Yosefu (babu)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Yosefu akitangazwa waziri wa Misri katika mchoro wa miaka ya 1900.

Yosefu (kwa Kiebrania יוֹסֵף, Yossef au Yôsēp̄; kwa Kiarabu, kwa mfano katika Qur'an, jina hilo linaandikwa يوسف, Yūsuf) ni jina la mtoto wa kiume wa kumi na mmoja wa Yakobo Israeli na babu wa kabila mojawapo la Israeli lililoitwa kwa jina lake mwenyewe, au kwa kawaida zaidi liligawanyika pande mbili: kabila la Manase na kabila la Efraimu kufuatana na majina ya watoto wake wawili wa kiume.

Tangu kale anaheshimiwa na baadhi ya Waorthodoksi na Waorthodoksi wa Mashariki kama mtakatifu.

Sikukuu yake huadhimishwa tarehe 4 Septemba, lakini pia 26 Mei na 31 Julai.

Katika Kitabu cha Mwanzo[hariri | hariri chanzo]

Kama kawaida ya mitara, kulikuwa na upendeleo na wivu kati ya watoto wa Yakobo. Hasa Yosefu alichukiwa na kaka zake wote 10, ingawa alikuwa mnyofu hata kuwasimulia ndoto zake za ajabu (Mwa 37:2-11).

Kijicho na chuki vilifikia hatua ya kuwafanya watamani kumuua. Walipopata nafasi walifanya njama, ingawa si wote. Mwisho uamuzi ukawa kumuacha hai lakini kumuuza kama mtumwa kwa wafanyabiashara walioelekea Misri (Mwa 37:12-36).

Lakini katika maovu ya binadamu Mungu akazidi kulishughulikia taifa lake teule. Hivyo Yosefu akawa mfano wa Yesu ambaye alichukiwa bure tu, akauawa msalabani kwa wokovu wa wadogo zake wakosefu.

Mwa 39 inaonyesha jinsi Yosefu alivyozidi kumtiii Mungu na kukwepa dhambi. Hivyo baada ya majaribu mbalimbali akatukuzwa kuwa liwali wa Farao kwa nchi yote, hasa kwa usimamizi wa akiba ya chakula (Mwa 41:1-49) kwa ajili ya miaka saba ya njaa aliyotabiri itafuata.

Kadiri ya mpango wa Mungu njaa hiyo ikawalazimisha kaka zake waje kumuinamia, naye hakulipa kisasi; halafu, kama vile alivyotafsiri ndoto mbalimbali, aliwafafanulia maana ya matukio ya maisha yao katika mpango wa Mungu: kwamba ndiye aliyemtuma Misri kusudi awaokoe (Mwa 45:1-15).

Mwa 46:1-7 inasimulia Yakobo na wazawa wake wote, jumla wanaume 70, walivyohamia Misri. Lakini hawakusahau nchi waliyoahidiwa na Mungu: ndiyo sababu Yakobo na Yosefu walidai waapiwe kuwa watakuja kuzikwa kwao (Mwa 49:29-50:26).

Kabla ya kufa Yakobo aliwabariki watoto wake 12, akiwemo wa mwisho wao (Benyamini), na kwa namna ya pekee Yuda ambaye atatawala moja kwa moja (Mwa 49:8-12).

Katika Kurani[hariri | hariri chanzo]

Yosefu pamoja na baba yake Yakobo na kaka zake nchini Misri, Istanbul, Uturuki (1583).

Yosefu ("Yusufu") anahesabiwa na Waislamu kama nabii (Qur'an, sura vi. 84, xl. 34), na kati ya manabii wote, habari za maisha yake tu zinachukua sura nzima Yusufu (sura) (sura xii.).

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mtu wa Biblia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Yosefu (babu) kama habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.