Kiingereza

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Pitio kulingana na tarehe 13:43, 9 Januari 2016 na 84.168.225.165 (majadiliano) (→‎Kiingereza Afrika: Gambia no longer: http://www.aljazeera.com/news/africa/2014/03/gambia-drop-english-as-colonial-relic-2014313141814734996.html)
EN (ISO 639-1)

Kiingereza ni lugha ya Kigermanik cha Magharibi iliyokua nchini Uingereza.

Leo, zaidi ya wasemaji milioni mia nne duniani wanazumgumza Kiingereza kama lugha ya kwanza. Watu wengi zaidi wanazumgumza Kiingereza kama lugha ya pili, kwa sababu ni muhimu sana kwenye nyanja za sayansi na uchumi wa kimataifa.

Uenezi wa Kiingereza

Buluu nyeusi: Nchi ambako Kiingereza ni lugha ya kwanza ya wananchi wengi;
buluu nyeupe: nchi ambako Kiingereza ni lugha rasmi lakini si lugha ya kwanza ya watu wengi.
Kiingereza kipo pia kati ya lugha rasmi za Umoja wa Ulaya.

Kiingereza ni lugha rasmi pekee katika nchi za Uingereza, Marekani, Australia, Nyuzilandi, Jamaica, na nchi nyingine.

Kiingereza ni lugha rasmi pamoja na lugha nyingine katika nchi nyingi, kwa mfano Kanada (pamoja na Kifaransa), India (pamoja na Kihindi na lugha za majimbo), Ireland (pamoja na Kigaelik), Philippines (pamoja na Kitagalog).

Kiingereza Afrika

Nchi nyingi za Afrika zinatumia Kiingereza kama lugha rasmi, lakini ni Waafrika wachache (isipokuwa Waafrika Kusini) wanaoitaja kuwa lugha ya kwanza kwao. Nchi hizo ni Afrika Kusini, Ghana, Lesotho, Liberia, Kamerun, Kenya, Namibia, Nigeria, Sierra Leone, Swaziland, Zambia na Zimbabwe.

Kiingereza kinazumgumzwa pia katika nchi nyingine za Afrika ambapo si lugha rasmi.

Lugha nyingi za Afrika zimeazima maneno ya Kiingereza. Maneno haya yamerekebishwa kulingana na sauti ya lugha nyingine, kwa mfano: Kiingereza: train --> Kiswahili: treni.

Historia ya Kiingereza

Mwanzo wa lugha

Lugha ya Kiingereza ilianzia huko Uingereza kutokana na kuingiliana kwa lugha mbalimbali hasa lugha za kale za Ujerumani, Denmark na Ufaransa.

Sehemu ya kusini ya kisiwa cha Britania ilikuwa ndani ya Dola la Roma hadi mwanzo wa karne ya 5. Wenyeji walitumia lugha ya Kikelti pamoja na Kilatini cha Waroma, hasa mjini.

Uvamizi wa Waanglia-Saksoni: kuja kwa Kigermanik

Baada ya kuondoka kwa Waroma makabila kutoka Ujerumani wa Kaskazini na Denmark walianza kuvamia kisiwa hicho. Katika mwendo wa karne mbili waliteka sehemu kubwa ya Britania isipokuwa sehemu za magharibi kama vile Cornwall na Wales na sehemu za kaskazini walipoishi Waskoti.

Wavamizi walileta lugha zao za Kisaksoni na Kianglia (Ujerumani wa Kaskazini) zilizounganika kuwa lugha ya Kiingereza cha Kale. Inaonekena ya kwamba wenyeji walio wengi walianza kutumia lugha ya watawala wapya, wengine waliuawa au walihamia sehemu zisizo chini ya Waanglia-Saksoni.

Lugha hii iliathiriwa mara mbili. Kwanza Wadenmark ndio waliojaribu kujenga ufalme wao kisiwani. Waliteka sehemu za Uingereza ya Magharibi. Kiasi cha maneno kutoka lugha yao kimeingia Kiingereza cha kale kama Wales.

Uvamizi wa Wanormandy: kuja kwa Kifaransa, lugha mbili kando

Mwaka 1066 jeshi la Kinormandy kutoka Ufaransa wa Kaskazini walivamia na kuteka Uingereza. Wanormandy walikuwa wa asili ya Skandinavia lakini walikuwa wameshaanza kutumia lugha ya Kifaransa cha kale. Wanajeshi hawa walikuwa mabwana wapya wa Uingereza wakitumia Kifaransa chao cha Normandy.

Kwa karne kadhaa lugha mbili zilitumika kandokando: Kiingereza cha Kianglia-Saksoni cha watu wa kawaida na kile Kifaransa cha Kinormandy cha tabaka la watawala. Kwa jumla watawala walianza kutumia lugha ya raia lakini lugha hii ilibadilika pia kwa kupokea maneno mengi kutoka Kifaransa. Kuna makadirio ya kwamba zaidi ya theluthi moja ya maneno yote ya Kiingereza yana asili ya Kifaransa.

Kuingiliana kwa lugha zote mbili: Kiingereza cha Kati

Kipindi hiki cha kuingiliana kati ya Kifaransa cha mabwana na lugha ya kawaida kilileta Kiingereza cha Kati. Hadi leo asili ya maneno kutoka Kijerumani na Kifaransa ni wazi kabisa.

Mfano mzuri ni maneno tofauti ya wanyama kadhaa na nyama yao: ng'ombe huitwa "cow" (sawa na Kijerumani wa Kaskazini "Kau") lakini nyama yake ni "beef" (kutokana na neno la Kifaransa kwa ng'ombe "boeuf"); vilevile "sheep" kwa mnyama kondoo na "mutton" kwa nyama yake (Kijerumani ya Kaskazini: "Schaap" - Kifaransa: "mutton"), vilevile swine – pork (nguruwe) na calf – veal (ndama).

Wakulima wafugaji walitumia lugha yao kwa mnyama - mabwana wasiogusa mnyama lakini kula nyama yake waliendelea kutumia neno la Kifaransa kwa ajili ya mnyama yuleyule. Maneno yote mawili yaliingia katika Kiingereza cha Kisasa lakini kwa mambo mawili tofauti.

Kiingereza cha Kisasa

Kiingereza cha Kisasa kimeanza na tafsiri ya Biblia ya William Tyndale; baadaye na washairi wakuu kama William Shakespeare.

Teknolojia ya uchapaji vitabu ilisambaza lugha hii nchini kote na kupunguza athira ya lahaja mbalimbali.

Wakati ule Kiingereza kilipokea pia maneno mengi kutoka lugha za Kilatini na Kigiriki zilizokuwa lugha za taaluma na sayansi hadi karne ya 18 kote Ulaya.

Kiingereza cha Kisasa kimeendelea kurahisisha lugha. Lakini urekebisho wa tahajia umeshindikana hadi leo hata kama kulikuwa na majaribio mbalimbali. Kutokana na historia yake Kiingereza kimebaki na tahajia isiyolingana na matamshi ya maneno.

Mwandishi George Bernhard Shaw alionyesha tatizo hilo kwa pendekezo la dhihaka kwamba neno "fish" (samaki) liandikwe "ghoti": gh kama sauti ya "f" katika "cough", o kama sauti ya "i" katika "women", na ti kama sauti ya "sh" katika "nation".

Uenezi wa Kiingereza duniani

Tangu karne ya 19 idadi kubwa ya wasemaji wa Kiingereza hawakuishi tena Uingerezea bali Marekani. Katika karne ileile Kiingereza kilikuwa lugha ya utawala katika maeneo makubwa ya makoloni ya Dola la Uingereza.

Baada ya makoloni kuwa nchi huru mara nyingi Kiingereza kimeendelea kuwa lugha rasmi za nchi hizo.

Kutokana na matukio hayo yote Kiingereza kimekuwa leo lugha ya kwanza ya mawasiliano duniani hata kama si lugha yenye wasemaji wengi wa lugha ya kwanza.

Viungo vya nje