Lucy Lameck

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Lucy Lameck

Amekufa 21 Machi 1993
Nchi Tanzania
Kazi yake siasa

Lucy Lameck (1934 - 21 Machi 1993) alikuwa mwanasiasa wa Kitanzania, na mwanamke mtanzania wa kwanza kuwahi kushika wadhifa wa uwaziri kwenye serikali ya kitaifa.

Alizaliwa katika familia ya wakulima, akajifunza kazi ya uuguzi kabla ya kuingia katika shughuli za siasa.

Alisoma baadaye kwenye Chuo cha Ruskin, huko Oxford, Uingereza. Mwaka 1960 aliingia mara ya kwanza katika Bunge la Tanganyika kabla ya kuchaguliwa katika Bunge la Kitaifa la Tanzania mnamo 1965. Aliendelea kushikilia nafasi ya mbunge hadi kifo chake, isipokuwa miaka 1975 hadi 1980.

Anakumbukwa kama kielelezo cha kuigwa, akiwa amefanya kazi katika maisha yake yote kuboresha hali ya wanawake nchini Tanzania.

Utoto na Ujana[hariri | hariri chanzo]

Lucy Lameck na Victoria Kopney Modeling walionyesha mavazi yaliyopendekezwa kuwa ya kitaifa.

Lucy Selina Lameck Somi, aliyejulikana baadaye kama Lucy Lameck, alizaliwa mnamo 1934 Moshi mjini iliyokuwa wakati ule sehemu ya Tanganyika ya Kiingereza.

Alilelewa katika familia ya wakulima, ambao walikuwa wakijihusisha na siasa na siku moja walikuwa wenyeji wa Julius Nyerere. Lucy alihudhuria Shule ya Misioni ya Kanisa Katoliki ya Kilema, iliyoendeshwa na Masista Wamisionari wa Afrika.

Baada ya mafunzo ya kazi ya muuguzi mnamo 1950, hakutaka kushiriki katika mfumo wa matibabu wa kikoloni wa Uingereza, na kwa hiyo alianza kufanya kazi ya karani. Kati ya miaka 1955 na 1957, alifanya kazi kwa Kilimanjaro Native Cooperative Union alipoanza kujiingiza katika siasa.

Alijiunga na chama cha TANU[1] akichaguliwa kiongozi wa Umoja wa Wanawake wa TANU. Hapa alishiriki katika jitihada za kubuni mavazi ya kitaifa ya Tanganyika. [2] Alikuwa mmoja wa wanachama wa kwanza wakati TANU ilipofungua tawi huko Moshi. [3]

Kazi ya kisiasa[hariri | hariri chanzo]

Kutokana na shughuli hizo za kisiasa alipata nafasi ya kusoma siasa huko Uingereza kwenye Chuo cha Ruskin mjini Oxford kwa msaada wa Umoja wa Wafanyakazi wa Uingereza. Alipokuwa Uingereza, alitoa hotuba mbele ya Waafrika wengine pale London, na pia alipata nafasi ya kusoma mhula mmoja kwenye Chuo Kikuu cha Western Michigan huko Marekani. [1] Mhula huo ulidhaminiwa na kundi la Delta Sigma Theta Sorority, na Lucy alichunguza tofauti ya kiuchumi kati ya Marekani na Tanganyika.[4] Lameck alieleza mipango yake kwenye mahojiano na gazeti la Jet Magazine" kuwa alitaka kuwahi kurudi kwa ajili ya uchaguzi katika Tanganyika, uchaguzi wa kwanza kabla ya uhuru. Aliongezea pia kuwa mahusiano baina ya mibari (races) katika Tanganyika yalikuwa bora kuliko alivyoona huko Marekani. [5]

Alirudi Tanganyika, ambapo aliteuliwa na waziri mkuu Nyerere kuwa mbunge katika Bunge la Tanganyika. Kati ya miaka 1962 na 1965, alikuwa waziri mdogo wa Shirika na Maendeleo ya Jamii.[1] Hii ilikuwa nafasi ya kwanza ya uwaziri kushikiliwa na mwanamke huko Tanganyika au Tanzania. [4]

Katika uchaguzi wa kwanza baada ya maungano ya Tanganyika na Zanzibar mwaka 1965, alichaguliwa na wananchi kuwa mbunge na kushika nyadhifa mbili za Naibu Waziri wa Shirika na Maendeleo ya Jamii kati ya 1965 na 1970, na Naibu Waziri wa Afya kati ya 1967 na 1972. Alitetea kiti chake katika uchaguzi wa 1970, lakini akakipoteza mnamo 1975. Lameck alishinda ubunge tena baada ya uchaguzi mkuu mnamo 1980, na aliendelea kushikilia hadi kifo chake. Alianzisha sheria anuwai, pamoja na zile za kuboresha hali ya wanawake ndani ya nchi. [1]

Aliaga dunia tarehe 21 Machi 1993 kutokana na ugonjwa wa figo. Mazishi yake yalihudhuriwa na Nyerere, Rais wa Zanzibar Salmin Amour na Waziri Mkuu wa Tanzania John Malecela . [6]

Tangu wakati huo amekumbukwa kama mfano wa kuigwa kwa wanawake, haswa wanasiasa wanawake, ndani ya Tanzania.

Mengineyo[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 2020 mtaa mjini Berlin ulipewa jina lake, kuwa Lucy-Lameck-Straße. Mtaa huo uliwahi kuitwa kwa jina la Hermann von Wissmann, gavana wa awali wa iliyokuwa Afrika ya Mashariki ya Kijerumani.[7]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. 1.0 1.1 1.2 1.3 Akyeampong, Emmanuel Kwaku; Gates, Jr., Henry Louis (2012). Dictionary of African Biography. New York: Oxford University Press. p. 464. ISBN 978-0-195382-075. 
  2. "CO 1069-164-74". 
  3. Mwakikagile, Godfrey (2010). Nyerere and Africa: End of an Era (5th ed.). Pretoria: New Africa Press. p. 86. ISBN 978-0-980253-412. 
  4. 4.0 4.1 Brown, Tamara L.; Parks, Gregory S.; Phillips, Clarenda M., eds. (2012). African American Fraternities and Sororities: The Legacy and the Vision. Lexington, Kentucky: University Press of Kentucky. p. 30. OCLC 940737830. 
  5. "Says Tanganyika Race Relations Outstrip U.S.". Jet (Ebony Media Operations): 4. 4 February 1960. 
  6. Obituaries. Tanzanian Affairs (1 May 1993). Iliwekwa mnamo 6 November 2017.
  7. [http://web.archive.org/20201127234642/https://www.thecitizen.co.tz/tanzania/news/germany-to-name-a-street-in-berlin-after-tanzanian-independence-activist-3211946 Archived 27 Novemba 2020 at the Wayback Machine. }Germany to name a street in Berlin after Tanzanian independence activist
Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Lucy Lameck kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.