulaya. Milki ya Osmani ilipaswa kukubali polepole uhuru ya mataifa mbalimbali ya Balkani kama Waserbia, Wabulgaria na Waromania na katika mchakato wa kupanga mipaka mipya eneo la Montenegro liliongezeka pia.

Mwaka 1910 kwenye sherehe ya miaka 50 ya utawala wake, Nikola alipokea cheo cha "mfalme wa Montenegro".

Nchi hii ndogo iliingia katika Vita Kuu ya Kwanza upande wa Serbia ikavamiwa na jeshi la Austria-Hungaria mwaka 1915 na mfalme alipaswa kukimbilia Ufaransa.

Baada ya vita mkutano wa kimapinduzi ulitangaza kuunganishwa kwa Montenegro na Serbia. Wakati wa kuporomoka kwa Austria-Hungaria lilitangazwa dola jipya la Ufalme wa Yugoslavia lililojumuisha Serbia - Montenegro, Kroatia, Slovenia pamoja na maeneo ya Bosnia-Herzegovina. Montenegro ilikuwa sasa mkoa mmojawapo ndani ya Yugoslavia.

Ufalme huo ulivamiwa na Italia na Ujerumani wakati wa Vita Kuu ya Pili na kugawiwa kwa muda.

Baada ya vita wanamgambo Wakomunisti chini ya Josip Broz Tito walishinda wapinzani wote na kuanzisha Shirikisho la Jamhuri ya Watu wa Yugoslavia na katika katiba yake Montenegro ilikuwa tena moja kati ya jamhuri sita zilizounda shirikisho hili.

Baada ya kifo cha Tito umoja wa Yugoslavia ulidhoofika. Mashindano kati ya mataifa ndani ya nchi yaliongezeka. Mwaka 1991 Kroatia, Slovenia na Masedonia zilichukua hatua ya kutoka nje ya shirikisho na kujitangaza kuwa nchi huru za pekee. Mwaka 1992 jimbo la Bosnia na Herzegovina likafuata na kutoka nje.

Tangu hapo "Yugoslavia" ilikuwa jina la umoja wa Serbia na Montenegro pekee. Mwaka 2003 jina la Yugoslavia lilifutwa. Mwaka 2006 hata umoja uliobaki kati ya Serbia na Montenegro ulifutwa na kila nchi imeendelea peke yake.

Hivyo Montenegro ni tena nchi ya kujitegemea.

Wakazi[hariri | hariri chanzo]

Wananchi ni mchanganyiko mkubwa upande wa kabila na lugha, ingawa wengi wana asili ya Kislavoni.

Upande wa dini wengi ni Waorthodoksi (72.07%), wakifuatwa na Waislamu (19.11%) na Wakatoliki (3.44%).

Makala hii kuhusu maeneo ya Ulaya bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Montenegro kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.