Sudan Kusini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Jamhuri ya Sudan Kusini (Kiswahili)
Bendera ya Sudan Kusini Nembo ya Sudan Kusini
(Bendera ya Sudan Kusini) (Nembo ya Sudan Kusini)
Lugha rasmi Kiswahili Kiingereza
Mji Mkuu Juba
Mji Mkubwa Juba
Serikali Jamhuri
Rais Salva Kiir Mayardit
Eneo km² 619,745
Idadi ya wakazi 10,975,927 (2018)
Wakazi kwa km² 18
Uchumi nominal Bilioni $3.194
Uchumi kwa kipimo cha umma $246
Pesa Pauni ya Sudan Kusini
Kaulimbiu "Haki, Uhuru, Mafanikio"
Wimbo wa Taifa South Sudan Oyee!
Sudan Kusini katika Afrika
Saa za Eneo UTC +3 (Wakati wa Afrika Mashariki)
Mtandao .ss
Kodi ya Simu +211

Sudan Kusini (jina rasmi: Jamhuri ya Sudan Kusini) ni nchi huru iliyojitenga rasmi na Sudan tarehe 9 Julai 2011, ikiwa ni ya 54 katika bara la Afrika na ya 193 duniani.

Nchi mpya[hariri | hariri chanzo]

Hatua hiyo ilitokana na kura ya mwezi wa Januari 2011, ambako wakazi wa Sudan Kusini walipiga kura juu ya swali la kujitenga na Sudan wakaamua karibu kwa kauli moja (98.83%) kuwa nchi huru. Tofauti kubwa kati ya pande hizo ilikuwa kwamba katika Sudan yenyewe idadi kubwa ya watu wamekuwa Waislamu na utamaduni wao una mchaganyiko wa tabia za Kiarabu na Kiafrika pamoja na usambazaji mkubwa wa lugha ya Kiarabu. Kumbe kusini kuna Waislamu wachache, wengi ni wafuasi wa dini za jadi au ni Wakristo. Kiuchumi na kielimu kusini wako nyuma sana kulingana na kaskazini.

Nchi ina muundo wa shirikisho.

Tangu upatikane uhuru, nchi imeendelea kuvurugwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe na kwa sasa inashika nafasi ya kwanza katika orodha ya nchi dhaifu.

Mji mkuu ni Juba, wenye wakazi 1.118.233.

Imepakana na Sudan kaskazini, Ethiopia mashariki, Kenya, Uganda, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kusini, na Jamhuri ya Afrika ya Kati upande wa magharibi.

Inakadiriwa kwamba Sudan Kusini ina wakazi 12,340,000 (2015), lakini kutokana na ukosefu wa sensa kwa miongo kadhaa, makisio haya yaweza kuwa si sahihi.

Uchumi unategemea kilimo vijijini na cha kujikimu, lakini mwanzoni mwa mwaka 2005, uchumi alianza mpito wa kutoka vijijini na mijini katika Sudan Kusini kumeonekana maendeleo kupindukia.

Mnamo Machi 2016 nchi imefaulu kujiunga na Jumuia ya Afrika Mashariki kama mwanachama wa sita.

Historia[hariri | hariri chanzo]

John Garang, aliyekuwa Rais wa kwanza wa Sudan Kusini kabla ya uhuru na Makamu wa kwanza wa Rais wa Sudan, baada ya kuongoza wanamgambo wa Sudan ya Kusini kupigania uhuru wa majimbo ya kusini.

Kuna nyaraka chache sana za historia ya mikoa ya kusini mpaka mwanzo wa utawala wa Misri upande wa kaskazini mapema 1820 na baadaye kuendelezwa kwa biashara ya utumwa kuingia kusini.

Kabla ya wakati huo, habari zote zinapatikana kwa misingi ya historia simulizi. Kulingana na mila hizo, watu wa Niloti (Wadinka, Nuer, Shilluk) na wengine waliingia kusini mwa Sudan kwa mara ya kwanza wakati fulani kabla ya karne ya 10.

Katika kipindi cha kati ya karne ya 15 na karne ya 19, uhamiaji wa makabila, hasa kutoka eneo la Bahr al Ghazal, ulileta watu hawa katika maeneo yao ya sasa. Makabila yasiyo Niloti yaani Waazande, ambao waliingia Sudan Kusini katika karne ya 16, waliunda jimbo kubwa zaidi katika kanda hii.

Katika karne ya 18, watu wa Avungara waliingia na kwa haraka wakaweka mamlaka yao juu ya Waazande. Utawala wa Avungara ulikaa kwa muda bila kupingwa mpaka kuwasili kwa Waingereza mwishoni mwa karne ya 19. Vizuizi vya kijiografia viliwalinda watu wa kusini kutokana na kuenea kwa Uislamu, na kuwawezesha kurejesha turathi zao za kijamii na kitamaduni na urithi wao wa kisiasa na taasisi za kidini.

Misri, chini ya utawala wa Khedive Ismail Pasha, ilijaribu kwa mara ya kwanza kuikoloni kanda hiyo katika miaka ya 1870, na kuanzisha jimbo la Equatoria katika sehemu ya kusini. Gavana wa kwanza wa Misri alikuwa Samwel Baker, aliyeanza kuhudumu mwaka 1869, akifuatiwa na Charles George Gordon mwaka 1874 na Emin Pasha mnamo 1878.

Maasi ya Mahdist ya miaka ya 1880 yaliuyumbisha mkoa huu mchanga, na Equatoria ilikoma kuwepo kama milki ya Misri mwaka 1889. Makazi muhimu katika Equatoria yalikuwa pamoja na Lado, Gondokoro, Dufile na Wadelai.

Sudan Kusini ilitawaliwa kama eneo la pekee wakati wa ukoloni wa Kiingereza hadi 1947 ilipounganishwa na kaskazini kama nchi moja bila kuwauliza wenyeji.

Wakati wa uhuru wa Sudan mwaka 1956 viongozi wa kusini walidai haki ya kujitawala ndani ya taifa jipya, lakini mapatano yalishindikana na hali hiyo ilisababishwa kutokea kwa vita ya Anyanya kati ya 1956 na 1972.

Baada ya kipindi cha amani, vita vilianza upya mwaka 1983 wakati kanali John Garang alipounda SPLA dhidi ya badiliko la Sudan kutangazwa nchi ya Kiislamu.

Vita hivyo vya pili vilikwisha mwaka 2005 kwa mkataba wa amani ulioacha kusini kama sehemu ya kujitawala ndani ya Sudan hadi ipigwe kura juu ya swali la kujitenga iliyopangwa kwa mwaka 2011.

Nchi imeathiriwa vibaya na vita mbili za Anya-nya na pia Vita ya Pili ya Wenyewe kwa Wenyewe ya Sudan iliyopiganaiwa na harakati ya SPLA kwa karibu miaka 21 dhidi ya serikali ya Khartoum. Vita hiyo ilileta uharibifu mkubwa na kusababisha kuhama lwa watu wengi kutoka makazi yao.

Zaidi ya watu milioni 2.5 wameuawa, zaidi ya milioni 5 kuachwa bila makao na wengine kuwa wahamiaji wa ndani, na kuwa wakimbizi kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe na sababu zingine zinazohusiana na vita.

Baada ya kifo cha John Garang, majeshi ya Southern Sudan Army na South Sudan Defense Force (SSDF) yalisitisha uhasama wao na kuungana mnamo Januari 2006, chini ya Azimio la Juba. SSDF ilianzishwa na Makamu wa Rais wa sasa wa Sudan Kusini, Dkt. Riek Machar.

Chini ya Azimio la Juba, Jenerali Matip akawa Naibu Kamanda Mkuu wa Jeshi la Sudan Kusini, na vikosi vyake vya SSDF kuingizwa katika Jeshi la Sudan Kusini, na kuongezea safu yake kutoka 50,000 hadi 309,000. Jumla ikawa askari 359,000. Wote sasa ni jeshi moja linalojulikana kama Jeshi la Sudan Kusini.

Jenerali Oyay Deng Ajak aliteuliwa kuwa Ofisa-mkuu-wa-Watumishi wa Jeshi la Sudan Kusini, hadi Mei 2009 wakati alipompisha Meja Jenerali James Hoth Mai[1].

Mbali na Katiba ya Mpito ya Jamhuri ya Sudan [2], Katiba ya Mpito ya Sudan Kusini ya 2005 iliwekwa kuwa sheria kuu [3] ya Sudan Kusini.

Katiba imeweka Tawi Kuu linaloongozwa na Rais ambaye ni Mkuu wa Nchi, Mkuu wa Serikali, na Kamanda Mkuu wa Sudan People's Liberation Army. John Garang, mwanzilishi wa SPLA / M alikuwa Rais wa kwanza hadi kifo chake tarehe 30 Julai 2005.

Salva Kiir Mayardit, naibu wake, aliapishwa kama Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan na Rais wa Serikali ya Sudan Kusini tarehe 11 Agosti 2005. Riek Machar aliingia mahala pake kama Makamu wa Rais.

Nguvu za kuunda sheria ziko mikononi mwa serikali na Bunge la pamoja la Sudan Kusini.

Katiba pia imeweka mahakama huru, chombo cha juu kabisa kikiwa Mahakama Kuu.

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Picha ya nchi kutoka satelaiti.
Majimbo 10 ya Sudan Kusini yalivyotokana na wilaya 3 za Sudan      Bahr el Ghazal      Equatoria      Greater Upper Nile.
Majimbo 28 yaliyotangazwa mwaka 2015.

Hadi mwaka 2020 nchi ilikuwa na majimbo 32:

  1. Aweil
  2. Aweil East
  3. Eastern Lakes
  4. Gogrial
  5. Gok
  6. Lol
  7. Tonj
  8. Twic
  9. Wau
  10. Western Lakes
  11. Amadi
  12. Gbudwe
  13. Imatong
  14. Jubek
  15. Maridi
  16. Kapoeta
  17. Tumbura
  18. Terekeka
  19. Yei River
  20. Boma
  21. Central Upper Nile
  22. Akobo
  23. Northern Upper Nile
  24. Jonglei
  25. Latjoor
  26. Maiwut
  27. Northern Liech
  28. Ruweng
  29. Southern Liech
  30. Bieh
  31. Fashoda
  32. Fangak

Maeneo matatu ya Milima ya Nuba, Abyei na Nile ya Buluu kiutamaduni na kisiasa ni sehemu za Sudan Kusini lakini kwa mujibu wa CPA yatakuwa na utawala tofauti mpaka kura ya maoni ambayo ifanyike juu ya kujiunga na Sudan Kusini au kubaki chini ya utawala wa Sudan. Lakini kuna wasiwasi kama Sudan itaitisha kura za namna hiyo.

Baada ya hapo, Sudan Kusini inajumuisha majimbo kumi ambayo kihistoria yanaunda mikoa mitatu ya Bahr el Ghazal, Equatoria, na Nile ya juu.

Idadi ya Watu[hariri | hariri chanzo]

Mwanamke mzawa.
Nyumba za kijijini.

Inakubaliwa na wengi kuwa kabila kubwa zaidi Sudan Kusini ni Wadinka (15%), ikifuatiwa na Wanuer (10%) kisha Wabari, Waazande, Washilluk. Makabila mengine ni Waacholi, Wamurle, Wanubi, Wakuku, Wafunj, Wamaban, Wazandi, Waoduk na mengineyo.

Sensa ya Tano ya Watu na Makazi ya Sudan (2008)[hariri | hariri chanzo]

"Sensa ya Tano ya Watu na Makazi ya Sudan" nzima, ilifanywa mwezi Aprili 2008. Hata hivyo matokeo ya sensa yalikataliwa na viongozi wa Sudan ya Kusini kwa makisio kuwa "Ofisi kuu ya Takwimu mjini Khartoum ilikataa kutoa takwimu za kitaifa za sensa ya Sudan kwa kituo cha Sudan kusini cha Sensa, takwimu na tathmini." [4]

Sensa ya Sudan Kusini ilionyesha kuwa idadi ya watu ilikuwa million 8.26[5] hata hivyo Rais Salva Kiir "alishuku kuwa takwimu zilikuwa zinapunguzwa katika baadhi ya maeneo na kuongezwa katika mengine, na hivyo kufanya Hesabu ya mwisho "kutokubalika"." [6]

Alidai pia kuwa idadi ya watu wa Sudan Kusini ilikuwa thuluthi moja ya watu wa Sudan, ilhali sensa ilionyesha kuwa ni asilimia 22 pekee[5].

Ilisemekana pia kuwa watu wengi wa Sudan Kusini hawakuhesabiwa "kutokana na hali ya hewa mbaya, hali mbaya ya mitandao ya mawasiliano na usafirishaji, na baadhi ya maeneo yalikuwa hayafikiki, na watu wengi kutoka Sudan Kusini walikuwa uhamishoni katika nchi jirani na kupelekea 'matokeo yasiyokubalika', kulingana [na] mamlaka ya Sudan Kusini[6].

Mshauri Mkuu wa kiufundi wa Marekani wa sensa ya Kusini pia alisema wasajili wa sensa pengine walifikia asilimia 89 pekee ya wakazi[7].

Sensa mpya[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 2009 Sudan ilianza upya sensa ya Sudan Kusini kabla ya kura ya maoni ya uhuru wa Sudan Kusini, 2011, ambayo ilisemekana pia kujumuisha Wanasudan Kusini walio nchi zingine.

Hata hivyo harakati hii ilikashifiwa kwani iliziacha nje nchi zenye idadi kubwa ya watu kutoka Sudan Kusini, na badala yake kuhesabu nchi ambapo idadi hii ilikuwa ndogo[8].

Kadirio la mwaka 2016 ni kwamba wakazi ni 12,230,730[9].

Lugha[hariri | hariri chanzo]

Sudan Kusini inajumuisha zaidi ya makabila 200 yakizungumza lugha 60 zinazopatikana hasa katika Sudan ya Kusini na nyingine kutoka nchi jirani za Kenya, Ethiopia, Uganda, Kongo, Sudan (Khartoum) na nyingine (angalia Orodha ya lugha za Sudan Kusini).

Lugha rasmi ni Kiingereza, pamoja na kutambulika kwa lugha mbalimbali za mitaa katika majimbo au miji. Kiswahili kinapangiwa kuenezwa nchini, hasa baada ya Sudan Kusini kujiunga na Jumuia ya Afrika Mashariki.

Lugha tatu kubwa za Kiafrika zinazotumika Sudan Kusini ni Kithongjieng (wazungumzaji 3,000,000), Kithok Naadh (wazungumzaji 1,599,000), na Kishilluk (zaidi ya wazungumzaji 1,000,000).

Kinuer kinazunguzmwa katika Bentiu, Nasir, Akobo, Maywuut nk na Shilluk inazunguzmwa katika Upper Nile au katika Ufalme wa Shilluk; Kiarabu cha Juba kinazunguzmwa karibu katika kila sehemu ya Sudan Kusini lakini hasa katika majimbo ya Equatoria Mashariki, Equatoria Magharibi na Bahr el Jabel.

Lugha za Wanubi zinazungumzwa sana katika milima ya Jimbo la Nuba.

Lugha ya Kiuduk huzungumzwa na watu wa Uduk, na pia baadhi ya majirani zao.

Kima cha uwezo wa kusoma katika Sudan Kusini mwaka 2006 kilikuwa kinakadiriwa kufikia asilimia 37 kwa wanaume, 12 kwa wanawake au 24 kwa jumla kama wastani.

Dini[hariri | hariri chanzo]

Watu wa Sudan kusini hujihusisha zaidi na Ukristo na dini asilia za Kiafrika (32.9%).

Ukristo una wafuasi takriban asilimia 60.5 za wakazi wa Sudan Kusini, wengi wakiwa wa Kanisa Katoliki na Anglikana, yakiwemo pia Wakalvini na madhehebu mengine mengi madogo zaidi[10].

Uislamu unafuatwa na 6.2%.

Uchumi[hariri | hariri chanzo]

Sehemu kubwa ya bajeti ya Serikali inatoka katika pesa za mafuta. Mafuta na rasilimali nyingine za madini za Sudan Kusini zinaweza kupatikana karibu kila mahali, lakini Bentiu inajulikana kama jimbo lenye utajiri wa mafuta.

Mafuta[hariri | hariri chanzo]

Katika miaka ya hivi karibuni, uchimbaji wa kiasi muhimu na makampuni ya kigeni umeanza huko Sudan Kusini, na kuinua hadhi yake ya kijiografia na ya kisiasa. Khartoum ilipogawanya Sudan katika vitalu, takriban asilimia 85 ya mafuta zilitoka Kusini.

Vitalu 1, 2, na 4 hudhibitiwa na kampuni kubwa zaidi kutoka ng'ambo, inayoitwa Greater Nile Petroleum Operating Company (GNPOC).

Vitalu vingine vinavyotoa mafuta katika Kusini ni vitalu 3 na 7 katika Upper Nile ya Mashariki.

Kitalu kingine muhimu cha Kusini, kiitwacho Kitalu B, kinadaiwa na wadau kadhaa. Total ya Ufaransa ilipatiwa kandarasi ya kitalu hicho chenye kilomita mraba 90,000 katika miaka ya 1980 lakini tangu wakati huo imefanya kazi chache huku ikidai "force majeure". Vipengele mbalimbali vya SPLM vilitoa kitalu hiki au sehemu zake kwa wadau wengine wa Sudan Kusini. Mikataba kadhaa kama hii iliyofanywa kabla ya Naivasha ilidhalilishwa wakati kiongozi wa SPLM / A John Garang de Mabior alipoondoka mamlakani.

Sehemu ya CPA kuhusu ugavi wa mali inasema kwamba mikataba yote iliyotiwa saini kabla ya CPA itasalia; haitakuwa kuangaliwa upya na Tume ya Kitaifa ya Mafuta (NPC), tume iliyoanzishwa na CPA na inayojumuisha Khartoum na wawakilishi wa kusini na uenyekiti wa ushirikiano baina ya Rais Al-Bashir wa Khartoum na Rais Kiir wa Sudan Kusini. Hata hivyo, CPA haielezi bayana nani ana uwezo wa kutia saini mikataba ya kabla ya CPA.

Pande zote mbili za Khartoum na Sudan Kusini zimewahi kujaribu kudai uwezo wa kutia saini makubaliano chini ya haki ya "self determination" iliyopewa upande wa kusini ambayo ilitangaza mnamo 19 Septemba 2009 katika nchi zaidi ya 105 duniani kote.

Hali ya binadamu[hariri | hariri chanzo]

Sudan Kusini ilikiri kuwa na baadhi ya viashiria vya afya vibaya zaidi duniani[11]. [12]

Mwaka 2004, kulikuwa na madaktari wapasuaji watatu tu kutumikia Sudan Kusini yote, na hospitali sawa tatu, na katika baadhi ya maeneo hayo kuna daktari mmoja tu kwa kila watu 500,000[11].

Kufikia wakati wa Mkataba Mwafaka wa Amani wa 2005, mahitaji ya kiutu katika Sudan Kusini yalikuwa makubwa. Hata hivyo, mashirika ya kibinadamu chini ya uongozi wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) yaliweza kuhakikisha kuna fedha za kutosha kuleta nafuu kwa wakazi. Pamoja na misaada ya dharura na maendeleo, miradi ya kibinadamu ilijumuishwa katika Mpango wa Kazi wa 2007 wa Umoja wa Mataifa na washirika wake.

Mnamo 2007, OCHA (chini ya uongozi wa Eliane Duthoit) ilianza awamu ya kumalizia Kusini mwa Sudan mahitaji ya kibinadamu polepole lakini kwa kugeuka juu ya udhibiti wa kufufua na maendeleo ya shughuli za NGOs na mashirika ya kijamii. [13]

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. http://www.newsudanvision.com/index.php?option=com_content&view=article&id=1715:developing-story-major-general-james-hoth-mai-appointed-spla-new-chief-of-staff & Itemid = 6
  2. Interim National Constitution of the Republic of Sudan, 2005.
  3. Interim Constitution of Southern Sudan of 2005.
  4. "South Sudan parliament throw outs census results", SudanTribune, 8 Julai 2009. Retrieved on 2010-01-02. Archived from the original on 2014-07-12. 
  5. 5.0 5.1 Fick, Maggie. "S. Sudan Census Bureau Releases Official Results Amidst Ongoing Census Controversy", !enough The project to end genocide and crimes against humanity, 8 Juni 2009. 
  6. 6.0 6.1 Birungi, Marvis. "Southern Sudanese officials decry ‘unfortunate’ announcement of census results", The New Sudan Vision, 10 Mei 2009. Retrieved on 2010-01-02. Archived from the original on 2011-07-14. 
  7. Thompkins, Gwen. "Ethnic Divisions Complicate Sudan's Census", NPR, 15 Aprili 2009. 
  8. "South Sudan says Northern Sudan's census dishonest", Radio Nederland Wereldomroep, 6 Novemba 2009. Retrieved on 2010-01-02. Archived from the original on 2011-07-24. 
  9. "World Population Prospects: The 2017 Revision". ESA.UN.org (custom data acquired via website). United Nations Department of Economic and Social Affairs, Population Division. Retrieved 10 September 2017.
  10. Christianity in Southern Sudan. Hope for the Future International.
  11. 11.0 11.1 Ross, Emma (28 Januari 2004). Southern Sudan as unique combination of worst diseases in the world Archived 8 Aprili 2014 at the Wayback Machine.. Sudan Tribune .
  12. Moszynski, Peter (23 Julai 2005). Conference plans rebuilding of Southern Sudan's health service. BMJ .
  13. SUDAN: Peace bolsters security in the south. IRIN. 18 Aprili 2007.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Coordinates: 4°51′N 31°36′E / 4.850°N 31.600°E / 4.850; 31.600

Nchi za Afrika Bara la Afrika
Afrika ya Kati (Jamhuri ya) | Afrika Kusini | Algeria | Angola | Benin | Botswana | Burkina Faso | Burundi | Cabo Verde | Chad | Cote d'Ivoire | Eritrea | Eswatini | Ethiopia | Gabon | Gambia | Ghana | Guinea | Guinea Bisau | Guinea ya Ikweta | Jibuti | Kamerun | Kenya | Komori | Kongo (Jamhuri ya) | Kongo (Jamhuri ya Kidemokrasia ya) | Lesotho | Liberia | Libya | Madagaska | Malawi | Mali | Misri | Morisi (Visiwa vya) | Mauritania | Moroko | Msumbiji | Namibia | Niger | Nigeria | Rwanda | Sahara ya Magharibi | Sao Tome na Principe | Senegal | Shelisheli | Sierra Leone | Somalia | Sudan | Sudan Kusini | Tanzania | Togo | Tunisia | Uganda | Zambia | Zimbabwe
Maeneo ya Afrika ambayo ni sehemu za nchi nje ya Afrika
Hispania: Kanari · Ceuta · Melilla | Italia: Pantelleria · Pelagie | Ufaransa: Mayotte · Réunion | Uingereza: · St. Helena · Diego Garcia | Ureno: Madeira
Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Sudan Kusini kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.