Waamuzi (Biblia)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kitabu cha Waamuzi ni cha saba katika orodha ya vitabu vya Tanakh (Biblia ya Kiebrania) na vya Agano la Kale katika Biblia ya Kikristo.

Kinaleta mapokeo mbalimbali kuhusu historia ya Israeli kwenye miaka 1200-1025 hivi K.K.

Kama vitabu vingine vyote vya Biblia, hiki pia kinatakiwa kisomwe katika mfululizo wa historia ya wokovu ili kukielewa kadiri ya maendeleo ya ufunuo wa Mungu kwa binadamu.

Baada ya makabila 12 ya Waisraeli kugawana nchi takatifu, kila moja likaanza kujitegemea: lakini bila ya umoja hakuna nguvu upande wa dini wala wa siasa.

Upande wa dini, Waisraeli wakaanza kuchanganyikana na wenyeji Wapagani na kufuata utamaduni wao uliostaarabika zaidi, hata wakaabudu miungu yao kwa ukahaba wa kidini na kwa kuitolea sadaka watoto wao.

Kutokana na makosa hayo, Mungu akawaacha wanyanyaswe na makabila mbalimbali.

Mara kwa mara Waisraeli wakamlilia, naye akawainulia mwanamume au mwanamke fulani awashinde maadui na kuwarudishia amani (Amu 2:6-19).

Watu wa namna hiyo wanaitwa “waamuzi” kwa maana ya “watawala”.

Mmojawao ni Gideoni aliyedumisha amani kwa miaka 40. Alipoitwa na Mungu alijitetea kwa kusisitiza udogo na ufukara wake, lakini akajaliwa ishara zote alizoziomba ili kuhakikishiwa msaada (Amu 6:11-24,36-40). Sura ya 7 inasimulia Mungu alivyopunguza askari wake ili ionekane wazi kuwa ushindi ni wa Mungu mwenyewe, hautegemei uhodari na wingi wa watu au silaha zao. Ni kawaida ya kazi ya Mungu kuonyesha uweza wake katika udhaifu wa binadamu. Waisraeli walipotaka Gideoni awe mfalme wao, akakataa katakata ili Bwana tu aendelee kuwatawala (Amu 8:22-23), lakini wazo hilo likaendelea kuenea, ingawa wengine walilipinga (Amu 9:1-21).

Yaliyomo

[hariri] Mazingira

Kitabu cha Waamuzi kinashughulika na matukio ya Israeli wakati wa miaka mia mbili hivi baada Yoshua kuiteka nchi ya Kanaani. Chini ya Yoshua Waisraeli walishinda vita vile vikubwa, lakini watu hawakutii amri ya Mungu ya kuwaangamiza Wakanaani wote. Matokeo yake, Wakanaani waliobaki nchini kila wakati walisababisha matatizo katika Israeli, kwa upande wa dini na kwa upande wa siasa pia.

Wakati ule katika historia ya Israeli hali fulani iliingia ambayo habari zake tunaweza kuzisoma katika kitabu cha Waamuzi mara kwa mara. Baada ya muda, Waisraeli walimwacha Mungu wao wakaiga desturi za dini za kipagani za Wakanaani, wakawa dhaifu upande wa siasa, na mwisho wakashindwa na Wakanaani au na mataifa ya jirani. Lakini Mungu, aliyewatumia maadui wale ili kuwaadhibu watu wake waliomwasi, alivumilia sana katika neema yake. Kila mara, kwa wakati wake mwenyewe, aliwapa kiongozi na mwokozi aliyeitwa kutoka miongoni mwa Waisraeli ambaye aliwashinda maadui na kuwaongoza Waisraeli ili wamtambue Mungu wao tena.

Watu wale walioleta wokovu waliitwa Waamuzi, kwa sababu walitimiza uamuzi wa Mungu, wakiwashinda maadui na kuwaokoa watu wake. Wengine wasiokuwa watu wa vita, walitimiza uamuzi wa Mungu kwa njia ya kuongoza mambo ya kila siku ya watu wa Mungu kadiri ya sheria yake. Kutokana na viongozi wale, wakiwa wa kiraia au wa kijeshi, kitabu hiki kilipata jina lake.

[hariri] Waisraeli na maadui wao

Inaonekana kwamba vita mabalimbali vya mataifa ya jirani na ushindi wake, na mapinduzi ya baadaye yaliyoletwa na Waamuzi wa Israeli, mara nyingi zaidi yalikuwa katika sehemu fulani ya nchi tu, bila ya kuingia katika nchi yote ya Kanaani. Kwa kawaida makabila yaliyohusika yalikuwa yale ya maeneo yao tu. Pia iliwezekana kwamba ushindi na mashambulio yake yalikuwa sehemu mbalimbali kwa wakati mmoja. Kwa mfano, habari za Yefta na Waamoni ziliweza kuwa zimetokea wakati ule ule ambao Samsoni alishughulika na Wafilisti (taz. 10:7-8; 11:5; 13:1). Haukuwepo umoja sana katika Israeli, na kila kabila, au hata makundi ya makabila fulani, yaliangalia mambo yaliyotokea katika maeneo yao, bila kujali mambo ya makabila mengine.

Sababu kuu ya ukosefu ule wa umoja ilikuwa kwamba, watu walikuwa wamemwacha Mungu, kwa sababu kama wangalimfanya Yeye kuwa mkuu na sehemu ya katikati ya maisha yao ya kitaifa, uaminifu wao kwa Mungu ungaliwaunganisha. Matengano yao yalikuwa mabaya zaidi, kwa sababu hawakuwaangamiza maadui wote. Ngome za Wakanaani (pamoja na askari zake waliobaki sehemu mbalimbali za maana) zilizuia umoja wa makabila ya Israeli. Katika nchi yenyewe ya Kanaani (yaani eneo la kati ya Mto Yordani na Bahari ya Kati), makabila ya Israeli yalikuwa katika makundi makubwa matatu, yaani ya kaskazini, ya katikati na ya kusini, ambapo makabila ya mashariki yalitengwa na makabila mengine na Mto Yordani.

Matengano yale ya makabila ya Israeli hayakuwa ya kisiasa au ya kieneo tu, bali pia yalileta shida kwa umoja wa kidini, kwa sababu watu wengi walitengwa na mahali maalumu pa kuabudia, yaani hema la kukutania lililokuwepo Shilo (Yos 18:1; 22:9). Kwa kifupi, matatizo yote ya Waisraeli, yakiwa ya maendeleo, ya kisiasa au ya kidini, yalitokana na ukosefu wa watu wa kutii amri ya Mungu ya kuwaangamiza Wakanaani kabisa (taz.1:21, 27-36; Kum 7:2-4; 9:5; Yos 24:14-24).

[hariri] Dini za Wakanaani

Miungu ya Wakanaani ilijulikana kwa jina la Baalim au Mabaali (wingi wa Baali; taz. 2:11; 10:10; 1 Fal 16:31), na miungu ya kike iliitwa Maashtorethi (wingi wa Ashtorethi; taz. 2:13; 1 Sam 7:3-4), na Asherimu au Ashera (wingi wa Ashera; taz. 6:25-26; 2 Fal 23:4; kumbuka pia 'Uasherati'). Miungu ile ilikuwa ya kustawisha uzazi wo wote, pia iliaminiwa kuwa ingeweza kuongeza ustawi wa mimea. Waisraeli walijua kwamba Mungu alikuwa Mwumbaji wa hali yote ya uzazi na ustawi, na hivyo ilikuwa hatua ndogo tu kwa Waisraeli kuunganisha na kuchanganya mawazo ya Kikanaani na ujuzi wao wenyewe, na hivyo kumwabudu Yahweh kama Baali mwingine. Maana ya neno 'baali' ilikuwa bwana, mume, au mwenyewe. Waisraeli walimjua Yahweh (Yehova) kuwa Mume na Bwana wao, kwa hiyo walikuwa katika hatari zaidi ya kuunganisha Mabaali wa Kikanaani na Mungu wao aliye Yahweh (Hos 2:5-10).

Mahali ambapo Wakanaani walipenda kuendesha ibada yao ya Mabaali na Asherimu palikuwa katika vilele vitakatifu vya milima mbalimbali palipoitwa 'palipoinuka' au 'mahali pa juu' (Hes 33:51-52; 2 Fal 23:13). Baadhi ya vitu vilivyotumiwa mahali pale vilikuwa miti mitakatifu na nguzo za mawe matakatifu vilvyoitwa Maashera (au Ashera, mungu wa kike ambaye vitu vile vilichukua jina lake; taz. 6:25-26; 1 Fal 14:23). Tangu mwanzo Waisraeli walikuwa wamemwabudu Mungu mahali mbalimbali katika milima (taz. Mwa 22:2; Kut 17:8-15; 19:3), na hapo pia ilikuwa rahisi kuteleza na kuchukua sehemu za juu za Mabaali na kuzitumia kwa ibada zao za Yahweh. Mambo hayo yote yalifanyika, ingawa Mungu alikuwa ameamuru kwamba sehemu zote za ibada ya Mabaali zibomolewe kabisa (Hes 33:52; Kum 12:2-3).

Makahaba wa kike na wa kiume walipatikana katika 'mahali pa juu' kwa ajili ya sherehe mbalimbali za uzazi na ustawi wa nchi. Sherehe zile zilikuwa za kidini nao waliamini kwamba sherehe hizo za kuingiliana kimwili zingestawisha nafaka, mifugo yo yote na hata maisha ya kifamilia (1 Fal 14:23-24; Yer 13:27). Katika kuyafuata mambo ya Mabaali, watu wa Israeli walikuwa na hatia ya zinaa ya kidini pia. Agano baina ya Waisraeli na Mungu lilifananishwa na kufungwa ndoa, na hivyo Waisraeli walipojiunga na Mabaali na miungu mingine, walifanya dhambi ya zinaa (taz. 2:12-13, 17; Yer 2:20; 3:6-8; Hos 2:13; 4:12).

[hariri] Yaliyomo

1:1-2:10 Muhtasari wa ushindi wa Yoshua

2:11-16:31 Utawala wa Waamuzi

17:1-21:25 Machafuko katika Israeli

[hariri] Viungo vya nje

Vitabu vya Agano la Kale

Mwanzo Kutoka Walawi Hesabu Kumbukumbu Yoshua Waamuzi Ruthu Samueli I Samueli II Wafalme I Wafalme II Mambo ya Nyakati I Mambo ya Nyakati II Ezra Nehemia TobitiDK YudithiDK Esta Wamakabayo IDK Wamakabayo IIDK Yobu Zaburi Methali Mhubiri Hekima DK SiraDK Wimbo Bora Isaya Yeremia Maombolezo BarukuDK Ezekieli Danieli Hosea Yoeli Amosi Obadia Yona Mika Nahumu Habakuki Sefania Hagai Zekaria Malaki - Alama ya DK inaonyesha vitabu vya deuterokanoni visivyopatikana katika matoleo yote ya Biblia.