Eurasia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Eneo la Eurasia
Namna mbalimbali za kuchora mpaka kati ya Ulaya na Asia.

Eurasia ni jina linalotumika kutaja kwa pamoja nchi zote za Asia na Ulaya. Jina hilo linaunganisha maneno "Europa" na "Asia".

Hali halisi mabara ya Ulaya na Asia yako pamoja kama nchi kavu mfululizo na hakuna bahari inayoyatenganisha. Kwa hiyo Ulaya na Asia haziitwi mabara kwa sababu za kijiografia bali kwa sababu za kihistoria na za kiutamaduni tu.

Desturi hii inatokana na Wagiriki wa Kale waliokuwa watu wa kwanza wa kugawa dunia katika sehemu tatu tofauti (Ulaya, Asia na Afrika) na hivyo kuweka msingi wa ugawaji wa dunia kwa mabara.

Wataalamu wengi wa jiografia wanaona ya kwamba masi ya nchi kavu inayojumlisha Ulaya na Asia ina tabia zote za bara moja na hivyo hutumia jina la "Eurasia". Karibu eneo lote liko juu ya bamba la gandunia lilelile, yaani Bamba la Ulaya-Asia.

Tangu kale suala la mpaka kati ya Ulaya na Asia lilikuwa tata na kuna majibu mbalimbali. Wengi hukubaliana ya kwamba mstari unafuata milangobahari ya Dardaneli na Bosporus (nchini Uturuki), mwambao wa Bahari Nyeusi na Bahari Kaspi halafu safu ya milima ya Ural hadi Bahari Aktiki. Lakini kati ya Bahari Nyeusi na Kaspi katika eneo la Kaukasus mawazo hutofautiana sehemu gani ni za Asia na zipi za Ulaya.

Makala hii kuhusu eneo fulani bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu eneo hilo kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Je, unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.


Usitaje majina ya madiwani na viongozi au maafisa wengine wa sasa maana wanabadilika haraka mno.