Kabinda (mkoa)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru


Kabinda
Mahali paKabinda
Mahali paKabinda
Mahali pa Mkoa wa Kabinda katika Angola
Nchi Angola
Mji mkuu Kabinda
Eneo
 - Jumla 7,270 km²
Ramani ya Angola pamoja na Kabinda.
Ramani ya Kabinda

Mkoa wa Kabinda (pia: Cabinda) ni kati ya mikoa kumi na nane ya Angola. Uko kwenye pwani ya Atlantiki.

Umepakana na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Jamhuri ya Kongo na Atlantiki. Kumbe eneo lake haligusani na maeneo mengine ya Angola kwa kuwa limetengwa nayo kwa kanda la ardhi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo lenye upana wa kilomita 30.

Sehemu ya wenyeji wamepinga kutawaliwa na Angola wakidai uhuru.

Una wakazi 152,100 kwenye eneo la km² 7,270 na wakazi lakhi 3. Makao makuu ya mkoa yapo Kabinda (pia: Cabinda. Miji mingine ni Belize, Cacongo na Buco Zau.

Uchumi[hariri | hariri chanzo]

Kabinda inazalisha kahawa, kakao, ubao na mawese. Msingi wa uchumi ni hasa mafuta ya petroli. Mapato ya mafuta huingiza 80% za pato lote la serikali ya Angola.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Ufalme mdogo chini ya Manikongo na Wareno[hariri | hariri chanzo]

Kihistoria Kabinda ilikuwa mahali pa falme tatu ndogo za Ngoyo, Loango and Cacongo. Falme hizi ziliwahi kuwa chini ya Manikongo mfalme wa milki ya Kongo. Baada ya mwisho wa utawala huo falme ziliendelea pekee yao zikifanya biashara ya watumwa na Wareno. Ureno ulikuwa na vituo vya biashara kwenye pwani bila kuonyesha nia ya kutawala kweli nje ya kujipatia watumwa kupitia watawala wa falme hizi.

Mashindano juu ya mdomo wa mto Kongo[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1884/5 ulikuwa kipindi cha kugawiwa kwa Afrika na Mfalme Leopold II wa Ubelgiji alijaribu kutwaa maeneo yote ya Kongo. Ufaransa ilitangulia kufanya mikataba ya ulinzi na maeneo kaskazini ya mto Kongo.

Ureno iliogopa ya kwamba Wafaransa pamoja na Leopold II wataisukuma nje ya nafasi yake kwenye mdomo wa Kongo ikatangaza madai yake juu ya nchi mdomoni wa mto Kongo na kuitangaza kimataifa kuwa koloni yake. iliona haja ya kuimarisha vituo vyake vya biashara hivyo ikaona afadhali kuwa na koloni huko ingekuwa njia afadhali. Inaonekana hata watawala wadogo wa eneo walipendelea kushirikiana na Wareno waliozoea tayari kuliko Wabelgji au Wafaransa. Hivyo tar. 1 Februari 1885 watawala wa Kabinda walifanya mapatano ya kukubali ulizi wa Ureno kwa mkataba wa Simulambuco. Waliahidia ya kwamba haki zao zitaheshimiwa. Wareno walitegemea kuwa na eneo fululizo kutoka Kabinda hadi mdomo wa Kongo halafu ng'ambo yake eneo lao la Angola.

Ureno iliingia katika mkutano wa Berlin wa 1885 ikaonyesha mkataba huu lakini mkutano uliamua kumpa Leopold kanda la eneo la kufika baharini kwa himaya yake katika Kongo. Hivyo kanda la ardhi kaskazini ya mdomo wa mto Kongo likakatwa na maeneo yaliyodaiwa na Ureno na kuwekwa chini ya Dola la Kongo.

Nchi lindwa la Kongo ya Kireno[hariri | hariri chanzo]

Kabinda iliendelea kama nchi lindwa ya pekee chini ya Ureno. Mara nyingi iliitwa "Kongo ya Kireno" kama vile "Kongo ya Kibelgiji" au "Kongo ya Kifaransa". Mwaka ule Wareno waliamua kupunguza gharama za utawala wa koloni zao wakaweka Kabinda chini ya Gavana Mkuu wa Angola.

Katiba ya Ureno wa 1933 iliorodhesha Kabinda kama eneo la ng'ambo kando la Angola na maeneo mengine.

Mwaka 1956 Wareno waliweka Kabinda chini ya Gavana Mkuu wa Angola kwa kusudi la punguza gharama za utawala.

Mwaka 1964 mkutano wa Umoja wa Muungano wa Afrika ulidai uhuru kwa maeneo ya Kireno katika Afrika kwa kuorodhesha Kabinda kama nchi ya 39 ya Afrika.

Sehemu ya Angola[hariri | hariri chanzo]

Wakati wa uhuru wa Angola serikali mpya haikuwa tayari kutafakari uhuru wa pekee kwa Angola kutokana na kawaida ya utawala wa kikoloni iliyoshughulika mambo ya Kabinda kama sehemu ya Angola hata kama katiba ya Ureno ilitaja Kabinda kama kitu cha pekee.

Wakati wa mapinduzi ya Ureno ya 1974/75 iliyoleta uhuru wa koloni zake kikundi cha kupigania uhuru wa Kabinda FLEC kiliandaa kutangaza serikali mpya. Lakini MPLA ya Angola haikukubali ilituma wanajeshi waliotwaa mamlaka mwisho wa 1975.

FLEC iliendesha vita ya msituni kwa miaka kadhaa lakini mwishowe ilishindwa. Iliunda serikali ya nje na kutangaza "Jamhuri ya Kabinda" (Republica de Cabinda).

Angola inategemea mapato ya mafuta ya Kabinda. Kutopatikana kwa mapato haya kwa Kabinda yenyewe ni sababu muhimu ya masikitiko ya wenyeji shidi ya serikali kuu.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]


Makala hii kuhusu maeneo ya Angola bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Kabinda (mkoa) kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.