Punt

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Land of Punt)

kwa eneo la kujitawala katika kaskazini ya Somalia angalia Puntland

Malkia Ati, mke wa Mfalme Perahu wa Punt. Taswira kwenye hekalu ya Farao Hatshepsut huko Deir el-Bahri.

Punt (iliitwa pia Pwenet au Pwene[1] na Wamisri wa Kale) ilikuwa milki katika Zama za Kale. Habari zake zinajulikana kutokana na taarifa za Wamisri wa Kale waliofanya biashara nayo. Ilikuwa na sifa za kuzalisha dhahabu, ubao wa mpingo, meno ya ndovu na uvumba zilizotafutwa sana nchini Misri. [2]

Taarifa za Wamisri[hariri | hariri chanzo]

Katika makaburi na majengo mengine ya Misri ya Kale yaliyohifadhiwa hadi leo kuna picha za Punt na maandishi yanayorejelea Punt. Vyote vinasema ya kwamba Punt ilikuwa karibu na bahari na njia ya kuifikia ilikuwa kupitia Bahari ya Shamu. Kati ya watu wake kulikuwa na vikundi vitatu vilivyotofautiana katika nguo na namna ya kupamba nywele zao. Kulikuwa na nyumba zilizojengwa juu ya nguzo na ufugaji wa ng'ombe. Katika hadithi za Wamisri nchi ya miungu ilikuwa karibu na Punt.

Farao mbalimbali walituma misafara ya kibiashara kwenda Punt na taarifa zao ni msingi wa habari zetu juu ya nchi hii. Farao wa kwanza anayejulikana alikuwa Sahure katika nasaba ya tano (karne ya 25 KK). Safari nyingine zilifuata.

Taarifa pana zaidi inapatikana katika hekalu la Hatshepsut wa nasaba ya 18 (karne ya 15 KK). Huyu malkia aliamuru kujenga kundi la meli zilizozunguka mara kwa mara kwenye Bahari ya Shamu hadi Punt. Picha za safari za meli 5 bado zinaonekana ukutani mwa hekalu la Deir el-Bahri. Katika maandishi ya picha majina ya mfalme na malkia wa Punt wa wakati ule yamehifadhiwa: ni mfalme Parahu na malkia Ati.

Baada ya mwaka 1000 KK mawasiliano yalififia na hatimaye kwisha, labda kutokana na kipindi cha mvurugo katika Misri.

Mahali pa Punt[hariri | hariri chanzo]

Maeneo ambako uwepo wa Punt umejadiliwa

Mahali pa Punt bado haijatambuliwa na wanahistoria kwa uhakika. Zamani maoni yalitofautiana zaidi, lakini tangu kutambua taarifa inayopatikana katika hekalu la kaburi la malkia Hatshepsut inaeleweka ya kwamba Punt ilikuwa upande wa kusini wa Misri. Ilhali njia ya bahari inaacha uwezekano ya kwamba Punt ilikuwepo ama Uarabuni kusini au kinyume upande wa Eritrea na Somalia, kuna bado taarifa nyingine iliyotambuliwa.[3] Hapo msafara fulani ulirudi Misri kwa kufuata njia ya mto Naili. Kwa hiyo leo wataalamu wengi wanafikiri mahali pa Punt ilkuwa barani Afrika, kwenye pwani za Sudan, Eritrea au Somalia. Wachache wamehisi Punt kuwa kusini zaidi, hadi Afrika ya Mashariki.

Leo hii sehemu ya kaskazini ya Somalia inayojitawala iliamua kutumia jina hili la kale na kujiita Puntland.[4]

Picha za Punt kutoka Hekalu la Hatshepsut[hariri | hariri chanzo]

Maelezo[hariri | hariri chanzo]

  1. Ian Shaw & Paul Nicholson, The Dictionary of Ancient Egypt, British Museum Press, London. 1995, p.231.
  2. Shaw & Nicholson, p.231.
  3. Simson Najovits, Egypt, trunk of the tree, Volume 2, (Algora Publishing: 2004), p.258.
  4. Puntland profile, BBC News. http://www.bbc.com/news/world-africa-14114727
Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Punt kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.