Salibu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Salibu (en:Crux)
Ramani ya Crux - Salibu

Salibu (kwa Kiingereza: en:Crux, au Southern Cross [1]) ni kundinyota mashuhuri yenye umbo la msalaba kwenye angakusi inayoonekana kutoka nusutufe ya kusini ya Dunia. Salibu lipo kati ya kundinyota zinazotambuliwa kirahisi[2]. Ni kundinyota dogo lakini nyota zake kuu zina uangavu mzuri wa mag 2.8 au zaidi.

Mahali pake

Salibu lipo katika sehemu angavu ya njia nyeupe karibu na Kantarusi (kundinyota) (Centaurus) inayopakana nayo kwa pande tatu. Upande wa kusini lipo Nzi (en:Musca).

Jina

Jina "Salibu"[3] latokana na Kiarabu صليب ṣaliib ambalo ni tafsiri ya kilatini Crux inayomaanisha "msalaba". Jina lilibuniwa na mabaharia kutoka Ulaya walipoanza kuzunguka kwenye nusutufe ya kusini ya Dunia baada ya safari ya Magellan wakafurahi kuona ishara ya dini yao angani.

Nyota zake zilionekana tayari kwa Klaudio Ptolemaio miaka 2,000 iliyopita akazihesabu kuwa sehemu ya Kantarusi (Centaurus). Kutokana na badiliko la mwelekeo wa mhimili wa Dunia nyota zake hazionekani tena katika nusutufe ya kaskazini. Johann Bayer alipotunga orodha yake ya nyota bado alizieleza kama sehemu za Kantarusi alipomrejelea Ptolemaio. Lakini jina la Crux lilianza kuenea baadaye na kubaki.[4].

Magimba ya angani

Ndani ya eneo la Salibu kuna nyota 49 zinazoonekana kwa macho matupu lakini hasa zile nne angavu zaidi zinazounda umbo la msalaba au "Salibu". Hizi nyota nne zinajulikana kama Acrux, Becrux au Mimosa, Gacrux na Decux ambayo ni mafupisho ya majina marefu yaani Alfa, Beta, Gamma na Delta Crucis.

Gacrux inaonekana kwa darubini ndogo kuwa nyota maradufu lakini hali halisi nyota zake mbili zina umbali wa miakanuru 160 kati yao kwa hiyo zinaonekana tu kama nyota maradufu. Nyota kubwa inayoonekana kwa macho ni jitu jekundu chenye umbali wa miakanuru 88 kutoka Dunia.

Tanbihi

  1. Uhusika milikishi (en:genitive) ya neno "Crux" katika lugha ya Kilatini ni "Crucis" na hili ni umbo la jina linaloonekana katika majina ya nyota za kundi hili kama vile Alfa Crucis, nk.
  2. The Constellations, tovuti ya International Astronomical Union , iliangaliwa Julai 2017
  3. Salibu ni umbo la jina linatokana na na Jan Knappert - taz. Marejeo
  4. Linganisha Allen, Names of Stars, uk. 185 ff

Marejeo

  • Richard Hinckley Allen: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 184f (online kwenye archive.org)
  • Jan Knappert, 1993: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331