Franz Kafka

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Franz Kafka mnamo 1906

Franz Kafka (* 3 Julai 1883 - † 3 Juni 1924) alikuwa mwandishi kutoka milki ya Austria-Hungaria aliyetumia lugha ya Kijerumani.

Alizaliwa katika familia ya Kiyahudi mjini Praha (leo: nchini Ucheki) wakati ilipokuwa sehemu ya Austria-Hungaria. Lugha ya nyumbani ilikuwa Kijerumani lakini alijifunza pia Kicheki iliyokuwa lugha ya wakazi wengi wa Praha pamoja na Kifaransa alichofundishwa shuleni. Franz alikuwa na dada watatu waliouawa baada ya kifo chake wakati wa utawala wa Nazi kwenye makambi ya KZ.

Baada ya kumaliza shule ya sekondari mwaka 1901 aliitikia mapenzi ya babaye akasoma sheria kwenye chuo kikuu cha Praha kati ya 1901-1906 akimaliza kwa digrii ya PhD. Alipata kazi katika kampuni ya bima ya wafanyakazi.

Kafka aliona kazi yake ya ofisini kama kazi nyepesi iliyokosa maana.

Mwaka 1912 aliandika masimulizi yake ya kwanza "Das Urteil" (Hukumu). Hii ilikuwa kati ya kazi chache alizotoa mwenyewe. Mengine aliyoandika kama riwaya tatu "Der Process" (Kesi), "Amerika" (Marekani) na "Das Schloss" (Husuni) alitunza kwenye deski yake. Zilitolewa tu baada ya kifo chake.

Kafka aligonjeka mwaka 1917 kwa kifua kikuu akafa 1924. Aliacha maagizo ya kwamba maandiko yake yote yachomwe moto. Lakini rafiki yake Max Brod aliamua kuzitoa hata hivyo.

Vitabu vyake vilisambaa polepole lakini tangu vita kuu ya pili ya dunia Kafka hutazamiwa mara nyingi kama sauti ya Ulaya ya kisasa ambako mwanadamu anayeishi peke yake anajikuta mbele ya dunia isiyoeleweka tena.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]