Ukanda wa visayari

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Ukanda wa asteroidi)
Ukanda wa visayari (nukta nyeupe) uko kati ya njia za Mrihi na Mshtarii. Unateganisha sayari za ndani (Utaridi, Zuhura, Dunia, Mirihi) na sayari za nje (Mshtarii, Zohali,Uranus, Neptun)
Kisayari 951 Gaspra ni kisayari cha kwanza kilivyopigwa picha kwa karibu na chombo cha angani; ina urefu wa km 18 na upana wa km 10, unene wa km 6-8

Ukanda wa visayari (Kiing. asteroid belt) ni mviringo wa visayari au miamba mikubwa na midogo na vumbi unaozunguka jua kati ya njia za Mirihi na Mshtarii katika mfumo wa jua letu. Umbali wake na jua ni eneo kati ya 2 hadi 3.4 vizio astronomia.

Gimba kubwa katika ukanda huo ni 1 Seresi ambayo ni sayari kibete.

Sayari za Utaridi (Mercury) hadi Mirihi (Mars) zilizopo ndani ya ukanda huu huitwa "sayari za ndani"; sayari zilizoko nje ya ukanda kutoka jua kuanzia Mshtarii (Jupiter) hadi Neptuni huitwa "sayari za nje".

Idadi ya magimba ya ukanda haihesabiki lakini mengi ni madogo sana. Vipande vilivyohesabiwa ni kama 400,000. Gimba la pekee linaloonekana kwa macho bila darubini ni 4 Vesta kwa sababu uso wake unaakisisha nuru nyingi kushinda kisayari kingine hata kushinda sayari kibete Seresi.

Masi ya ukanda wote huhesabiwa kuwa takriban asilimia 5 ya masi ya mwezi wa dunia yetu. Zaidi ya nusu ya masi hii ya visayari vya ukanda ni magimba 4 makubwa ambayo ni sayari kibete Seresi na visayari vikubwa vya 4 Vesta, 2 Pallas na 10 Hygiea. Zote 4 huwa na kipenyo kinachozidi kilomita 400. Yote mengine ni madogo zaidi hadi kuwa punje za vumbi tu. Lakini densiti ya masi ya ukanda si kubwa na vyombo vya angani kadhaa vimeshapita ukanda bila kugongana na vipande vyake.