Mecklenburg

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Bendera ya Mecklenburg
Mecklenburg 1815–1934

Mecklenburg (tamka mek-len-bug) ni eneo katika kaskazii ya Ujerumani. Zamani ilikuwa utemi wa kujitegemea chini ya Dola Takatifu la Kiroma na leo hii ni sehemu ya jimbo la Mecklenburg-Vorpommern. Miji mikubwa zaidi ni Rostock, Schwerin, Neubrandenburg na Wismar.

Asili ya jina[hariri | hariri chanzo]

Jina latokana na maneno "mikil" iliyomaanisha "kubwa" katika lahaja ya Kisaksoni ya kale na "burg" inayomaanisha "boma" kwa hiyo maana yake ni "boma kubwa". Boma hili lilikuwepo kati ya miji ya Schwerin na Wismar likawa boma la familia ya watawala wa eneo hili.

Eneo na wakazi[hariri | hariri chanzo]

Mecklenburg ina eneo la 15,721 km². Nchi ni tambarare hakuna milima, na sehemu za juu znafikia mita 179 juu ya uwiano wa bahari. Kuna maziwa mengi madogo, misitu na hasa mashamba mengi. Upande wa kaskazini Mecklenburg inapakana na bahari ya Baltiki.

Wakazi ni wachache na tangu karne ilikuwa eneo lenye msongamano mdogo wa wakazi katika Ujerumani.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Mipaka ya Mecklenburg mnamo 1300
Albrecht II, Mtemi wa Mecklenburg mnamo 1348

Habari za hakika juu ya historia ya Mecklenburg zinaptikana tangu mnamo mwaka 1,000. Wakati ule nchi ilikaliwa na makabila ya Kislavoni waliofuata dini za asili. Kabila kuwa lilijulikana kama Obodriti na tangu mwaka 1160 lilikubali ubwana wa juu ya watawala wa kisaksoni wa Ujerumani ya kaskazni-maharibi. Chifu Pribislav wa Waobodriti alikuwa mtawala wa kwanza wa kienyeji aliyekubaliwa kama mtemi ndani ya muundo wa Ujerumani na mwaka 1167 alipokea imani ya Kikristo.

Tangu mwaka 1200 walowezi Wajerumani kutoka sehemu za magharibi walianza kufika kwa wengi wakaunda miji na vijiji. Katika karne zilizofuata wenyeji na walowezi waliunganika kiutamaduni. Kijerumani kilichukua nafasi ya lugha za Kislavoni za wazalendo asilia. Tofauti na maeneo mengine ya Ujerumani ya Mashariki yaliyowahi kukaliwa na Waslavoni nasaba ya watawala wa kienyeji iliendelea kutawala hadi mwaka 1918 ambako ufalme ulikwisha kote Ujerumani.[1].

Sehemu za pwani zilishambuliwa mara kwa mara na Waskandinavia na miji kadhaa ya pwani yalikuwa chini ya Denmark au Uswidi kwa muda fulani. Kwa jumla miji yenye bandari kwenye pwani la Baltiki ilijiunga na maungano ya miji ya Hanse.

Utemi wa Mecklenburg ulitawaliwa mara kadhaa kati ya matawi mbalimbali ya nasaba ya watemi wake lakini baadaye sehemu hizi ziliunganika tena kwa hiyo kwa jumla wakazi walijisikia wako pamoja kama Mecklenburg moja.

Wakati wa matengenezo ya kiprotestanti katika karne ya 16 watawala wa utemi na serikali za miji waliamua kujiunga na kanisa la Kiluteri kama sehemu kubwa ya Ujerumani ya kaskazini kwa jumla.

Mwanzoni mwa karne ya 19 Mecklenburg ilitwaliwa na Ufaransa chini ya Napoleon Bonaparte lakini baada ya kushindwa kwake mwaka 1815 madola 2 ya Mecklenburg yenye miji mikuu ya Schwerin na Strelitz zilirudishwa na kudumu hadi 1918, tangu 1871 kama sehemu ya Dola la Ujerumani. Mwaka 1918 wakati wa mapinduzi ya Ujerumani baada ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia zilikuwa jamhuri zikaunganika mwaka 1934.

Baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia Mecklenburg ikawa sehemu ya kanda la Kisovyeti la Ujerumani na tangu 1949 jimbo la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kijerumani yaani sehemu ya kikomunisti ya Ujerumani. 1952 majimbo ya Ujerumani ya Mashariki yalifutwa nchi ikagawiwa kwa mikoa. Baada ya mwisho wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kijerumani jimbo likaundwa upya na pamoja na mabaki ya mabaki ya jimbo la Pomerania likawa jimbo la Mecklenburg-Vorpommern ambalo likajiunga na Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Katika maeneo mengine watawala wa asili ya Kislavoni walipinduliwa na Wajerumani wenyewe