Khalid bin Barghash wa Zanzibar

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Khalid bin Barghash wa Zanzibar.

Sayyid Khalid bin Barghash Al-Busaid (18741927) (kwa mwandiko wa Kiarabu خالد بن برغش البوسعيد) alikuwa mtawala wa 6 wa Usultani wa Zanzibar.

Alikuwa sultani kwa siku tatu pekee kuanzia tarehe 25 Agosti hadi 27 Agosti 1896 akaondolewa madarakani na Waingereza kwa nguvu ya jeshi katika Vita ya Uingereza dhidi ya Zanzibar.

Khalid bin Bargash alikuwa mwana wa kwanza wa Sayyid Barghash bin Said Al-Busaid. Baada ya kifo cha mjomba wake, sultani Hamad bin Thuwaini wa Zanzibar, alitangazwa na sehemu ya viongozi kuwa sultani mpya, lakini wengine walimpinga. Kulikuwa na uvumi wa kwamba alisababisha kifo cha mjomba wake kwa kumsumisha. [1]

Basil Cave, balozi wa Uingereza aliwahi kumkubali mgombea mwingine kutoka familia ya sultani, Hamud bin Mohammed, hakuwa tayari kumwona Khalid kwenye kiti cha mtawala akirejea mkataba kati ya Uingereza na Zanzibar ya mwaka 1890 iliyowapa Waingereza nafasi ya kumkubali sultani mpya.

Khalid alipewa muda wa kuondoka katika jumba la Sultani akakataa, akakusanya zaidi ya askari 2000 tayari kwa utetezi.

Asubuhi ya 27 Agosti 1896 Waingereza walikuwa na manowari 5 tayari kwenye bandari ya Zanzibar zilizolengesha bunduki zake kwa jumba la sultani. Saa 9.02 zilianza kulipiga jumba la sultani na kikosi cha wanajeshi kilishambulia jumba. Saa 9.40 jeshi la Sultani likajisalimisha baada ya kifo cha Wazanzibari 500. Sultani mwenyewe alikimbilia ubalozi wa Ujerumani alipopokewa na balozi Albrecht von Rechenberg (baadaye gavana wa Afrika ya Mashariki ya Kijerumani).

Baadaye Wajerumani walimpeleka Dar es Salaam, alipopewa hifadhi katika koloni la Afrika ya Mashariki ya Kijerumani[1], na Hamud bin Mohammed alipanda kiti cha sultani.

Sultani aliyefukuzwa aliishi Dar es Salaam hadi mwaka 1916. Mwaka ule Waingereza walitwaa mji wakati wa vita kuu ya kwanza ya dunia wakamkuta huyo aliyewahi kuwa sultani wa siku 3 wakampeleka kifungoni huko visiwa vya Shelisheli na baadaye Morisi.

Baada ya vita kwisha aliruhusiwa kurudi Afrika ya Mashariki.

Aliaga dunia mjini Mombasa mwaka 1926[1][2].

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. 1.0 1.1 1.2 Hernon, Ian (2003). Britain's Forgotten Wars. Stroud, Gloucestershire: Sutton Publishing. pp. 396–404. ISBN 9780750931625. 
  2. BBC h2g2 entry on the Anglo-Zanzibar War
Alitanguliwa na
Hamad bin Thuwaini
Sultani wa Zanzibar
1896
Akafuatiwa na
Hamud bin Muhammad
Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Khalid bin Barghash wa Zanzibar kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.