Madawa ya kulevya katika Mombasa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Utumiaji wa madawa ya kulevya umekuwa mojawapo kati ya masuala makubwa nchini Kenya, hasa Mombasa ambayo ni sehemu iliyoathirika zaidi ya nchi.

Wakazi wengi hasa wanaume wameathiriwa na suala hili. La kuhatarisha sana ni kuwa wengi wanaotumia madawa haya wako katika umri wa miaka ishirini.

Akina mama mjini Mombasa wamefanya maandamano wakitaka serikali kukomesha matumizi ya madawa ya kulevya miongoni mwa vijana katika eneo hili. Huko Kilindini mjini Mombasa kuna maeneo arobaini ambayo walevi hutambua kama 'maskani' ambapo wao hukutana ili kutumia madawa haya.

Hivi sasa utumiaji wa heroin umepita ule wa bangi. Asilimia sabini wanaotumia madawa ya kulevya wamekiri kuwa wao hutumia heroin.

Sababu za kuongezeka kwa utumiaji wa madawa ya kulevya[hariri | hariri chanzo]

Ukosefu wa ajira[hariri | hariri chanzo]

Nchini Kenya kiwango cha ukosefu wa ajira kimo juu sana. Ukosefu wa ajira umesababisha vijana wengi kukaa ovyo bila chochote cha kufanya na hivyo kugeukia madawa ya kulevya.

Shinikizo kutoka kwa marafiki[hariri | hariri chanzo]

Hii ni moja ya sababu kuu ya kutumia madawa ya kulevya. Wengi wanaotumia madawa ya kulevya katika ukanda huu wamekubali kwamba walianza kutumia madawa kwa sababu marafiki wao wengi walikuwa wanayatumia. Wengi wa vijana ambao wanapatikana kule baharini wanatumia madawa haya ili wapate ujasiri wa kuzungumza na wateja wao.

Ushirikina[hariri | hariri chanzo]

Wakazi wengi wa eneo hili wanaamini ushirikina. Kulingana na utafiti uliofanywa nchini hivi juzi inaaminika kuwa vijana wengi katika mkoa huu unatumia madawa wanafanya hivi kwa sababu ya kujihami kutokana na uvamizi wa vizuka.

Athari[hariri | hariri chanzo]

Uhalifu[hariri | hariri chanzo]

Katika ukanda huu vijana hawa hawawezi kukaa bila kutumia dawa hizi. Dawa hizi huwa ghali mno, na la kusikitisha ni kuwa vijana hawa hawana ajira. Hii inamaanisha kuwa vile wanavyoweza kupata pesa ni kwa kuwaibia wakazi wenzao. Hii inasababisha usalama wa ukanda huu kutoaminika.

Maradhi[hariri | hariri chanzo]

Hii ni athari kubwa ya madawa ya kulevya. Kuna maradhi mengi ambayo vijana hawa wanapata kutokana na madawa haya. Maradhi haya yanawapata vijana hawa kwa kasi mno kwa sababu ya kutokula vyema. Hawawali lakini wanaendelea kutumia madawa haya. Baadhi yao wamekuwa wendawazimu.

Pia wanaambukizana maradhi kwa kubadilishana sindano. Hii imesababisha kusambaa kwa UKIMWI katika eneo hili.

Kukosekana kwa maendeleo[hariri | hariri chanzo]

Madawa ya kulevya pia yamesababisha kutoendelea katika maeneo mengi ya Mombasa ambayo ndiyo bandari kubwa katika Afrika Mashariki. Hii ni kutokana na uhaba unaosababishwa na baadhi ya wanaotumia madawa ya kulevya ambao huwashambulia wakazi wa maeneo haya. Jambo hili hutisha wafanyabiashara na kuwafanya wahamie mbali. Vijana hawa pia huwa wavivu na hawataki kufanya jambo lolote ambalo laweza kusaidia kukuza maeneo hayo, wao wanataka kuketi na kuvuta bangi.

Kifo[hariri | hariri chanzo]

Mwishowe athari hizi zote zaelekeza kaburini. Kiwango cha vifo katika ukanda huu kinaongezeka kwa kasi mno. Vijana wengi wanaaga dunia katika miaka yao ya thelathini. Vifo hivi vinasababishwa hasa na maradhi yanayoletwa na madawa ya kulevya. Hili ni jambo linaloitia nchi ya Kenya wasiwasi.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]