Kilimia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kilimia angani (upande wa kulia, juu ya mti)
Kilimia kikiagaliwa kwa darubini

Kilimia (pia: thuria kutokana na Kar. "ثریا"; ing. - gir. Pleiades) ni fungunyota katika kundinyota la Ng’ombe (zamani Tauri, lat. Taurus). Jina la kisayansi ni "M45" (katika orodha ya Messier).

Tabia za kiastronomia

Kwa macho nyota sita hadi saba zinaonekana vizuri sana, na hadi 14 kwa macho mazuri. Lakini kwa darubini kilimia ni fungunyota lenye nyota 1,200. Umbali wake na jua letu ni miakanuru 410. Umri wake hukadiriwa kuwa miaka milioni 125.

Ishara ya mvua

Fungunyota hili linaonekana vizuri kabisa kwa macho. Linaanza kuonekana angani masaa ya mwanzo wa usiku katika miezi kuanzia Oktoba. Hivyo kuonekana kwake imechukuliwa na wazee katika Afrika Mashariki kama kalenda ya kuandaa mashamba na kilimo kwa sababu mvua umekaribia. Hii ni sababu ya kupewa jina la "kilimia" kutokana na "kulima, kilimo".

Waswahili walitumia pia jina la kiarabu la "thuria" (ثریا).

Nafasi ya nyota kama ishara za kalenda zinapungua kwa sababu nyakati za kuonekana au kuzama hubadilika polepole baada ya karne kadhaa kutokana na mwendo wa mfumo wa jua letu angani.

Kilimia katika mapokeo ya tamaduni mbalimbali

Kwa lugha nyingi kilimia huitwa kwa jina kama "nyota saba" kwa sababu ni takriban nyota 6 hadi saba zinazoonekana vizuri kwa macho. Mtu mwenye macho mazuri sana ataona hata 9 hadi 14.

Wazee wa Afrika ya Mashariki walikitazama na kuielewa kama ishara ya hali ya hewa hasa mvua wakatunga methali "Kilimia kikizama kwa jua huzuka kwa mvua, kikizama kwa mvua huzuka kwa jua"[1].

Kilimia ni pamoja na Jabari kati ya nyota zinazotajwa mara kadhaa katika Biblia (Ayubu 9:9 na 38:31; Amosi 5:8).

Kuonekana kwao kulikuwa alama ya kalenda katika tamaduni nyingi kama kati ya Wakelti, Wagermanik, Waazteki na wengine.

Wagiriki wa Kale walikiita "Pleiadi" na kusimulia hadithi ya mabinti saba wazuri waliopelekwa angani na mungu Zeus ili kuwalinda dhidi ya tamaa za mwindaji Orion (Jabari). Miaka 2500 iliyopita ilionekana Ugiriki jioni wakati wa Mei hivyo ilikuwa ishara ya kuanza mavuno. Kuzama wakati ule mwezi wa Novemba kulikuwa ishara ya kulima mashamba kabla ya baridi.

Marejeo

  1. Kamusi ya methali za Kiswahili, Ahmed E. Ndalu, Kitula G. King'eiuk. 116, methali no. 778 & 779, East African Publishers, 1989 (kupitia google books, iliangaliwa Fenruari 2017
Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kilimia kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.