Kighoma Malima

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kighoma Ali Malima (15 Desemba 1938 - 6 Agosti 1995) alikuwa mwanasiasa wa Tanzania na mwanachama wa CCM.[1]

Maisha ya awali na elimu[hariri | hariri chanzo]

Kighoma Malima alizaliwa katika kijiji cha Marui, wilaya ya Kisarawe na Ali bin Abdallah Kighoma Malima na Habiba binti Suleiman wa Bura. Aliitwa Abdallah, na baba yake mzazi aliyefariki katika Vita vya dunia vya kwanza.

Alisoma shule ya Msingi Marui na Shule ya Sekondari Mzumbe na Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora kuanzia mnamo mwaka 1948 hadi mwaka 1957. Malima alikatisha masomo yake mnamo mwaka 1957 ili kujiunga na TANU na kupigania uhuru chini ya uongozi wa Julius Nyerere.

Baada ya uhuru Malima aliteuliwa kuwa Katibu wa Wilaya huko Masasi na Njombe. Mnamo Juni mwaka 1961 alihudhuria kozi fupi katika Chuo cha Itikadi cha Kivukoni, mkoani Dar es Salaam kabla ya kuondoka kwenda Amerika mnamo mwaka 1962 kwa masomo zaidi katika Chuo cha Dartmouth, Hanover, New Hampshire ambapo alipata shahada ya kwanza katika nyanja ya Uchumi mnamo mwaka 1965.

Kighoma Malima na Mariam Fivawo walikutana huko Boston, mnamo mwaka 1965. Mariam Venantia alikuwa amehitimu katika chuo cha Regis Weston, na Kighoma Malima alikuwa amehitimu katika Chuo cha Dartmouth. Miezi michache baadaye walioana na kuhamia New Haven ambapo Kighoma Malima alienda kufuata masomo yake ya shahada ya pili ya Uchumi katika Chuo Kikuu cha Yale na alihitimu mnamo mwaka 1966. Kisha akaendelea na msomo katika Chuo Kikuu cha Princeton na akapewa tuzo nyingine ya shahada ya uzamili katika Uchumi mnamo mwaka 1970. Kisha akawa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Prof Malima alikuwa Mtanzania wa kwanza kufundisha uchumi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Maisha binafsi[hariri | hariri chanzo]

Malima na Mariam Fivawo Malima wamezaa watoto sita.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Obituary: Prof. Malima. Iliwekwa mnamo 2 January 2014.