Mapenzi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mikono miwili ikiunganika kutengenezea umbo la moyo.
Sehemu ya mfululizo wa makala kuhusu mapendo

Moyo katika mapokeo ya Ulaya
ni mchoro unaowakilisha mapendo.
Vipengele Msingi
Mapendo kadiri ya sayansi
Mapendo kadiri ya utamaduni
Upendo (fadhila)
Upendo safi
Kihistoria
Mapendo ya kiuchumba
Mapendo ya kidini
Aina za hisia
Mapendo ya kiashiki
Mapendo ya kitaamuli
Mapendo ya kifamilia
Mapendo ya kimahaba
Tazama pia
Mafungamano ya binadamu
Jinsia
Tendo la ndoa
Maradhi ya zinaa
Siku ya wapendanao

Mapenzi ni neno la Kiswahili linalojumlisha idadi kadhaa ya hisia, kuanzia mahaba, pendo hadi upendo wa Kimungu.

Ni kwamba kitenzi "kupenda" kinaweza kurejelea aina za hisia, hali na mitazamo tofautitofauti, kuanzia ridhaa ya jumla ya kitu ("Napenda chakula hiki"), hadi mvuto mkali kati ya binadamu ("Nampenda mume wangu"). Uanuwai wa matumizi na maana, pamoja na utata wa hisia zinazohusika, hufanya kuwe na ugumu katika ufafanuzi, hata kulingana na hali nyingine za kihisia.

Kidhahania, mapenzi kwa kawaida yanarejelea hisia za ndani, zisizoelezeka, za kudumu kwa mwingine, yakishirikisha hisia tofauti, kutoka hamu na urafiki wa kimahaba hadi ukaribu wa kihisia wa kifamilia na kitaamuli, usioelekea kabisa ngono[1] na hata umoja wa kina au ibada ya upendo wa kidini. [2]

Mapenzi katika aina zake mbalimbali husimamia mafungamano na, kutokana na umuhimu wake mkuu katika saikolojia, ni mojawapo ya maudhui yanayopatikana sana katika sanaa.

Ufafanuzi[hariri | hariri chanzo]

Mapenzi ya kindugu (250-900 BK). Jumba la ukumbusho la Anthropolojia katika Xalapa, Veracruz, Mexico.

Wakati yanapojadiliwa kidhahania, mapenzi kwa kawaida yanarejelea pendo kati ya watu, hisia alizonazo mtu kuhusu mtu mwingine. Ingawa desturi au chanzo cha mapenzi ni suala ambalo hujadiliwa mara kwa mara, sura tofauti ya neno hili zinaweza kuwekwa wazi kwa kuamua nini si mapenzi:

  • kama njia ya kawaida ya kuonyesha hisia chanya (aina kubwa ya kupenda), mapenzi kwa kawaida hugonganishwa na chuki (au kutojali);
  • kama pendo ambalo linaegemea zaidi kwenye uhusiano wa kirafiki kuliko wa kingono, mapenzi kwa kawaida hugonganishwa na tamaa; na
  • kama uhusiano kati ya watu, unaohusisha mahaba, mapenzi hugonganishwa na urafiki, ingawa neno mapenzi linaweza kutumika pia kwa urafiki wa karibu katika miktadha fulanifulani.

Neno la Kiingereza "love" linaweza kuwa na maana zinazohusiana lakini tofauti kadiri ya miktadha. Kumbe, lugha nyingine huweza kutumia maneno mbalimbali kueleza dhana tofauti ambazo Kiingereza hutumia neno "love" tu kurejelea; mfano mmoja ni wingi wa maneno ya Kigiriki yanayorejelea "mapendo".

Tofauti za utamaduni katika kufafanua mapenzi, hufanya liwe jambo gumu kutoa ufafanuzi wowote. [3]

Aidha, mawazo kuhusu mapenzi yamebadilika sana kadiri ya wakati. Baadhi ya wanahistoria wanahusisha dhana za kisasa za mapenzi ya kimahaba na Ulaya wakati au baada ya Karne za Kati, ingawa kuwepo kwa mahusiano ya kimahaba kabla ya wakati huo kunaonyeshwa na ushairi wa kimapenzi wa kale. [4]

Kuna mithali kadhaa kuhusu mapenzi, mojawapo ikiwa ile ya Vergilio ya kuwa "Pendo hushinda yote" na ile ya kundi la Beatles "All you need is love" (Unachohitaji ni mapenzi tu).

Mwanafalsafa Gottfried Leibniz alisema mapenzi ni "kuwa na furaha tele kutokana na furaha ya mwingine." [5]

Mapenzi yasiyohusu mtu maalum[hariri | hariri chanzo]

Mtu anaweza kusema anapenda nchi, kanuni au shabaha maalumu ikiwa anaithamini sana na kuizingatia kwa makini.

Vilevile, katika huduma za huruma na kazi za kujitolea "upendo" wa kazi unaweza kutokana na mapenzi yasiyohusishwa na kitu pamoja na utu na imani za kisiasa badala ya mapenzi kati ya watu.

Watu pia wanaweza "kupenda" vitu, wanyama, au shughuli ikiwa watajitolea kujihusisha na vitu vile. Kukiwa na tamaa ya kingono pia, hali hiyo inaitwa parafilia.[6]

Mapenzi kati ya watu[hariri | hariri chanzo]

Wapenzi Romeo na Julieta walivyochorwa na Frank Dicksee.

Mapenzi kati ya watu wawili ni hisia za nguvu kuliko kumpenda mwingine kwa jumla.

Mapenzi yasiyotuzwa ni hisia za mapenzi ambazo haziwezi kulipwa au kurudishwa. Mapenzi kama hayo yanaweza kuwepo kati ya wanafamilia, marafiki, na wanandoa. Pia kuna matatizo kadhaa ya kisaikolojia yanayohusiana na mapenzi.

Tangu kale historia, falsafa na dini ndizo taaluma ambazo zimewaza sana suala la mapenzi.

Katika karne ya 20, sayansi ya saikolojia imeandika mambo mengi juu ya suala hili.

Katika miaka ya karibuni, saikolojia ya mabadiliko, biolojia ya mabadiliko, anthropolojia, sayansi ya nyuro na biolojia zimezidisha ufahamu juu ya mapenzi.

Msingi wa kikemia[hariri | hariri chanzo]

Biolojia ya jinsia huona mapenzi kama hisia za mamalia, sawa na njaa au kiu.[7]

Helen Fisher, mtaalamu wa mada ya mapenzi, amegawa mapenzi katika sehemu tatu zinazolingana: tamaa, mvuto na pendo. Tamaa huwafunua watu kwa wengine; mvuto wa kimahaba huwahamasisha kuzingatia nguvu yao kwa kuhusiana kingono; na pendo linahusisha kustahimili mwenzako (au mtoto) kwa muda wa kutosha kumlea.

Tamaa ni hamu ya mwanzo ya ngono ambayo inaendana na kutolewa kwa wingi kwa kemikali kama vile testosterone na estrogen. Athari hizo huwa hazikai zaidi ya wiki chache au miezi michache.

Pendo ni hamu ya binafsi na ya kimahaba zaidi inayoelekezwa kwa mtu maalum wa kuhusiana kingono, ambayo hutokana na tamaa wakati wajibu kwa mtu huyo unakua.

Utafiti uliofanywa hivi karibuni na Sayansi ya nyuro umeonyesha kuwa kadiri watu wanavyoendelea kupendana, ubongo huwa unatoa aina fulani za kemikali, ikiwa ni pamoja na 'pheromones', 'dopamine', 'norepinephrine', na 'serotonin', ambazo hufanya kazi sawa na 'amphetamines', kuchochea kiini cha furaha kwenye ubongo na kusababisha ongezeko la mapigo ya moyo, kupoteza hamu ya kula na kulala, na hisia kali za msisimko. Utafiti umeonyesha kwamba hatua hiyo kwa jumla hudumu kuanzia mwaka mmoja na nusu hadi miaka mitatu. [8]

Kwa kuwa hatua za tamaa na mvuto huendelea kwa muda tu, hatua ya tatu inahitajika kuelezea mahusiano ya muda mrefu. Upendo ni maingiliano ambayo hukuza mahusiano ya kudumu kwa miaka na hata miongo mingi. Upendo kwa jumla umejengwa kwenye wajibu kama vile ndoa na watoto, au kuheshimiana kirafiki kulikojengwa kwenye mambo kama vitu mnavyovipenda. Upendo umehusishwa na kuwepo kwa viwango vya juu vya kemikali ('oxytocin' na 'vasopressin') ikilinganishwa na mahusiano ya muda mfupi. [8]

Enzo Emanuele na wenzake walieleza kuwa molekuli ya protini inayojulikana kama chanzo cha ukuaji wa neva (nerve growth factor = NGF) ina viwango vya juu wakati watu wanapoanza kupendana, lakini viwango hivyo hurudi kwenye vipimo vya awali baada ya mwaka mmoja. [9]

Msingi wa kisaikolojia[hariri | hariri chanzo]

Bibi na mjukuu, Sri Lanka.

Saikolojia inaonyesha mapenzi kama jambo tambuzi na la kijamii.

Mwanasaikolojia Robert Sternberg alibuni nadharia ya miraba mitatu ya mapenzi akasema mapenzi yana vipengele vitatu tofauti: urafiki, kujitoa, na uchu. Urafiki ni aina ambayo watu wawili huambiana siri na mambo kadhaa kuhusu maisha yao binafsi. Kuwajibika, kwa upande mwingine, ni matumaini kuwa uhusiano huo utadumu. Aina ya mwisho na inayopatikana sana ni mvuto wa kingono au uchu. Mapenzi ya uchu ni kama yanavyoonyeshwa katika kupumbazwa kimapenzi pamoja na mapenzi ya kimahaba. Aina zote za mapenzi hutazamwa kama mchanganyiko tofauti wa vipengele hivyo vitatu.

Mwanasaikolojia kutoka Marekani, Zick Rubin alijaribu kutumia saikometriki. Kazi yake inasema kuwa mapenzi yamejengwa na vipengele vitatu: upendo, kujali na urafiki. [10] [11]

Kufuatia maendeleo katika nadharia za umeme, kama vile sheria ya Coulomb ambayo ilionyesha kuwa nguvu chanya na nguvu hasi huvutiana, milinganisho katika maisha ya binadamu ilifanywa, kama vile "vitu vilivyo kinyume kuvutiana." Katika karne ya 20, utafiti juu ya mahusiano ya kingono miongoni mwa binadamu umepata kwa jumla kuwa jambo hili si kweli kuhusu tabia za watu kwa sababu hao kwa kawaida kuwapenda wale walio na sifa zinazofanana na zao. Hata hivyo, katika nyanja chache zisizo za kawaida na maalumu, kama vile mifumo ya kinga, inaonekana kwamba binadamu hupendelea binadamu ambao ni tofauti nao (mfano, walio na mfumo wa orthojoni), kwa kuwa jambo hili litasababisha kupata mtoto ambaye ana sifa bora za pande zote mbili. [12] Katika miaka ya hivi karibuni, nadharia mbalimbali za maingiliano ya binadamu zimebuniwa na kuelezewa kwa kuzingatia upendo, mahusiano, maingiliano, na mivuto.

Baadhi ya wataalamu wa Magharibi hugawanywa katika vipengele viwili vikuu, chenye utu na chenye kujipenda. Mtazamo huo umewakilishwa na Scott Peck, ambaye anasema kuwa mapenzi ni mchanganyiko wa "wasiwasi kuhusu ukuaji kiroho wa mwingine," na kujipenda sahili. [13] Kwa pamoja, mapenzi ni shughuli, si hisia tu.

Ulinganifu wa mifumo ya kisayansi[hariri | hariri chanzo]

Mifumo ya kibiolojia ya mapenzi huyatazama kama msukumo wa kimamalia, sawa na njaa au kiu[7], kumbe saikolojia huyatazama kama jambo linalotegemea zaidi jamii na utamaduni. Pengine kuna chembe za ukweli katika mitazamo yote miwili.

Hakika mapenzi huathiriwa na homoni, na jinsi watu hufikiri na kutenda katika mapenzi huathiriwa na mawazo yao kuhusu hayo. Mtazamo wa kawaida katika biolojia ni kwamba kuna misukumo miwili mikuu katika mapenzi: mvuto wa kingono na pendo. Pendo kati ya watu wazima huchukuliwa kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni sawa na zile zinazomfanya mtoto mchanga kumpenda mama yake. Mtazamo wa jadi wa kisaikolojia huangalia mapenzi kama muungano wa mapenzi ya kimwenzi na mapenzi ya kiuchu. Mapenzi ya kiuchu ni hamu kubwa, na mara nyingi huandamana na mhemko wa kimwili (kupumua kwa nguvu, mpigo wa moyo wa kasi); mapenzi ya kimwenzi ni mapenzi na hisia za kirafiki zisizoandamana na mhemko wa kimwili.

Uchunguzi umeonyesha kuwa ubongo wa waliopumbazwa na mapenzi unafanana na ule wa wenye ugonjwa wa akili. Mapenzi huanzisha shughuli katika eneo la ubongo sawa na njaa, kiu, na hamu ya madawa. Mapenzi mapya, kwa hiyo, yanaweza kuegemea upande wa mwili kuliko wa hisia. Kadiri wakati unavyopita, athari hizo zinazotokana na mapenzi hukomaa, na maeneo mbalimbali ya ubongo yanaamshwa, hasa yale yanayohusiana na ahadi za muda mrefu.

Mitazamo ya kitamaduni[hariri | hariri chanzo]

Uajemi[hariri | hariri chanzo]

Hata baada ya muda huu wote
Jua haliambii ardhi, "ninakudai."
Angalia kinachotokea na Upendo kama huo!

'

- Linaangaza mbingu nzima. (Hafiz)

Maulana Rumi, Hafez na Sa'di ni ishara za uchu na mapenzi ambazo huwasilishwa na lugha na utamaduni wa Kiajemi. Neno la Kiajemi linalorejelea mapenzi ni eshgh, lililotokana na la Kiarabu Ishq. Katika utamaduni wa Kiajemi, kila kitu kinazungukwa na mapenzi na yote huwa ni kwa ajili ya mapenzi, kuanzia kupenda marafiki na familia, mabibi na mabwana, na hatimaye kufikia upendo wa Kimungu ambao ndio lengo halisi la maisha. Zaidi ya karne saba zilizopita, Sa'di aliandika:


Watoto wa Adamu ni viungo vya mwili mmoja
Baada ya kuumbwa kwa kiini kimoja.
Wakati msiba wa wakati unaathiri kiungo kimoja
Viungo hivyo vingine haviwezi kuwa na amani.
Ikiwa hauna huruma kwa matatizo ya wengine
Wewe hustahili kuitwa kwa jina la "mtu."

China na tamaduni za jirani[hariri | hariri chanzo]

The traditional Chinese character for love (愛) consists of a heart (middle) inside of "accept," "feel," or "perceive," which shows a graceful emotion.

Ukonfusio kwa desturi ulisisitiza wajibu, mwelekeo na tendo katika uhusiano (km wema kutoka kwa wazazi, utiifu wa mzazi kutoka kwa watoto, uaminifu kwa mfalme, na kadhalika) kuliko mapenzi yenyewe. Katika kuzingatia hayo, dhana ya "mapenzi" umekuja tu hivi majuzi kutoka Magharibi. Hata hivyo, Ren (仁) inaweza kuonekana kama wema wa mapenzi, ambayo ni sehemu muhimu ya maisha ya kimaadili, na lazima ifuatwe na wote. Mozi alibuni dhana ya Ai (爱) iliyotokana na ile ya Kikonfusio Ren, ambayo inakaribiana zaidi na ile ya kimagharibi ya mapenzi bia. Badala ya kuonyesha mitazamo tofauti kwa watu tofauti, dhana ya Mohism inasisitiza kumpenda kila mtu, si marafiki au familia pekee, bila kuzingatia kama wao pia watafanya hivyo.

Katika lugha ya Kichina na tamaduni za kisasa, istilahi kadhaa hutumiwa kurejelea dhana ya mapenzi:

  • Ai (爱) ni kitenzi (km Wo Ai Ni 我爱你, au "Ninakupenda") na istilahi (kama Ai Qing 爱情, au "Mapenzi ya Kimahaba"). Neno hili ndilo ambalo linatumiwa sana kurejelea mapenzi, na linaweza kuwa na maana mbalimbali katika mazingira tofauti, kama ilivyo katika Kiingereza. Tangu mwaka 1949, eneo la Bara China limekuwa likitumia neno Ai Ren (爱人, asilia lililomaanisha "mpenzi") kama neno kuu la "mke/mume" (wakati maneno tofauti ya "bibi" na "bwana" yalidumishwa, yalikosa kusisitizwa ili kukuza usawa wa kijinsia); neno Ai Renouce lina maana dhahania hasi nchini China, jambo ambalo bado linajitokeza miongoni mwa wengi nchini Taiwan.
  • Istilahi Lian (恋) inaelezea hali kupenda na kutegemea ya mtu binafsi inayotokana na mapenzi, na kwa hivyo huwa halitumiki sana likiwa peke yake. Mara nyingi huwa linatumiwa hasa kuelezea mapenzi ya kimahaba au kingono, kama vile "kuwa katika mapenzi" (恋爱, Lian Ai), "mpenzi" (恋人, Lian Ren) au "ushoga" (同性恋, Tong Xing Lian).
  • Istilahi Qing (情), au "hisia", mara nyingi inaonyesha "mapenzi" katika muktadha sahihi. Linapotumiwa pamoja na Ai (爱) neno hili hasa huwa linatumiwa kuelezea mapenzi ya kimahaba, kama katika Ai Qing 爱情. Qing Ren (情人) ni istilali ingine inayorejelea "mpenzi", ikimaanisha kuwa kumekuwa na uhusiano wa kingono .
  • Istilahi Gănqíng (感情) inajumuisha hisia zilizoko na upendo ambao umekua kutokana na kuwa na uhusiano wa karibu. Ujenzi wa gănqíng hii, au maingiliano, kwa hivyo ni muhimu katika kuanzisha na kudumisha mapenzi.
  • Yuanfen (缘份) ni muungano wa kudura. Mwanzo wa uhusiano wa maana (uwe wa kimahaba au kirafiki) huwa unafikiriwa kuwa mara nyingi unategemea yuanfen. Mtazamo sawa na huu katika Kiingereza ni "hatima" au "kudura".

Japani[hariri | hariri chanzo]

Katika Ubudha wa Kijapani, neno ai (爱) linarejelea mapenzi ya uchu na kujali, na hamu ya msingi. Inaweza kukua kuelekea ama ubinafsi au kutokuwa na ubinafsi na kutaalamika. Amae (甘え), neno la Kijapani lenye maana ya "kujihusisha na utegemezi," ni sehemu ya utamaduni wa Ujapani wa kumlea mtoto. Akina mama wa Kijapani wanatarajiwa kukumbatia na kuendekeza watoto wao, na watoto wanatarajiwa kuwatuza mama zao kwa kuwashikilia na kuwahudumia. Baadhi ya wanasosholojia wamependekeza kuwa maingiliano ya kijamii ya Kijapani katika maisha ya baadaye yamejengeka juu ya 'amae' ya mama kwa mtoto.

Ugiriki wa kale[hariri | hariri chanzo]

Ugiriki ya Kale ina maneno mbalimbali na tofauti: philia, eros, agape, storge na xenia. Hata hivyo, imekuwa vigumu kihistoria kutofautisha kabisa maana za maneno hayo ya Kigiriki (kama ilivyo kwa lugha nyingine nyingi). Tafsiri ya Biblia ya Ugiriki ya kale ina mifano ya kitenzi agapo kikiwa na maana sawa na phileo.

Agape inamaanisha mapenzi katika Ugiriki ya sasa kisasa. Neno S'agapo linamaanisha Ninakupenda katika Kigiriki. Neno agapo ni kitenzi Ninapenda. Kwa jumla linarejelea aina ya mapenzi ambayo ni "safi", badala ya mvuto wa kimwili unaopendekezwa na eros. Hata hivyo, kuna baadhi ya mifano ya agape inayotumika kuleta maana sawa na eros. Pia imetafsiriwa kama "upendo wa nafsi."

Eros ni mapenzi ya kimahaba, yaliyo na shauku na hamu. Neno la Kigiriki erota linamaanisha katika mapenzi. Ingawa mapenzi ya eros kwa kawaida huwa yanahisiwa kwa mtu, kwa kutafakari yanakuwa ni kuthamini uzuri ndani ya mtu, au hata inakuwa ni kuthamini uzuri wenyewe. Mapenzi ya eros husaidia nafsi kukumbuka ujuzi wa uzuri na huchangia katika ufahamu wa ukweli wa kiroho. Wapenzi na wanafalsafa wote huchochewa na eros kutafuta ukweli. Baadhi ya tafsiri huyaorodhesha kama "mapenzi ya mwili."

Philia kama mapenzi ya wema yasiyo na uchu, ilikuwa ni dhana iliyobuniwa na Aristotle. Inahusisha uaminifu kwa marafiki, familia na jamii, na inahitaji wema, usawa, na kufahamiana. Philia huchochewa na kwa sababu za kiutendaji; mmoja au wawili wa wahusika kufaidika na uhusiano. Inaweza pia kumaanisha "mapenzi ya akili."

Storge ni mapenzi ya kawaida, kama wanayohisi wazazi kwa watoto wao.

Xenia (ξενία xenía), ukarimu, ulikuwa jambo muhimu sana katika Ugiriki wa kale. Ulikuwa karibu na urafiki wa kitaambiko ulioanzishwa kati ya mwenyeji na mgeni wake, ambao hapo awali wangekuwa hawafahamiani. Mwenyeji alimlisha na kumpatia mgeni malazi, na mgeni alitarajiwa kulipia kwa shukrani pekee. Umuhimu wa jambo hili unaweza kuonekana kupitia visasili vya Kigiriki, hasa vile vya Homer ambavyo ni Iliad na Odyssey.

Uturuki[hariri | hariri chanzo]

Katika Kituruki, neno "mapenzi" huwa na maana kadhaa. Mtu anaweza kumpenda Mungu, mtu, wazazi, au familia. Lakini mtu huyo anaweza "kupenda" mtu mmoja tu kutoka jinsia tofauti na yake, jambo ambalo wao hulipatia neno "aşk", yaani mapenzi kwa maana za kimahaba na kingono pekee. Ikiwa Mturuki atasema kuwa yeye anampenda (aşk) mtu, si aina ya mapenzi ambayo mtu anaweza kuhisi kwa wazazi wake, ni ya mtu mmoja tu, na inaonyesha ashiki kuu. Neno hili hupatikana kwenye lugha za Kiturki, kama zile za Azerbaijani (Esq) na Kazakh (ғашық).

Roma ya Kale (Kilatini)[hariri | hariri chanzo]

Lugha ya Kilatini ina vitenzi mbalimbali vinavyolingana na neno la Kiingereza "love." Amare ndilo neno msingi la mapenzi, na bado ndilo linalotumiwa kwenye Kiitalia hadi leo. Warumi walilitumia kurejelea uhusiano wa kirafiki na wakimahaba au kingono. Kutoka kitenzi hiki tunapata amans- mpenzi, amator, "mpenzi wa kitaalamu," mara nyingi likiwa na wazo la ziada la uzinzi - na amica, "mpenzi", na mara nyingi hutumiwa kitafsida kurejelea kahaba. Neno linalolingana ni amor (umuhimu wa neno hili kwa Warumi unaonyeshwa katika ukweli kwamba, jina la mji Rome-, katika Kilatini: Roma-linaweza kutazamwa kama anagramu ya amor, neno ambalo lilitumika kama jina la siri la mji katika duru pana nyakati za zamani), [14] na ambalo ni pia linatumika katika wingi kuashiria mahusiano ya kimapenzi na matukio ya kingono. Kutoka kwenye kiini kile bado tunapata amicus - "rafiki" na Amicitia, "urafiki" (unaojengwa kwenye ushirika, na kulingana wakati mwingine kwa karibu na "uwiwa" au "ushawishi"). Cicero aliandika makala inayoitwa de Amicitia, ambayo inazungumzia wazo hili kwa urefu fulani. Ovid aliandika mwongozo wa kupendana uitwao Ars Amatoria ambao unazungumzia, kwa kina, kila kitu kutoka masuala ya uhusiano nje ya ndoa hadi masuala ya wazazi wanaomnyima mtu uhuru.

Wakati mwingine Kilatini hutumia neno Amare katika sehemu ambazo huzua utata. Hata hivyo, katika Kilatini kwa jumla kuna maneno placere au delectāre, ambayo hutumiwa zaidi katika miktadha isiyo rasmi, na neno la mwisho la delectāre likitumiwa mara nyingi katika ushairi wa kimapenzi wa Catullus. Neno Diligere mara nyingi linazua wazo la "kuwa na upendo wa," "kuheshimu," na kwa nadra sana hutumiwa kurejelea mapenzi ya kimahaba. Neno hili linaweza kufaa kuelezea urafiki wa watu wawili. Nomino inayolingana diligentia, hata hivyo, ina maana ya "bidii" au "uangalifu," na ina uhusiano mdogo sana wa kisemantiki na kitenzi hicho. Observare ni kisawe cha diligere; licha ya kuwa na asili moja na Kiingereza, kitenzi hicho na nomino inayolingana, observantia, mara nyingi huashiria "heshima" au "upendo." Neno Caritas hutumika katika tafsiri za Kilatini za Biblia ya Kikristo kwa maana ya "upendo wenye hisani"; maana hiyo, hata hivyo, haipatikani katika maandiko ya Kirumi ya Kipagani.

Maoni ya dini[hariri | hariri chanzo]

Dini za Kiabrahamu[hariri | hariri chanzo]

"LOVE sculpture" 1977 ya Robert Indiana, 'spelling ahava in Israel'

Uyahudi[hariri | hariri chanzo]

Katika Kiyahudi, Ahava ndilo neno linalotumika sana kurejelea upendo kati ya watu na upendo wa Mungu. Uyahudi unatumia ufafanuzi mpana wa upendo, kati ya watu na kati ya mtu na Mungu. Kuhusu upendo kati ya watu, Torati inasema, "Mpende jirani yako kama ujipendavyo" (Mambo ya Walawi 19:18). Kuhusu upendo wa pili, mtu ameamuriwa kumpenda Mungu "kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote na kwa nguvu zako zote" (Kumb 6:5), zilizochukuliwa na Mishna (ufafanuzi wa sheria) za Wayahudi kurejelea mema, mtu kuwa tayari kutoa maisha yake kama dhabihu badala ya kutenda makosa fulani makubwa, mtu kuwa tayari kutoa mali yake yote kama sadaka, na kumshukuru Mungu licha ya mashaka (Berakhoth 9:5). Fasihi ya Marabi hutofautiana katika jinsi upendo huu unaweza kuendelezwa, kwa mfano, kwa kutafakari matendo ya Mungu au kushuhudia makuu yaliyoumbwa. Na kuhusu upendo kati ya washirika wa ndoa, jambo hili huchukuliwa kama kiungo muhimu cha maisha: "Ishi maisha na mke umpendaye" Kitabu cha Mhubiri 9:9). Kitabu cha Biblia Wimbo Ulio Bora huchukuliwa kama fumbo la upendo wa kindoa kati ya Mungu na taifa lake, lakini kwa kawaida wasomaji hukiona kama wimbo wa mapenzi.

Rabi Eliyahu Eliezer Dessler (karne ya 20) hunukuliwa mara nyingi kwa kufafanua upendo kwa mtazamo wa Wayahudi unaosema upendo ni "kutoa bila kutarajia kupokea" (kutoka Michtav me-Eliyahu, Vol. 1).

Ukristo[hariri | hariri chanzo]

Mapenzi matakatifu dhidi ya mapenzi ya kiulimwengu, mchoro wa Giovanni Baglione wa mwaka 1602-1603.

Uelewa wa Ukristo unasema kwamba upendo hutoka kwa Mungu. Mapenzi ya mwanamume na mwanamke ("eros" katika Kigiriki) na mapenzi yasiyo na ubinafsi kwa wengine ("agape") mara nyingi hulinganishwwa kama mapenzi ya "kupaa" na "kushuka", lakini hatimaye ni jambo moja. [15]

Kuna maneno kadhaa ya Kigiriki yanayorejelea "mapenzi" ambayo yanatajwa katika duru za Wakristo.

  • Phileo: Pia katika Agano Jipya, phileo ni itikio la binadamu kwa kitu ambacho hufurahisha. Pia yanajulikana kama "mapenzi ya kindugu."
  • Maneno mengine mawili yanayorejelea mapenzi katika lugha ya Kigiriki ambayo ni: eros (mapenzi ya kingono) na storge (mapenzi ya mtoto kwa mzazi), hayakutumika katika Agano Jipya.

Wakristo wanaamini kwamba kumpenda Mungu kwa moyo wako wote, akili, na nguvu na kumpenda jirani yako kama ujipendavyo ni mambo mawili muhimu katika maisha, amri kuu ya Torati, kulingana na mafundisho na maisha ya Yesu (taz. Injili ya Marko sura ya 12, Aya 28-34). Mtakatifu Agostino wa Hipo aliyafupisha haya alipoandika "Umpende Mungu, halafu ufanye utakavyo."

Mtume Paulo alitukuza upendo kama kitu muhimu kulilo vyote. Huku akielezea upendo katika shairi maarufu katika Waraka wa kwanza kwa Wakorintho aliandika, "Upendo huvumilia, upendo ni mwema, hauna wivu, haujivuni, hauna kiburi. Si ufidhuli, hauna majivuno, haukasirishwi kwa haraka, hauhesabu mabaya uliotendewa. Upendo haufurahii maovu bali hufurahia ukweli. Upendo daima hulinda, daima huamini, daima huwa na matumaini, na daima huvumilia." (1 Kor 13:4-7).

Mtume Yohane aliandika, "Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa Mwana wake wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwanawe ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Kila mtu amwaminiye hahukumiwi, lakini yeyote asiyemuamini tayari ana hatia kwa sababu yeye hajaamini jina la Mwana pekee wa Mungu." (Yoh 3:16-18).

Yohane pia aliandika, "Marafiki zangu, hebu tupendane kwani upendo hutoka kwa Mungu. Kila mtu anayependa amezaliwa wa Mungu na anamjua Mungu. Yeyote asiyependa hamjui Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo." (1 Yoh 4:7-8).

Mtakatifu Augustino anasema ni lazima mtu aweze kutambua tofauti kati ya upendo na tamaa. Tamaa ni kujihusisha katika jambo kupindukia, bali kupenda na kupendwa ndilo jambo ambalo amelitafuta maisha yake yote. Hata anasema, "Nilikuwa nimependana na upendo." Hatimaye, akawa anampenda Mungu na kupendwa naye. Augustino anasema kuwa yule anayeweza kukupenda kwa ukweli na ukamilifu ni Mungu, kwa sababu upendo kwa binadamu unaruhusu udhaifu kama vile "wivu, wasiwasi, hofu, hasira, na ushindani." Kulingana na Augustino, kumpenda Mungu ni "kufikia amani ambayo ni yako." (Maungamo ya Mtakatifu Augustino).

Wanateolojia Wakristo humwona Mungu kama chanzo cha upendo, ambao huonekana katika binadamu na mahusiano yao ya upendo.

Msomi mkubwa wa Biblia C. S. Lewis aliandika kitabu kinachoitwa The Four Loves.

Papa Benedikto XVI aliandika waraka wake wa kwanza kuhusu "Mungu ni upendo". Humo alisema kuwa mwanadamu, aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu ambaye ni upendo, anaweza kupenda; kujitoa kwa Mungu na wengine (agape) na kwa kupokea na kuhisi upendo wa Mungu kupitia tafakuri (Eros). Maisha haya ya upendo, kulingana na yeye, ni maisha ya watakatifu kama Bikira Maria na Mama Teresa wa Kolkata na ni mwelekeo ambao Wakristo huchukua wanapoamini kuwa Mungu anawapenda. [15]

Uislamu na Uarabu[hariri | hariri chanzo]

Kwa kiwango fulani, mapenzi hayahusishi mtazamo wa Kiislamu wa maisha kama undugubia ambao unahusisha wale wote ambao wanashika imani ya Kiislamu. Hakuna sehemu inayosema Mungu ni upendo, lakini miongoni mwa majina 99 ya Allah, kuna jina Al-Wadud, au "Anayependa," ambalo hupatikana katika Sura 11:90 na vilevile Sura 85:14. Linamtaja Mungu kama "aliyejaa fadhili." Wale wote ambao wanaamini wana mapenzi ya Mungu, lakini kwa kiasi gani au juhudi zipi amemfurahisha Mungu inamtegemea mtu binafsi.

Ishq, au mapenzi ya kiungu, ni msisitizo wa Usufi. Wasufi huamini kwamba mapenzi ni makadirio ya kiini cha Mungu kwa ulimwengu. Mungu anatamani kutambua uzuri, na kama mtu aangaliavyo kwenye kioo ili kujiona, Mungu "hujiangalia" kwenye mienendo ya asili. Kwa kuwa kila kitu kinaonyesha Mungu, shule ya usufi huzingatia kuona uzuri ndani ya kinachoonekana kuwa kibaya. Usufi mara nyingi unajulikana kama dini ya upendo. Mungu katika usufi hutajwa kwa majina matatu makuu, ambayo ni mpenzi, mpendwa, na kipenzi, na neno la mwisho kati ya maneno haya likijitokeza sana katika ushairi wa kisufi. Mtazamo wa kawaida wa Usufi ni kwamba kupitia mapenzi, wanadamu wanaweza kurudia usafi na neema yao ya awali. Watakatifu wa Usufi wanasifika kwa kuwa "walevi" kutokana na upendo wao wa Mungu; ndio maana mvinyo unatajwa sana katika mashairi na muziki wa kisufi.

Dini za Mashariki[hariri | hariri chanzo]

Ubudha[hariri | hariri chanzo]

Katika Ubudha, Kāma ni mapenzi ya kimihemko na kingono. Ni kikwazo katika njia ya kutaalamika, kwani yana ubinafsi. Karuṇā ni huruma na rehema, ambayo hupunguza mateso ya wengine. Huenda sambamba na hekima na ni muhimu kwa kutaalamika. Adveṣa na Metta ni mapenzi ya ukarimu. Mapenzi haya hayana masharti na yanahitaji mtu kwa kiasi fulani awe amejikubali. Mapenzi haya ni tofauti kabisa na yale ya kawaida, ambayo kwa kawaida huwa yanahusu upendo na ngono na ambayo ni nadra yawepo bila kujifikiria. Badala yake, katika Ubudha inarejelea uhisani wa ustawi wa wengine usio wa kibinafsi.

Maadili ya Bodhisattva katika Ubudha wa Mahayana yanahusisha kujinyima kamili ili kuchukua mzigo wa mateso ya dunia. Kichocheo kikuu alicho nacho mtu ili kuchukua njia ya Bodhisattva ni wazo la wokovu ndani yake, mapenzi ya kiutu kwa viumbe wote.

Uhindu[hariri | hariri chanzo]

Katika Ubanyani, kāma ni mapenzi matamu ya kingono, yaliyohuishwa na mungu Kamadeva. Kwa shule nyingi za kihindu, huu ndio mwisho wa tatu (artha) katika maisha. Mara nyingi Kamadeva huonyeshwa pichani kashika upinde wa miwa na mshale wa maua; yeye huweza hata kubebwa na kasuku mkubwa. Yeye huwa ameandamana na mke wake rati na sahibu wake Vasanta, mkubwa wa msimu wa kuchipua Sanamu za mawe za Kaama na rati zinaweza kuonekana kwenye mlango wa hekalu ya Chenna Keshava katika Belur, huko Karnataka, India. Määrä ni jina lingine la kama.

Tofauti na kama, prema  – au Prem  – yanarejelea mapenzi yaliyoinuliwa. Karuna ni huruma na rehema, ambazo humchochea mtu kusaidia kupunguza mateso ya wengine. Bhakti ni istilahi ya Kisanskriti, inayomaanisha "mapenzi ya ibada kwa Mungu mkuu." Mtu anayefuata bhakti anaitwa bhakta. Waandishi wa Kihindi, wanateolojia, wanafalsafa wametambua aina tisa za bhakti, ambazo zinaweza kupatikana katika kitabu cha Bhagavata Purana and works cha Tulsidas. Kazi ya kifalsafa Narada Bhakti Sutra iliyoandikwa na mwandishi asiyejulikana (anayefikiriwa kuwa Narada), inatambua aina kumi na moja za mapenzi.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Kristeller, Paul Oskar (1980). Renaissance Thought and the Arts: Collected Essays. Princeton University. ISBN 0-691-02010-8. 
  2. Mascaró, Juan (2003). The Bhagavad Gita. Penguin Classics. ISBN 0-140-44918-3.  (J. Mascaró, translator)
  3. Kay, Paul (Machi 1984). "What is the Sapir-Whorf Hypothesis?". American Anthropologist. New Series 86 (1): 65–79. doi:10.1525/aa.1984.86.1.02a00050.  Check date values in: |date= (help)
  4. Ancient Love Poetry. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-09-30. Iliwekwa mnamo 2021-07-17.
  5. Leibniz, Gottfried. Confessio philosophi. Wikisource edition. Iliwekwa mnamo Mar 25, 2009.
  6. DiscoveryHealth. Paraphilia. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-12-12. Iliwekwa mnamo 2007-12-16.
  7. 7.0 7.1 Lewis, Thomas; Amini, F., & Lannon, R. (2000). A General Theory of Love. Random House. ISBN 0-375-70922-3. 
  8. 8.0 8.1 Winston, Robert (2004). Human. Smithsonian Institution. 
  9. Emanuele, E.; Polliti, P.; Bianchi, M.; Minoretti, P.; Bertona, M.; & Geroldi, D (2005). "Raised plasma nerve growth factor levels associated with early-stage romantic love". Psychoneuroendocrinology. Sept. 05. 
  10. Rubin, Zick (1970). "Measurement of Romantic Love". Journal of Personality and Social Psychology 16: 265–27. doi:10.1037/h0029841. 
  11. Rubin, Zick (1973). Liking and Loving: an invitation to social psychology. New York: Holt, Rinehart & Winston. 
  12. Berscheid, Ellen; Walster, Elaine, H. (1969). Interpersonal Attraction. Addison-Wesley Publishing Co. CCCN 69-17443. 
  13. Peck, Scott (1978). The Road Less Traveled. Simon & Schuster. p. 169. ISBN 0-671-25067-1. 
  14. Thomas Köves-Zulauf, Reden und Schweigen, München, 1972.
  15. 15.0 15.1 Pope Benedict XVI. papal encyclical, Deus Caritas Est..

Vyanzo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Simple English Wiktionary
Simple English Wiktionary
Wikamusi ya Kiswahili ina dictionary definitions (word meanings):