Bungo-lengelenge

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Bungo-lengelenge
Bungo-lengelenge madoa-kumi-na-mbili (Hycleus lugens)
Bungo-lengelenge madoa-kumi-na-mbili (Hycleus lugens)
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Arthropoda (Wanyama wenye miguu yenye viungo)
Nusufaila: Hexapoda (Wanyama wenye miguu sita)
Ngeli: Insecta (Wadudu)
Ngeli ya chini: Pterygota (Wadudu wenye mabawa)
Oda: Coleoptera (Wadudu wenye mabawa magumu)
Nusuoda: Polyphaga
Familia ya juu: Tenebrionoidea
Familia: Meloidae
Gyllenhaal, 1810
Ngazi za chini

Nusuamilia 4:

Bungo-lengelenge ni mbawakawa wa familia Meloidae katika familia ya juu Tenebrionoidea ya oda Coleoptera ambao wanaweza kusababisha malengelenge ngozini wakishikwa.

Bungo-lengelenge ni wororo kulika mbawakawa wengine. Miguu ni mirefu na kichwa kikubwa chenye shingo nyembamba. Pronoto (kidari) ni nyembamba mbele kuliko nyuma. Urefu wao ni sm 0.5-5. Idadi ya hatua za lava wao inatofautiana kulingana na spishi na hali za mazingira. Hatua ya kwanza (triungulini) ni nyembamba yenye miguu mirefu kiasi na hutembea sana ili kutafuta chakula. Hatua za pili hadi tano au sita ni aina ya buu wenye miguu mifupi. Hatua ya sita au saba ni sawa na hiyo lakini ngozi inakuwa ngumu. Pia misuli inazorota na upumuaji unapungua mpaka kiwango cha chini sana (diaposi au usinziaji). Hatua hii huokoka majira ya baridi au ya ukame mara nyingi na inaweza kukaa hai kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja. Spishi nyingine huokoka kama mayai, triungulini au wapevu.

Wakifikiri kwamba wanatishwa bungo hawa hutoa kiowevu chenye kemikali inayosababisha malengelenge (cantharidin). Wanyama wanaowakula au kuwameza kwa nasibu huugua mara nyingi na hata wanaweza kufa, k.m. farasi wanaokula nyasi kavu yenye bungo-lengelenge. Malengelenge ngozini hupona katika siku kadhaa kwa kawaida.

Wapevu wa bungo hawa hula maua kwa kawaida lakini wengine hula majani pia. Kinyume na hii lava wa spishi nyingi zaidi hula majana ya nyuki na wale wa spishi nyingine hula mayai ya panzi. Bungo-lengelenge hutaga mayai yao juu ya au karibu na maua na kwa hivyo lazima triungulini wapate njia ya kuingia ndani ya koloni ya nyuki. Basi wanaingia katika ua na wanangoja mpaka nyuki anafika ili kula mbochi. Halafu wanashika manyoya ya nyuki na akirudi koloni yake triungulini wanatafuta mahali wanapokaa majana na wanaanza kujilisha nao. Lava wanaokula mayai ya panzi wanatafuta vizibo vya povu juu ya vibumba vya mayai, kisha wanaingia ili kula mayai hayo.

Spishi zilizochaguliwa za Afrika ya Mashariki[hariri | hariri chanzo]

  • Cyaneolytta granulipennis
  • Epicauta albovittata
  • Epicauta hirticornis
  • Epicauta velata
  • Hycleus apicicornis
  • Hycleus dicinctus
  • Hycleus dubiosus
  • Hycleus lugens
  • Hycleus lunatus
  • Hycleus sjoestedti
  • Hycleus vestitus
  • Mylabris bifasciata
  • Mylabris phalerata
  • Psalydolytta flavicornis


Picha[hariri | hariri chanzo]