Kunguni (familia)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Cimicidae)
Kunguni
Kunguni
Kunguni
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Arthropoda (Wanyama wenye mwili wa pingili na miguu ya kuunga wasio na ugwe wa mgongo kama wadudu, nge, buibui)
Nusufaila: Hexapoda (Arithropodi wenye miguu sita)
(bila tabaka): Dicondylia (Wadudu walio na mandibula zenye condyle mbili)
Ngeli: Insecta (Wadudu)
Nusungeli: Pterygota (Wadudu wenye mabawa)
Oda ya juu: Paraneoptera
Oda: Hemiptera
Haeckel, 1896
Nusuoda: Heteroptera
Familia ya juu: Cimicoidea
Familia: Cimicidae
Latreille, 1802
Ngazi za chini

Nusufamilia 6, jenasi 22; spishi 26 katika Afrika:

Kunguni ni wadudu wadogo wa familia Cimicidae katika oda Hemiptera ya nusungeli Pterygota (wenye mabawa). Wadudu hawa hufyonza damu ya wanyama wenye damu moto (mamalia na ndege). Spishi tatu huishi mara nyingi katika vitanda vya watu, lakini spishi nyingi sana huishi katika viota vya ndege au katika mapango au mahali pengine ambamo popo wanalala. Spishi hizi huitwa kunguni-ndege na kunguni-popo. Kunguni-mgunda ni jina la ujumla la spishi za nusuoda Heteroptera.

Biolojia[hariri | hariri chanzo]

Kunguni wote ni wadogo na wana umbo la duaradufu na bapa, ingawa mwili wao hufura baada ya kujilisha. Hawaruki lakini wana pedi ndogo za mabawa ambazo hazifanyi kazi. Pia wana sehemu za kinywa zinazofanana na kidomo ambazo hutumia kutoboa ngozi na kufyonza damu ya vidusiwa wao.

Kujilisha kunahitajika kwa uzalishaji wa mayai kwa majike na labda kwa uzalishaji wa manii kwa madume. Tabia ya kutaga mayai hutofautiana kati ya spishi. Kunguni wa Ulaya ataacha kutaga mayai yaliyowekewa manii kama siku 35 hadi 50 baada ya uingizaji wa mwisho wa manii. Kunguni-mbayuwayu, Oeciacus vicarius, hupitisha kipupwe baada ya kupandana wakati wa kupukutika na huanza kutaga wakati wa kuchipua ili kuambatana na kurudi kwa kidusiwa.

Kunguni huingiza manii kwa kujeruhi. Ingawa jike huwa na mfumo wa kawaida wa uzazi kwa kutaga mayai, dume huwa hautumii (isipokuwa katika spishi Primicimex cavernis), lakini hutoboa ukuta wa tumbo la jike; kisha manii huhamia kupitia mfumo wa kuzaa wa jike.

Inabidi kwamba kila hatua tano za tunutu zile mlo wa damu ili kuendelea hadi hatua inayofuata. Wapevu wameripotiwa kuishi miezi 3 hadi 12 katika kaya isiyopulizika kwa kiuawadudu. Mdudu aliyeachwa bila shida anaweza kuchukua dakika 3-15 ili kula mlo kamili kulingana na hatua ya maisha yake. Wanaweza kukaa muda mrefu bila kujilisha na kutoka tena mafichoni mwao wakati vidusiwa wanapopatikana tena. Wana tezi maalum za harufu na mara nyingi hutoa harufu bainifu ambayo kwa kawaida huweza kugunduliwa katika mahali palipojaa na kunguni sana. Madoa meusi ya mavi kwenye matandiko ya kitanda au nguo za kulalia, mayai yenye rangi ya lulu (urefu wa mm 1), na mavulio njano kama karatasi ni ishara nyingine za uwepo wa kunguni kwa tele, mara nyingi katika nyufa na mianya.

Vidusiwa[hariri | hariri chanzo]

Kunguni ni finyu kiasi katika uchaguzi wao wa vidusiwai kulingana na wadudu wengine wanaofyonza damu. Kunguni wengi wana kidusiwa anayempendelea, lakini wanakubali na wengine kadhaa wanapowasilishwa na chaguo, kama vile kunguni wa Ulaya na kunguni wa Afrika ambao mara nyingi hupatikana baina ya wanadamu, lakini pia wanaweza kuishi kwa kujilisha kwenye ndege, popo, sungura na panya. Nusufamilia kadhaa zinazuiliwa kwa spishi fulani za popo, wakati spishi moja, Primicimex cavernis, inaonekana kukubali spishi moja tu ya kidusiwa.

Kubadilisha kwa kidusiwa kunategemea mambo kadhaa pamoja na kulingana kwa ishara za kugundua kidusiwa na uwezo wa kumeng'enya aina tofauti za damu. Kwa mfano, seli nyekundu za damu za vifaranga ni ndefu zaidi kwa µm 3-5 kuliko zile za binadamu, ambayo inafanya damu ya watu kufaa zaidi mfereji mwembamba wa chakula wa kunguni wa Ulaya. Kunguni wa Afrika anaweza kutofautisha kipenyo cha mfereji wake wa chakula, ambayo inamruhusu kubadilika zaidi katika uchaguzi wa vidusiwa. Upendeleo kwa spishi ya kidusiwa unaweza kutofautiana kati ya makundi tofauti ya spishi fulani. Sababu za hii hazijulikani wazi.

Mwenendo[hariri | hariri chanzo]

Kunguni wanavutiwa na vidusiwa kwa aina tofauti za ishara pamoja na joto (hata tofauti ya joto ya 1° C) na kairomoni. Ishara za vidusiwa (angalau katika spishi kadhaa pamoja na kunguni wa Ulaya na Stricticimex antennatus) hubadilika kutoka kwa vivutio mpaka vifukuzi baada ya kujilisha kwa kunguni, ambyo inamsababisha kuondoka eneo la hatari.

Takriban kunguni wote hujilisha mara moja kila siku 3-7 katika hali ya asili. Kwa kawaida kunguni wa Ulaya hujilisha mara moja kila siku 7 na Ornithocoris toledoi kila siku 8, ingawa kunguni wa Afrika ameonwa kujilisha kila siku kwa siku kadhaa (katika tabianchi za joto). Halijoto za juu au za chini sana huvuruga mwenendo wa kawaida.

Upitishaji wa pathojeni[hariri | hariri chanzo]

Ingawa virusi na pathojeni nyingine zinaweza kuenezwa kwa kunguni, huzipitisha kwa vidusiwa wao mara chache. O. vicarius ni vekta ya virusi kadhaa, lakini hauawi na virusi hizi. Trypanosoma cruzi, tripanosomi ambayo husababisha ugonjwa wa Chagas, inapitishwa kwa nadra kutoka kunguni mpaka popo, lakini hakuonwa ikiongezeka tena baada ya kupitishwa. Virusi za UKIMWI na hepatitisi B zinaweza kuendelea katika kunguni wa Ulaya kwa muda wa wiki mbili, lakini bila virusi ziongezeke. Uwezekano wa virusi hizi na nyingine takriban zote kupitishwa kutoka kunguni wa Afrika mpaka wanadamu huzingatiwa kuwa mbali sana.

Spishi kadhaa za Afrika[hariri | hariri chanzo]