Kitanda

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa maana nyingine ya neno hili angalia hapa Kitanda (maana)

Kitanda cha Waswahili wa Kenya.

Kitanda ni samani ya kulala au kujipumzisha inayopatikana kwa kawaida katika kila nyumba.

Asili ya neno "kitanda" ni mzizi "-tanda".

Katika utamaduni wa Waswahili kitanda ni samani kubwa. Ina kiunzi au fremu ya ubao, yenye vitakizo viwili upande wa kichwa na mguuni vinavyoshikwa kwa mifumbati kila upande. Yote inakaa juu ya matendegu (miguu ya ubao) manne. Nafasi kati ya mifumbati inafumaniwa kwa kamba, usumba wa nazi au nyasi. Juu ya hii huwekwa mkeka au godoro. Vitakizo mara nyingi hupambwa kwa vioo vya rangi au vyenye picha. Kiunzi cha juu kinaweza kufunikwa kwa vitambaa au chandarua.

Ukubwa wa kitanda hutofautiana. Kuna kitanda kidogo cha mtoto, vitanda vya kawaida vya kulaliwa na mtu mmoja na pia kitanda kikubwa zaidi cha kulaliwa na watu wawili[1].

Kitanda cha wagonjwa[hariri | hariri chanzo]

Kitanda cha hospitalini kinachotumia umeme kikamilifu.
Kitanda cha wagonjwa wanaougua nyumbani kinachotumia mikono na umeme pia.

Tofauti na vitanda vingine, kitanda cha wagonjwa walio mahututi au wazee wanaopokea matibabu nyumbani ni kuwa kinaweza kubadilishiwa kimo pamoja na jinsi miguu na kichwa kilivyo. Haya hufanyika maana mgonjwa huwa haamki kwa kile kitanda na atatazama runinga au kupata chakula chake akiwa kitandani.

Muundo wa kitanda cha hospitali ambao una uwezekano kuwa chaweza kuinua kichwa au miguu ya mgonjwa ulianzishwa na daktari Mjerumani Friedrich Trendenburg ambaye alikuwa akiwatibu wagonjwa wa mshuto katika vita vikuu vya kwanza. Daktari huyo alikuwa akiwaweka wagonjwa kichwa chini na miguu juu. Baadaye, kukaa huku kuliitwa trendenburg.

Pia kuna kitanda cha mwinuko "elevation bed" ambacho hutumika hasa nyumbani sana sana na watu wenye shinda ya mzunguko wa damu miguuni, wanaopata maumivu ya maungio ya mifupa na pia wanao penda starehe kitandani. Kitanda cha muinuko pia kina uwezo wa kubadili kimo kama kitanda cha wagonjwa, na la ziada, chaweza pia kubadili umbo la msingi wa kulalia na kuchukua umbo la anayekilalia. Kitanda cha muinuko cha kisasa hutumia kisengeletua/kitanza mbali (remote control) kudhibiti muinuko na umbo lake.

Aina za vitanda vya wagonjwa[hariri | hariri chanzo]

Vitanda vya wagonjwa vinaweza kuainishwa mara tatu

  • 1. Kitanda kinachotumia mikono. Kitanda hiki huweza kubadilishwa kimo, kuinua kichwa na miguu kwa mikono maana kina kichuma maalumu miguuni.
  • 2. Kitanda kinachotumia kawi ya umeme. Kitanda hiki hutumia kawi za umeme au stima kufanya kazi na kubadilisha kimo, miguu na kichwa. Huuzwa kikiwa na mota ambayo husaidia kubadilisha kimo na mengineyo. Stima zikipotea, itabidi utumie mikono
  • 3. Kitanda kinachotumia kawi na mikono. Kitanda hiki hutumia mota kuinua kichwa au miguu ya mgonjwa lakini likija ni kubadilisha kimo, hutumia mikono kwa kuzungusha kijichuma.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya utamaduni bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kitanda kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.