Lamu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru


Lamu
Lamu is located in Kenya
Lamu
Lamu

Mahali pa mji wa Lamu katika Kenya

Majiranukta: 2°16′0″S 40°55′0″E / 2.26667°S 40.91667°E / -2.26667; 40.91667
Nchi Kenya
Kaunti Lamu
Idadi ya wakazi
 - Wakazi kwa ujumla 25,385

Lamu ni mji mkubwa wa kisiwa cha Lamu kwenye pwani ya Kenya wenye wakazi 25,385 (2019[1]). Mji huo ni pia makao makuu ya Kaunti ya Lamu.

Mji upo upande wa kaskazini-mashariki wa kisiwa kando ya mfereji unaotenganisha visiwa vya Lamu na Manda. Mfereji huo ni bandari asilia inayohifadhiwa dhidi ya dhoruba na mawimbi makali ya bahari.

Mji wa Lamu[hariri | hariri chanzo]

Lamu lina umbo la kanda ndefu mwambaoni. Mji wa kale umegawiwa katika mitaa arobaini lakini kuna hasa sehemu mbili: Mkomani upande wa kaskazini penye nyumba kubwa ya mawe na Langoni upande wa kusini ambako wakazi wapya walijenga nyumba za udongo.

Jengo kubwa la mji ni boma lililokaa zamani moja kwa moja ufukoni.

Mwambao wa leo umepatikana tu tangu karne ya 19. Mwambao wa kale unaonekana kwa barabara ya Harambee (au: Usita wa Mui). Wakati wa kujenga Boma ufuko wa kale ulikuwa na maji yenye kina kifupi, hivyo ikaamuliwa kujaza sehemu hizo na kupanua eneo la mji kuingia ufukoni. Watu wenye uwezo walijenga nyumba zao kubwa na mstari wa ufuko ukaimarishwa kwa ukuta.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Wataalamu wengi huamini ya kwamba mji wa Lamu uliundwa katika karne ya 14. Historia ya Kilwa ambayo ni taarifa iliyoandikwa kwa lugha ya Kiarabu mnamo karne ya 16 inadai ya kwamba chanzo cha mji kilitokea wakati wa kufika kwa familia moja kutoka Shiraz (Uajemi) katika karne ya tatu baada ya Hijra iliyonunua kisiwa kutoka kwa watu wa bara.

Biashara ya kimataifa[hariri | hariri chanzo]

Mji ulistawi kwa biashara kati ya pwani ya Afrika Mashariki na Bara Arabu pamoja na Uhindi. Kilwa ilikuwa kituo kwa ajili ya majahazi yaliyopita njiani. Miji yote ya Uswahilini ilinunua bidhaa kutoka kwa Waarabu na Wahindi na kuuza pembe za ndovu, maganda ya kobe na mazao pamoja na watumwa. Biashara kubwa ya Lamu ilikuwa miti aina ya mkoko yenye ubao usiooza kwa urahisi, na hasa hauliwi na mchwa, hivyo unafaa vizuri kwa ujenzi wa nyumba. Mikoko ilipatikana tele kwenye funguvisiwa la Lamu lakini siku hizi imepungua mno, hivyo serikali imekataa kuziuza nje.

Kipindi cha Wareno[hariri | hariri chanzo]

Wareno walifika Lamu mwaka 1506. Watawala wa Lamu walipaswa kupatana nao ingawa kuna taarifa za majaribio kadhaa za kuasi. Lamu haikuwa kati ya miji kama Malindi iliyoshikamana na Wareno kwa hiari. Mji ulitumia nafasi mbalimbali kuasi dhidi ya Wareno ukaabishiwa vikali kila safari hadi mwishowe Waarabu wa Omani waliwaondoa Wareno mnamo 1696 kabla ya kuteka kituo chao cha mwisho huko Mombasa mwaka 1698.

Karne za dhahabu[hariri | hariri chanzo]

Kuja kwa Wareno kulikuwa kumevuruga biashara ya Bahari Hindi pamoja na heri ya miji mingi ya Waswahili. Kuondoka kwao kulimaanisha ya kwamba nafasi hizo zikapatikana tena. Omani ilikuwa na utawala wa pwani ya Afrika ya Mashariki lakini kwa mbali tu na utawala wake haukuwa mzogo sana. Lamu ilianza kustawi kushinda miaka ya nyuma. Majengo mazuri yanayopamba mji wa kale yalijengwa wakati wa karne ya 18 na hasa ya 19.

Mwisho wa karne ya 18 Lamu ikajikuta katika mashindano makali na Pate. Sultani Fumo Madi ibn Abi Bakr wa Pate alifaulu kuteka Lamu akaanza kujenga boma kubwa lililopo hadi leo. Mwanzo wa karne ya 19 Lamu iliweza kujiondoa katika utawala wa majirani kwa ushindi wake juu ya jeshi la Pate katika mapigano ya Shela mwaka 1813.

Hadi mwisho wa karne Lamu ilikuwa mji wa kwanza katika funguvisiwa. Umuhimu wa biashara ya watumwa waliouzwa Zanzibar na Uarabuni ikaongezeka na kazi ya watumwa iliwezesha mabwana kulima mashamba makubwa wakiuza mazao nje.

Kukwama na kurudi nyuma[hariri | hariri chanzo]

Sehemu ya pili ya karne ya 19 iliona mabadiliko tena. Usultani wa Zanzibar ulikuwa umerithi ubwana wa pwani kutoka Omani lakini uliweza kukazia utawala wake kwa sababu haukuwa mbali mno.

Katika miaka tangu 1880 nchi za Ulaya zilianza kujenga ukoloni wao. Wajerumani walianzisha koloni lao katika Witu wakajenga ofisi ya Posta ya Kijerumani kwenye mji wa Lamu kwa sababu palikuwa na bandari iliyo karibu zaidi. Lakini kuja kwa Wazungu na meli zao kubwa kuliondoa pia sehemu ya biashara kutoka Lamu. Meli kubwa zilipendelea bandari kubwa zaidi kama Mombasa au Malindi.

Mwisho wa utumwa[hariri | hariri chanzo]

Pigo kubwa kwa Lamu ilikuwa kukatazwa kwa utumwa. Waingereza walikuwa wakilazimisha Zanzibar kukataza kwanza biashara ya watumwa na baadaye utumwa wenyewe. Mabwana wote wenye mashamba makubwa kwenye pwani ya Uswahilini walishindwa kuendelea na mashamba yao na kupata faida kwa sababu waliokuwa watumwa hawakutaka tena kuwahudumia kama watu huru.

Eneo lililosahauliwa katika Kenya huru[hariri | hariri chanzo]

Lamu ikakwama na kurudi nyuma katika Kenya iliyoona mabadiliko ya haraka wakati wa ukoloni na baadaye wakati wa uhuru. Wilaya ya Lamu ilipaswa kubeba mzigo wa kusahauliwa kama maeneo mengine ya nchi nje ya nyanda za juu. Barabara ya lami haikupatikana wilaya ya Lamu hadi mwaka 2006.

Miaka ya mwisho utalii umeleta tena biashara mpya lakini mara nyingi ni watu wa nje ya Lamu wanaofaidika.

Utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Mifano bora ya usanifu wa Uswahilini inapatikana Lamu. Hivyo imepokewa na UNESCO katika orodha ya urithi wa dunia kwa sababu ni "mji wa Uswahilini uliohifadhiwa kushinda miji yote mingine".

Boma la Lamu lililojengwa na watu wa Pate leo hii ni makumbusho yanayotembelewa na wageni wengi.

Makumbusho madogo yanakumbusha kituo cha kwanza cha posta ya Kijerumani katika Afrika ya Mashariki; Lamu ilikuwa kituo cha posta kwa koloni la Kijerumani huko Witu.

Lamu kote magari hayaruhusiwi isipokuwa gari mojamoja la mkuu wa wilaya, polisi na hospitali. Vinginevyo watu hutembea na kutumia sana usafiri wa punda.

Sherehe ya Maulidi[hariri | hariri chanzo]

Katika karne ya 20 Lamu imekuwa mahali pa sherehe ya Maulidi inayovuta wageni kutoka pande zote za Uswahilini na nchi za jirani. Sheikh Habib Saleh al Habshi alifika Lamu kutoka Hadramaut (Yemeni) katika miaka ya 1880 akafundisha kwenye madrasa. Akapata wanafunzi wengi akajenga Ribat ar-Riyada mwaka 1900. Chini ya uongozi wake sherehe ya Maulidi ikasheherekewa na wanafunzi wake wengi walioimba aya za sifa kwa Allah na mtume Muhammad.

Sherehe imeendelea kuvuta washiriki na watazamaji wengi hata baada ya kifo chake mwaka 1935 NA hadi leo.

Jahazi ya Maulidi.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

  1. https://www.citypopulation.de/en/kenya/cities/