Shirika la Kimataifa la Nishati ya Nyuklia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Bendera ya IAEA
Jiji la UM pamoja na maao makuu ya IAEA huko Vienna, Austria


Shirika la Kimataifa la Nishati ya Nyuklia (International Atomic Energy Agency (IAEA)) ni mamlaka ya kujitawala ya kimataifa inayoshirikiana na Umoja wa Mataifa (UM). Ilianzishwa tar. 29 Julai 1957 na nchi 81 wanachama wa UM.

Hata kama si moja kwa moja chini ya katiba ya UM inatoa taarifa zake kwa Mkutano Mkuu wa UM na Baraza la Usalama la UM.

Madhumuni[hariri | hariri chanzo]

Shabaha ya IAEA imekuwa tangu mwanzo matumizi ya nishati ya nyuklia yanayolingana na amani. Hapa imepewa madaraka ya kuangalia vituo vya kinyuklia katika nchi zote, kusaidia upanuzi wa teknolojia ya kinyuklia isiyo ya kijeshi na usalama wa matumizi ya nishati ya nyuklia. Shabaha muhimu ni pamoja na kuzuia uenezaji wa silaha za nyuklia.

IAEA ni shirika la kimataifa linalopaswa kuangalia masharti ya mkataba wa kuzuia usambazaji wa silaha za nyuklia wa 1968.

Muundo[hariri | hariri chanzo]

IAEA ina mikono mitatu:

  • Mkutano Mkuu mwenye wawakilishi wa nchi wanachama 144 unakaa mara moja kila mwaka. Unakubali bajeti na kuamua juu ya maswali yanayowekwa mbele yake na halmashauri, na mkurugenzi mkuu au na wanachama wenyewe.
  • Halmashauri ya Magavana inakaa mara tano kila mwaka na kufanya maazimio kuhusu mwelekeo wa kazi ya shirika; huwa na magavana 22 wanaochaguliwa na mkutano mkuu kwa muda wa miaka 2 halafu na magavana 13 wanaochaguliwa upya kila mwaka na halmashauri yenyewe.
  • Ofisi Kuu inaongozwa na Mkurugenzi Mkuu pamoja makamu wake sita. Chini yao kuna wafanyakazi 2,200 pamoja na wanasayansi, mahandisi, watawala na wasaidizi. Mkurugenzi Mkuu tangu 1997 ni Mmisri Mohamed ElBaradei.

Kazi inatekelezwa katika idara sita za utawala, sayansi ya nyuklia na matumizi yake, nishati nyuklia, usalama wa nyuklia, ushirikiano wa kiteknolojia na usimamizi wa vituo vya kinyuklia duniani.

Makao makuu yapo kwenye Jiji la UM huko Vienna (Austria). Ofisi za kanda zipo Toronto and Tokyo, halafu kuna ofisi ndogo kwenye makao ya UM huko New York na Geneva. IAEA ina pia maabara ya uchunguzi katika Seibersdorf (Austria) na Monako.

Mafanikio na matatizo[hariri | hariri chanzo]

Udhaifu mmojawapo wa IAEA ni katiba ya kwanza inayodai kibali cha nchi wanachama kwa uchunguzi wa hali ya vituo vya nyuklia katika nchi hizi. Kwa njia hii nchi kadhaa ziliweza kuficha jitihadi zao za kuunda silaha za kinyuklia. Kwa sababu hiyo kuna mapatano mapya inayoruhusu wachunguzi wa IAEA kuingia katika maabara na taasisi ziote zinazoshughulikia mambo ya nyuklia wakati wowote. Ila tu haya mapatano mapya yalikubaliwa na nchi 73 pekee hadi 2006.

IAEA pamoja na mkurugenzi Mohamed ElBaradei ilipokea tuzo ya Nobel ya Amani mwaka 2005. Tuzo hili lilitolewa kwa sababu IAEA ilijitahidi kuzuia uvamizi wa Irak mwaka 2001.

Wataalamu wa UM walikuwa wametambua maabara ya kinyuklia nchini Irak yaliyofichwa kinyume na masharti ya mkataba wa kuzuia usambazaji wa silaha za nyuklia. Katika miaka kabla ya uvamizi wa Irak na Marekani IAEA ilifaulu kuchunguza maabara na ofisi nyingi hadi Irak haikuwa tena na utafiti wa kuunda silaha za nyuklia isipokuwa serikali ya Marekani haikuamini taarifa za IAEA na kushambulia Irak hata hivyo. Kamati ya Nobel iliamua ya kwamba IAEA ilijitahidi kuzuia matumizi ya kijeshi ya nishati ya nyuklia na kujenga matumizi salama ya nishati hii.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Tovuti rasmi ya IAEA Archived 25 Oktoba 2012 at the Wayback Machine.