Godfrey Mwakikagile

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Godfrey Mwakikagile

Godfrey Mwakikagile (alizaliwa Kigoma, 4 Oktoba 1949) ni mwandishi Mtanzania aishiye nchini Marekani. Anajulikana hasa kwa kuandika wasifu wa rais Julius Kambarage Nyerere.

Ameandika zaidi ya vitabu sabini [1]. Vitabu vyake vingi vinatumiwa vyuoni katika nchi mbalimbali duniani. Ameandika vitabu vya siasa, uchumi, historia na masomo mengine kuhusu bara la Afrika na nchi mbalimbali katika bara hilo. Pia ameandika vitabu kuhusu watu weusi wenye asili ya Kiafrika nchini Marekani, Uingereza na visiwa vya Karibi pamoja na nchi ya Belize, bara la Amerika, ambayo pia ina asili ya watumwa kutoka Afrika.

Pia aliwahi kuwa mwandishi wa gazeti la Daily News ambapo wakati huo lifahamika kama "The Standard".

Mwakikagile alikuja kupata umaarufu baada ya kuandika kitabu kinachoitwa Nyerere and Africa: End of an Era [2], ambacho ni biografia ya Rais wa kwanza wa Tanzania Julius Nyerere na ambacho kinaongelea Afrika, maisha ya ukoloni, vita vya ukombozi katika nchi za kusini mwa Afrika ambapo Nyerere alisaidia kwa kiasi kikubwa.

Maisha yake ya mwanzo na kazi[hariri | hariri chanzo]

Kabla ya kwenda nchini Marekani, Godfrey Mwakikagile alikuwa mwandishi wa habari, Daily News moja kati ya magazeti makubwa na makongwe nchini Tanzania, pia ni kati ya magazeti makubwa Afrika Mashariki, Dar es Salaam, Tanzania. Pia aliwahi kuwa mwandishi wa habari katika Wizara ya Habari na Utangazaji, Dar es Salaam.

Mhariri wa Daily News wakati ule, Benjamin Mkapa, ambaye baadaye alichaguliwa kuwa rais wa Tanzania, alimsaidia kwenda Marekani kusoma. Alipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Wayne State, Detroit, Michigan, nchini Marekani, Godfrey Mwakikagile alichaguliwa kuwa rais wa Chama cha Wanafunzi wa Kiafrika katika chuo hicho.

Amewahi kufundisha sehemu mbalimbali nchini Marekani.

Pia amealikwa na vyuo vikuu mbalimbali nchini Marekani kwenda kuzungumza na wanafunzi na walimu wa vyuo hivyo kuhusu masuala mbalimbali kwa sababu ya vitabu alivyoandika. Vyombo mbalimbali vya habari, pamoja na BBC, Voice of America (VOA), PBS (Public Broadcasting Service) ya Marekani na vingine navyo vimemwalika kuzungumza naye kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu bara la Afrika pamoja na viongozi wake na sera zao.

Professor Guy Martin, katika kitabu chake, African Political Thought, ameandika kwamba Godfrey Mwakikagile ni miongoni mwa wasomi wa juu kutoka bara la Afrika ambao ni "populist scholars" na "thinkers" pamoja na viongozi kama Kwame Nkrumah, Mwalimu Julius Nyerere, Amilcar Cabral, Cheikh Anta Diop, Steve Biko, na Claude Ake, katika historia ya bara hilo tangu karne nyingi zilizopita.

Godfrey Mwakikagile anaendelea kuandika vitabu. Kitabu chake ambacho kilichapishwa tarehe 4 Oktoba 2019, siku yake ya kuzaliwa, kinaitwa Conquest of the Mind: Imperial subjugation of Africa.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Godfrey Mwakikagile Books | List of books by author Godfrey Mwakikagile. Iliwekwa mnamo 22 Nov 2022.
  2. Mwakikagile, Godfrey (22 Nov 2007). Nyerere and Africa: End of an Era. New Africa Press. Iliwekwa mnamo 22 Nov 2022.
Makala hii kuhusu mwandishi fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Godfrey Mwakikagile kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.