Helgoland

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mahali pa kisiwa cha Helgoland katika Bahari ya Kaskazini
Visiwa vya Helgoland (mbele) na Düne kwa macho ya ndege

Helgoland ni fungukisiwa ndogo cha Kijerumani katika Bahari ya Kaskazini takriban 70 km mbele ya Ujerumani bara. Ina visiwa viwili: Helgoland yenyewe ni kisiwa kinachokaliwa na watu halafu kisiwa kisicho na watu cha "Düne" (= tuta la mchanga). Kisiwa kikuu kina urefu wa 1700 m na wakazi 1,650.

Kiutamaduni Helgoland ni sehemu ya Frisia; wenyeji wanasema Kifrisia na Kijerumani. Iliwahi kuwa sehemu za nchi za Denmark na Ujerumani na kwa muda wa karne ya 19 BK pia chini ya Uingereza.

Zamani wakazi wa Helgoland walikuwa wavuwi na mabaharia. Tangu karne ya 19 utalii ilianza kuwa muhimu siku hizi wengi wanajipatia maisha kwa njia ya utalii.

Helgoland na Afrika[hariri | hariri chanzo]

Helgoland ilivamiwa na Uingereza wakati wa vita kati ya Napoleon na Uingereza mw. 1807. Kisiwa cha Helgoland kikabaki kituo cha kijeshi cha Uingereza hadi 1890. Tangu kutokea kwa utaifa katika Ujerumani utawala wa kigeni ulisikitisha Wajerumani wengi.

Serikali ya Dola la Ujerumani ilichukua nafasi ya majadiliano kuhusu mapatano ya mipaka ya kikoloni kati ya Uingereza na Ujerumani kuingiza swali la Helgoland katika mapatano haya.

Mapatano kati ya Ujerumani na Uingereza ya tarehe 01. 07. 1890 yalisuluhisha maswali mbalimbali kuhusu mipaka ya maeneo yao katika Afrika ya Mashariki, ya Kusini-Magharibi na ya Magharibi. Maeneo mawili yaliyoangaliwa hasa na watu yalikuwa Zanzibar na Helgoland. Hivyo mapatano yamejulikana zaidi kwa jina la Mkataba wa Helgoland-Zanzibar ingawa jina rasmi lilikuwa "Mkataba kuhusu koloni na Helgoland" ikiwa visiwa viwili vilikuwa tu vipengele katika orodha ndefu ya maswali yaliyopata usulihisho.

Wafuasi wa hoja la kupanusha athira ya Ujerumani duniani walisikitika sana ya kwamba serikali ya Chansella Caprivi ilifuta madai ya Ujerumani juu ya Zanzibar na Uganda kwa ajili ya "mwamba mdogo" wa Helgoland. Lakini miaka 73 baada ya mkataba Uingereza haukuwa tena na neno kuhusu Zanzibar lakini Helgoland imeendelea kuwa sehemu ya Ujerumani.