Pasaka ya Kikristo

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa matumizi tofauti ya jina hili angalia Pasaka, pia Pasaka ya Kiyahudi na Kipindi cha Pasaka

Picha takatifu ya Ufufuko, ikimuonyesha Kristo akiwa amevunja milango ya kuzimu na kutoa Adamu na Eva nje ya makaburi. Kristo anazungukwa na watakatifu, huko Shetani, aliyechorwa kama mzee, amefungwa kwa minyororo.
Mwaka wa Kanisa kadiri ya kalenda ya liturujia ya Roma kama kielelezo cha kawaida kwa Ukristo wa magharibi.
Mwaka wa liturujia
Magharibi
Mashariki

Pasaka ya Kikristo ni sikukuu ambayo Wakristo karibu wote hufanya kila mwaka ukumbusho wa kufufuka kwake Yesu Kristo siku ya tatu baada ya kusulubiwa, kufa na kuzikwa kwake.

Umuhimu wake

Inahesabiwa kuwa sikukuu muhimu kabisa katika madhehebu mengi ya Ukristo, kwa sababu ufufuko huo ndio msingi wa imani ya Kikristo. Mtume Paulo aliandika kwamba Kristo asingefufuka, imani hiyo ingekuwa haina maana, kwa kuwa asingeondolea dhambi za watu.

Pamoja na kifo cha Yesu, ndio kiini cha kanuni ya imani ya Wakristo wa kwanza kama alivyoipokea Paulo mwenyewe alipoongoka miaka sita baada ya matukio hayo. Katika Waraka wa kwanza kwa Wakorintho aliandika:

15:1 Basi, ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, 2 na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri isipokuwa mliamini bure. 3 Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; 4 na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; 5 na ya kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; 6 baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; 7 baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; 8 na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake. 9 Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. 10 Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami. 11 Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini.

12 Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu? 13 Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka; 14 tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure. 15 Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. 16 Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. 17 Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. 18 Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea. 19Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote.

20 Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala. 21 Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu. 22 Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa. 23 Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, atakapokuja. 24 Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. 25 Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. 26 Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti. 27 Kwa kuwa, Alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake. Lakini atakaposema, Vyote vimetiishwa, ni dhahiri ya kuwa yeye aliyemtiishia vitu vyote hayumo. 28 Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.

Jina la Pasaka

Jina la "Pasaka" limetokana na sherehe ya Pasaka ya Kiyahudi linaloitwa "פסח" (tamka: pasakh) kwa lugha ya Kiebrania. Kinyume cha Kiingereza, ambacho kina maneno mawili, Passover na Easter, katika Kiswahili na lugha nyingine nyingi majina ya sherehe za Kikristo na Kiyahudi hazitofautiani.

Asili yake ni kwamba kusulibiwa na kufufuka kwa Yesu Kristo kumetokea wakati wa sikukuu ya Pasaka ya Kiyahudi mnamo Aprili ya mwaka 30 BK.

Wakristo wa kwanza, ambao wote walikuwa Wayahudi, walisheherekea sikukuu ya Kiyahudi pamoja na kumbukumbu ya ufufuko wa Yesu. Baadaye sherehe na pia tarehe zikawa tofauti, ingawa bila kwenda mbali sana. Badiliko kubwa zaidi lilikuwa lile la Wakristo kuadhimisha daima Pasaka siku ya Jumapili kwa kuwa ndiyo siku ya ufufuko, wakati Wayahudi wanadhimisha Pasaka kwa kuangalia tarehe, bila kujali ni siku ipi ya juma.

Tarehe ya Pasaka

Tarehe za Pasaka kwa miaka 2000-2040
(Tarehe zote zinaonyeshwa kufuatana na kalenda ya Gregori)
Jumapili ya Pasaka
kuanzia 2000 hadi 2040
Mwaka Ukristo wa Magharibi
(Kalenda ya Gregori)
Ukristo wa Mashariki
(Kalenda ya Juliasi)
2000 23 Aprili 30 Aprili
2001 15 Aprili
2002 31 Machi 5 Mei
2003 20 Aprili 27 Aprili
2004 11 Aprili
2005 27 Machi 1 Mei
2006 16 Aprili 23 Aprili
2007 8 Aprili
2008 23 Machi 27 Aprili
2009 12 Aprili 19 Aprili
2010 4 Aprili
2011 24 Aprili
2012 8 Aprili 15 Aprili
2013 31 Machi 5 Mei
2014 20 Aprili
2015 5 Aprili 12 Aprili
2016 27 Machi 1 Mei
2017 16 Aprili
2018 1 Aprili 8 Aprili
2019 21 Aprili 28 Aprili
2020 12 Aprili 19 Aprili
2021 4 Aprili 2 Mei
2022 17 Aprili 24 Aprili
2023 9 Aprili 16 Aprili
2024 31 Machi 5 Mei
2025 20 Aprili
2026 5 Aprili 12 Aprili
2027 28 Machi 2 Mei
2028 16 Aprili
2029 1 Aprili 8 Aprili
2030 21 Aprili 28 Aprili
2031 13 Aprili
2032 28 Machi 2 Mei
2033 17 Aprili 24 Aprili
2034 9 Aprili
2035 25 Machi 29 Aprili
2036 13 Aprili 20 Aprili
2037 5 Aprili
2038 25 Aprili
2039 10 Aprili 17 Aprili
2040 1 Aprili 6 Mei

Tarehe ya Pasaka inafuata kuonekana kwa mwezi angani, kwa hiyo sikukuu hiyo haina tarehe imara katika kalenda ya kawaida. Inapatikana katika Machi au Aprili. Pasaka haifuati mwezi pekee lakini tarehe yake imefungwa pia kwa sikusare (au ekwinoksi), kwa hiyo haiendelei kuzunguka mwaka wote kama tarehe za Kalenda ya Kiislamu.

Mtaguso wa kwanza wa Nisea mwaka 325 uliamua ya kwamba Pasaka itasheherekewa Jumapili ya kwanza baada ya mwezi mpevu wa kwanza baada ya 21 Machi (tarehe ya sikusare machipuo ambayo ni siku ya usawa wa mchana na usiku, hivyo mwanzo wa majira ya kuchipua kaskazini mwa dunia). Kwa kuwa mwezi mpevu baada ya 21 Machi inaweza kutokea kati ya 22 Machi na 19 Aprili, tarehe ya Pasaka, ambayo ni Jumapili inayofuata, hutokea kati ya 22 Machi na 25 Aprili.

Katika Ukristo kuna kalenda mbili zinazotumika, hivyo pia tarehe mbili za Pasaka. Kanisa la magharibi, yaani Wakatoliki wengi na Waprotestanti, hufuata Kalenda ya Gregori (ambayo imekuwa kalenda ya kawaida ya kimataifa), lakini Waorthodoksi wanaendelea kutumia kalenda iliyotangulia, yaani Kalenda ya Juliasi. Ndiyo maana mara nyingi Pasaka inaendelea kuadhimishwa katika Jumapili tofauti kati ya pande hizo mbili. Hata hivyo kuna majadiliano yenye lengo la kufikia makubaliano ili kuadhimisha Pasaka pamoja. Kwa sasa tofauti ya kalenda inaleta Kanisa la Mashariki kusheherekea Pasaka wakati mwingine hata katika mwezi wa Mei wa kalenda ya Gregori, ingawa kwao bado ni Aprili kufuatana na kalenda ya Juliasi.

Tanbihi

Viungo vya nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Liturujia
Mapokeo
Hesabu
Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Pasaka ya Kikristo kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.