Mvua ya mawe

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Matone ya mvua ya mawe.
Kipande kikubwa cha barafu (kipenyo chake ni sentimeta 6) kilichotokea kwa kuungana kwa matone madogo zaidi hewani

Mvua ya mawe (kwa Kiingereza hail) ni aina ya mvua ambayo matone ya maji yamefika kwenye uso wa ardhi kwa umbo la vipande vya barafu. Inatokea wakati matone ya maji ya mvua yanapita kwenye hewa baridi na kuganda hadi kuwa barafu.

Hali halisi mvua inayonyesha si mawe bali vipande vya barafu.

Tone zito zaidi lililowahi kupimwa lilinyesha sehemu za Gopalganj (Bangladesh) tarehe 14 Aprili 1986, likiwa la kilogramu 1.02[1]. Kericho nchini Kenya penye mvua ya radi mara nyingi[2] ni mahali ambako mvua ya mawe inanyesha zaidi kushinda sehemu nyingine za Dunia[3].

Mchakato wa kutokea kwa mvua ya mawe[hariri | hariri chanzo]

Mvua ya mawe hutokea kwenye sehemu za chini za mawingu ya mvua ya radi. Sehemu za mawingu hayo zinapatikana katika hali baridi kiasi chini ya sentigredi sifuri.

Hapo matone madogo ya maji yanaweza kupatikana kwa hali baridi kiasi chini ya sentigredi sifuri lakini hayajaganda. Yakigusana katika hali hii na matone mengine huganda mara moja. Mara nyingi vipande vidogo vya barafu vinavyotokea hivyo huanza kuanguka na kuwa maji tena vikifika chini kama matone ya kawaida ya mvua.

Lakini mara nyingi kuna miendo ya hewa ya kuzunguka ndani ya mawingu ya mvua ya radi na hivyo vipande vidogo vya barafu vinaweza kurushwa juu. Katika mwendo huu hugusana na matone mengine ya maji baridi sana yanayoganda mara moja wakati wa kuguswa na hivyo kukuza kipande cha barafu. Kipande cha barafu kinainuliwa na upepo wa kupaa hadi kimefikia uzito wa kutosha au nguvu ya upepo wa kwenda juu inafifia. Hapo kinaanza kuanguka.

Kama masi ya barafu inatosha haiwezi kuyeyuka wakati wa kupita kwenye hewa yenye joto juu ya sifuri, hivyo inafika ardhini kama mvua ya mawe. Kutegemeana na uzito wake, vipande vya barafu vinaweza kusababisha uharibifu hata kuua watu na mifugo.

Katika Biblia[hariri | hariri chanzo]

Katika Kitabu cha Kutoka mvua ya mawe ni moja kati ya mapigo 10 yaliyowapata Wamisri wakati wa Musa.

Baadaye mvua ya mawe inatajwatajwa sehemu mbalimbali za Biblia kama ajabu la Mungu linalompatia sifa.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. World heaviest hailstone, tovuti ya Arizona State university. Anguko la mvua ya mawe ile liliua pia watu huko Bangla Desh.
  2. Ouma Fred Ogutu: Thunderstorm frequency over the Western Rift - Valley and Lake Victoria region of Kenya and its relation to aviation industry 10/1278/2012, tovuti ya University of Nairobi, Department of Meteorology, 2016
  3. What places in the world have the most hail in one year. Jalada kutoka ya awali juu ya 2017-10-17. Iliwekwa mnamo 2018-02-20.
Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mvua ya mawe kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.