Faustina Kowalska

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Helena Kowalska ujanani.
Sista Maria Faustina wa Sakramenti Kuu mwaka 1938, kidogo kabla ya kufa.

Maria Faustina Kowalska, (kabla hajaingia utawani aliitwa Helena Kowalska; anafahamika zaidi kama Mtakatifu Faustina; Głogowiec (soma Gwogoviec) karibu ya Łódź (soma Wodz) nchini Poland, 25 Agosti 1905 - Kraków, Poland, 5 Oktoba 1938[1]) alikuwa bikira anayejulikana hasa kama mtume wa Huruma ya Mungu, katibu wa Yesu Mwenye Huruma na mwandishi wa Hafidhi.

Anaheshimiwa kama mtakatifu wa Kanisa Katoliki, kutokana na sifa zake kama mtawa wa Shirika la Bibi Yetu wa Huruma, mcha Mungu, aliyejaliwa njozi na madonda ya Yesu.

Sikukuu yake huadhimishwa tarehe ya kifo chake[2].

Maisha

Helena Kowalska alizaliwa tarehe 25 Agosti 1905, kama mtoto wa tatu baina ya watoto kumi wa Stanisław na Marianna Kowalski, wakulima kutoka kijiji kinachoitwa Głogowiec; wote wawili walikuwa maskini lakini waadilifu.

Tangu alipokuwa na umri wa miaka saba alisikia wito wa maisha ya utawa. Mwaka 1916 alianza shule ya msingi kijijini Świnice Warckie (soma Shvinitse Vartskie).

Baada ya miaka mitatu ya mafunzo, licha ya matokeo yake mazuri alilazimika kumaliza elimu yake na kuanza kufanya kazi kwa watu tajiri kama mtumishi wa ndani nyumbani na mlezi wa watoto [3].

Alipokuwa na umri wa miaka 17 aliwaambia wazazi wake kuwa alitaka kujiunga na utawa. Wazazi wake hawakutaka kumpoteza binti yao mpendwa, kwa hivyo walimkatalia katakata mara mbili ombi lake.

Mnamo mwaka 1922 alikwenda Łódź kufanya kazi ya mtumishi wa ndani [4].

Mwaka 1924, wakati wa kucheza ngoma katika hifadhi ya "Venice" mjini Łódź alikuwa na maono ya "Yesu aliyeteswa sana, kavuliwa nguo, na mwili wake wote umejaa vidonda na anaguna, akisema maneno haya kwangu: Kwa muda gani nitakuvumilia mpaka utakubali?" (Hafidhi 9) [5].

Bila kuwajulisha wazazi wake alipanda gari la moshi akaenda Warszawa (soma Varshava). Baada ya kufika mjini huko alielekea kanisa la kwanza lililoko karibuni yaani Kanisa la Mtakatifu Yakobo katika barabara Grójecka.

Akakaa kijijini Ostrówek (soma Ostuvek), ambapo hadi mwaka 1925 alifanya kazi kwa akina Lipszyc. Hakuchoka kutafuta shirika la kitawa ambalo limpokee. Mara nyingi alikataliwa lakini hakukata tamaa kutafuta.

Hatimaye Sista Michael Moraczewska, mkuu wa Shirika la Bibi Yetu wa Huruma mjini Warszawa, alionyesha nia ya kumpokea shirikani mwao, ikiwa Helena ataweza kuchangia kiasi kidogo cha fedha (kama mahari) cha kununua mavazi ya kitawa[6].

Tarehe 1 Agosti 1925 alijiunga Shirika la Bibi Yetu wa Huruma mjini Warszawa barabara ya Żytnia na kuanza upostulanti.

Mazoezi ya kiroho na mafungo mengi vilimchosha Helena. Kwa sababu hiyo alishinda wiki chache mjini Skolimów (soma Skolimuv) karibu na Warszawa, akiwa na nia ya kusaidia afya yake, kutia mwili wake nguvu.

Tarehe 23 Januari 1926 alikwenda Kraków.

Tarehe 30 Aprili 1926 Helena alianza unovisi na wakati huo alipewa jina la Maria Faustina.

Tarehe 30 Aprili 1928, huko Kraków, aliweka nadhiri za kwanza: ya usafi wa moyo, umaskini na utiifu.

Akiwa sista mdogo wa nadhiri za kwanza (kipindi kinachodumu miaka mitano ambapo kila mwaka alirudia nadhiri) sista Faustina alifanya hasa kazi ya upishi katika nyumba nyingi za shirika. Alikaa katika nyumba ambayo ilikuwa pembeni mwa barabara iliyoitwa Żytnia, mjini Warszawa [7] na baadaye aliishi Vilnius, mji mkuu wa Lithuania (ambao wakati huo ulikuwa upande wa nchi ya Poland), tena mjini Warszawa, katika monasteri karibu na barabara ya Hetman na mjini Płock ambapo alikaa zaidi ya miaka miwili. Katika mji huo wa mwisho alifanya kazi ya mwuzaji katika duka la mikate.

Tarehe 1 Desemba 1931 Faustina alianza muda wake wa majaribio ya tatu katika maisha ya utawa mjini Warszawa. Wakati huo, baba Edmund Elter wa Shirika la Wajesuiti, profesa wa maadili, [[mafunzo ya kuhubiri] (hotuba), na balagha katika Chuo Kikuu cha Gregoriana mjini Roma, alimhakikishia kwamba yuko katika njia ya hakika na nzuri, na uhusiano wake na Yesu si wa mzaha, wala si wa mauzauza au mazingaombwe.

Mnamo tarehe 1 Mei 1933, Faustina aliweka nadhiri za milele mjini Kraków (soma Krakov).

Baada ya nadhiri alitumwa mji wa Wilno (soma Vilno). Alikuwa huko hadi mwaka 1936, akishughulika na kazi ya kutunza bustani. Hapo ndipo alikutana na Baba Michał Sopoćko (soma Mihaw Sopochko), ambaye atakuwa muungamishi wake na Baba wa kiroho (kwa sasa ni Mwenye Heri wa Kanisa Katoliki), Yesu alimwambia "Huyu ndiye mtumishi wangu mwaminifu, yeye atakusaidia kutimiza mapenzi yangu hapa duniani” (Hafidhi 263). [8]

Baada ya ugunduzi wa ugonjwa wa kifua kikuu (TB) mnamo 1936[9], sista Faustina alisafiri kwenda mji wa Kraków, njiani alisimama katika kijiji cha Walendów na Derdy (soma Valenduf na Derdi) kwa muda wa majuma machache.

Alipowasili mjini Kraków alishinda zaidi ya miezi minane katika hospitali ya Prądnik (soma Pradnik). Alitibiwa pia katika nyumba ya shirika mjini Rabka Rabka (soma Rabka).

Alifariki mnamo tarehe 5 Oktoba 1938 [10] katika nyumba ya shirika katika mtaa Kraków-Łagiewniki (soma Krakuv - Wagievniki) [11] [12].

Heshima baada ya kufa

Mazishi ya Sista Faustina yalifanyika tarehe 7 Oktoba 1938 [13]. Alizikwa katika shamba la Mungu la Shirika huko Łagiewniki.

Tarehe 25 Novemba 1966 mabakaa yake yamezikwa tena mahali pengine yaani kakika kanisa dogo la shirika (na tangu mwaka 1968 kanisa hilo liliwekwa katika orodha ya mahali pakatifu katika jimbo kuu la Kraków). Sasa hivi masalia ya mwili wake yamo ndani ya jeneza la jiwe, katika altare, chini ya picha "Yesu, ninakutumainia" ambayo inajulikana kwa fadhili na ilichorwa na Adolf Hyła (soma Adolf Hywa).

Tarehe 18 Aprili 1993, ambapo Sista Faustina alitangazwa na Papa Yohane Paulo II kuwa mwenye heri, masalia yake yaliwekwa hadharani.

Kanisa Katoliki linamheshimu kama tangu alipotangazwa na Papa huyohuyo kuwa mtakatifu tarehe 30 Aprili 2000.

Ufunuo na uzoefu wa uhusiano maalumu baina yake na Mungu

Kutokana na agizo la Baba Michał Sopoćko, halafu pia la baba Yusufu Andrasz SJ (muungamishi wa Kraków), Sista Faustina alikuwa anaorodhesha maono yake yote yaliyo mengi mengi na mafunuo: yote yalichapishwa baadaye katika Hafidhi (Diary).

Matokeo haya yote hayakuhusu maisha yake ya kiroho tu (kwa mfano uhusiano baina yake na Yesu, malaika na watakatifu), lakini zaidi ya hiyo misheni yake ya kinabii, ambayo Kristo alimjalia Faustina kwa ajili ya kumtumia duniani.

Ujumbe wake wa huruma unafanana na ukweli wa Biblia juu ya upendo wa huruma wa Mungu ambayo huletwa naye kwa kila binadamu na pia ulikuwa wito kwa kutangaza ukweli huo kwa nguvu mpya na ushahidi wa maisha, matendo, maneno na sala.

Tukio hilo lilisaidiwa na njia mpya za ibada alizopewa na Yesu, picha "Yesu, ninakutumainia", uanzishaji wa Sikukuu ya Huruma ya Mungu, sala ya Rozari ya Huruma ya Mungu, sala kwa ajili ya kifo chake msalabani (Saa ya Huruma) na tendo la kueneza ibada ya Huruma ya Mungu.

Yesu alitoa ahadi kubwa kwa wale watakaotekeleza maombi haya kwa imani kubwa kwa Mungu na kufanya matakwa yake na kuwapenda jirani zao kama nafsi zao.

Kutokana na maandiko yake Huruma ni kubwa kuliko sifa nyingine za Mungu ambazo binadamu anazishuhudia. Hiyo haina mipaka wala kikomo na inapatikana kwa binadamu wote, hasa kwa watu wakosefu. Kristo alipendekeza kuwa na imani kamili kwa huruma yake Mungu na aliomba watu wawatimizie wenzao vitendo vya huruma kutokana na mapenzi yake.

Kwa mujibu wa "Hafidhi", tarehe 22 Februari 1931, alipokuwa mjini Płock Sista Faustina alikuwa na maono ya Yesu akiwa amevaa kanzu nyeupe. Aliinua mkono wake wa kulia kwa ishara ya kutoa baraka, mkono wake wa kushoto uligusa mavazi kifuani katika mahali ambapo makengee mawili yalimulika. Mojawapo lilikuwa na rangi nyekundu huku lingine nyeupe (lilizingia). Hapo ndipo aliposikia: "Chora picha kulingana na muundo unaouona yenye maandiko ‘Yesu, ninakutumainia’. Napenda picha hii itukuzwe, kwanza kwenye kikanisa chenu, na badadaye duniani kote. Ninaahidi kwamba roho itakayotukuza picha hii haitaangamia. Mimi pia ninaahidi ushindi juu ya maadui na hasa katika saa ya kufa. Mimi mwenyewe nitaikinga kama utukufu wangu mwenyewe. "(Hafidhi 47-48)[14]. Njozi hii ilianzisha kazi yake ya kinabii.

Maono yake mengine yalihusu uanzishaji wa Sikukuu ya Huruma ya Mungu, ambayo watu waiadhimishe Jumapili ya kwanza baada ya Pasaka. "Natamani iwepo Sikukuu ya Huruma. Ninapenda picha ile utakayoichora na brashi; kuwa waweka heri juu yake Jumapili ya kwanza baada ya Pasaka, na Jumapili hii iwe Sikukuu ya Huruma. Nataka mapadri watangaze hii Huruma Yangu kubwa kwa roho za wenye dhambi. "(Hafidhi 49-50)[15]. Mwezi Novemba 1932, wakati wa uungamaji wa mafungo ya kiroho ya padre Edmund Elter SJ, Faustina alipata ushahidi wake wa kwanza uliothibitisha kwamba maono yake yalikuwa na asili ya ufunuo.

Picha ya Yesu mwenye Huruma imechorwa na Eugeniusz Kazimirowski mjini Vilnius. Mchoraji huyo alimaliza kazi hiyo mwezi Juni 1934. Kwa mujibu wa mtakatifu, taswira hiyo haikujaa na uzuri ambao hujaza kila kiumbe kinachojitokeza kwenye maono. "Si kwa uzuri wa rangi, wala wa brashi kulalapo ukuu wa picha hii, lakini katika neema yangu. "(Hafidhi 313) - Yesu alimjibu. [16]

Tarehe 9 Juni 1935 Faustina alisikia maneno haya: "Na kwa maombi yako, wewe na wenzako mtapata rehema kwa ajili yenu wenyewe na kwa ajili ya dunia"(Hafidhi 435)[17]. Yesu alisema kwamba Mungu apenda kuwe na shirika ambalo litatangaza Huruma ya Mungu kwa ulimwengu na kwa sala zake kuipata Huruma kwa ajili ya dunia (Hafidhi 436). [18] Katika mafunuo ya baadaye alieleza kuwa haitakuwa shirika moja, lakini kazi kubwa katika Kanisa, ambayo itajumuisha mashirika ya kutafakari na ya kitume, na waumini wote duniani kote.

Mnamo tarehe 13 - 14 Septemba 1935 Yesu alimtajia maneno ya sala inayojulikana kama Rozari ya Huruma. Kwa mujibu wa hafidhi yake mtakatifu Faustina, Yesu aliwaahidia wote wanaosali dua hiyo kwa imani kwamba wao watajaliwa neema zake zote, hasa neema ya kifo chema chenye shwari na hiyo itawahusu hata wao ambao wakifa wataoombewa sala hiyo na watu wengine.

Mnamo Oktoba 1937 Yesu alimdokezea Sista Faustina namna mpya ya ibada ya Huruma ya Mungu, yaani aliamuru watu waheshimu muda wa kifo chake msalabani: "Saa tisa alasiri, omba Huruma yangu, hasa kwa ajili ya wakosefu; na walau kwa kitambo kifupi jizamishe kwenye Mateso yangu, hasa pale nilipoachwa peke yangu bustanini katika saa ya masikitiko makuu. Hii ni saa ya huruma kubwa kwa dunia nzima." (Hafidhi. 1320). [19]

Hafidhi

Hafidhi yake Sista Faustina imeandikwa mjini Vilnius na Krakow kati ya 1934 na 1938 kwa msingi wa maelekezo ya Yesu, "Andika chini maneno haya, ambia ulimwengu juu ya rehema yangu na upendo wangu. Moto wa huruma unanichoma. Nataka kuumwaga nje kwa ajili ya nafsi ya binadamu. Oh, maumivu gani wananisababishia kwangu wakati hawataki kukubali wao ! Fanya lolote lililo kwenye uwezo wako ili kueneza ibada kwa rehema yangu. Mimi nitatimiza kile mkosacho. Mwambie mwanadamu aumwaye kwamba asogelee na Moyo Wangu wa huruma, nami nitamjaza na amani. Mwambie [watu wote], binti yangu, ya kwamba mimi ni Upendo na Huruma yenyewe". (Hafidhi 1074)[20] ), na agizo la waungamishi: Pd. Michael Sopocko na Baba Joseph Andrasz SJ na kwa idhini ya wakuu wa Usharika. Sentensi za kwanza ambazo zimehifadhika zimeandikwa Julai 1934. Sura za awali kabisa wamechomwa moto na mwandishi, ambaye hivyo alitimiza agizo la malaika wa tuhuma. Kwa sababu hii hafidhi ina maumbile yake ya mwisho yenye mlolongo wa fujo kidogo. Maingizo yake ya mwisho yamefanywa mnamo Juni mwaka 1938. Kwa jumla hafidhi ina sehemu sita. „Hafidhi" ni maelezo ya maisha ya mwandishi rohoni mwake. Anasimulia juu ya maisha yake ya kila siku rohoni na uzoefu wake wa uhusiano maalumu baina yake na Mungu, kwa mfano maono ya Kristo, Mama wa Mungu, malaika na watakatifu, maono ya jahanamu, toharani na mbinguni... Yesu Kristo anapendekeza Huruma ya Mungu kama wokovu wa pekee kwa dunia nzima (Watu hawatakuwa na amani mpaka zamu igeuke na uaminifu kwa huruma Yangu (Hafidhi 300))[21]

Hafidhi inashirikisha pia hotuba ya Huruma ya Mungu ambayo Yesu Kristo alimletea mhusika wetu mtakatifu pamoja na pendekezo la aina jipya za ibada. Hafidhi ya Faustina Mtakatifu inaelezea upendo wake wa Utatu Mtakatifu, ambao ulimwunganisha na Mungu. Kutokana na kumbukumbu inaelekea kwamba tendo la kutangaza Huruma ya Mungu limekuwa kiini kikuu cha maisha yake Maria Faustina. Katika Hafidhi tunapata pia maelezo ya neema za ajabu, baraka ya Mungu lakini pia matatizo na mateso ambayo yeye alilazimika kuyakabili, wajibu wake, maana yake maalumu, ushahidi wa utakatifu wake na thawabu kwa maisha yake mazuri Utaiandaa dunia kwa ajili ya kuja kwangu mara ya mwisho (Hafidhi 429) [22]. Kisha nikasikia maneno, Wewe ni shahidi wa Huruma yangu. Wewe utasimama mbele ya kiti changu cha enzi milele kama ushahidi hai kwa Huruma Yangu (Hafidhi 417) [23]. Mnamo Machi 1959 kutokana na tafsiri kosefu ya Hafidhi, Ikulu Takatifu ilitoa amri iliyokataza watu wasieneze ibada ya Huruma ya Mungu kwa namna yake Sista Faustina (AAS 6 Machi 1959, u. 271). Licha ya tukio hilo kutokana na juhudi zake Askofu Karol Wojtyła (baadaye Papa Yohane Paulo II) taratibu ya kumpatia Faustina hali ya mtu mwenye heri ilianza mjini Kraków. Marufuku haijafutwa mpaka mwaka 1978. Toleo la kwanza la kumbukumbu zake za kiroho lilitolewa mnamo 1981. Kitabu kimekuwa kinatafsiriwa kwa lugha nyingi. Akiongozwa na hafidhi zake Faustina, Papa Yohane Paulo II aliandika Ensiklika yake “Dives in misericordia” (1980) juu ya Mungu “aliye na huruma mno” Kiini cha maabudu haya ni kujenga ule uaminifu kwa Mungu ambao unatimizwa kwa namna ya kutekeleza dhamira zake zilizoko kwenye amri zake, wajibu wa jukumu yake, ualimu wa Injili na ilhamu za Roho Mtakatifu zinazojulikana. Nguzo ya pili ya Maabudu haya ni mwenendo wa kuwahurumia binadamu kwa njia ya matendo, maneno na sala.

Mchakato wa kumpatia hadhi ya mtu mwenye heri na baadaye pia hadhi ya mtu mtakatifu

Terehe 5, Aprili 1978, kufuata ombi la Kardinali Karol Wojtyła, Ikulu Takatifu ilibatili ibada ya Huruma ya Mungu kwa namna zilizochipukiza kutoka Maono ya Sista Faustina. Tarehe 7, Machi 1992 Yohane Paulo II alitoa azimio yake Faustina Kowalska, tena tarehe 21, Disemba 1992 – akatoa azimio la muujiza uliotokana na maombezi wake. Mnamo 18, Aprili 1993 lilitokea tukio Faustina mwenye heri ambalo liliongozwa na Papa Yohane Paulo II. Kaama muujiza unaohitajika kwa ajili ya kumwinua mtu altareni lilichukuliwa tukio ambapo mwanamke aliyekuwa ameshambuliwa na maradhi ya Lymphedema alipona (Lymphedema (kiingereza), Lymphedema (kifaransa)). Tarehe 30, Aprili 2000 uliwadia wakati kwa kumtangaza Faustina mtakatifu, na tukio hili liliongozwa na Papa Yohane Paulo II pia. Sherehe zilifanyika mijini Roma na Kraków. Hapo ndipo sikukuu ya Huruma ya Mungu ilianzishwa Kanisa nzima. Kama muujiza, lilichukuliwa tukio la kumponya padre Mpolandi ventrikali yake ya upande wa kushoto ambayo ilikuwa imeharibiwa (http://sw.wikipedia.org/wiki/Moyo#). Mnamo tarehe 10, Desemba 2005 kutokana na amri ya Askofu Mkuu Władysław Ziółek, alitangazwa mlinzi mtakatifu wa mji wa Łódź.

Tazama pia

Tanbihi

  1. Alan Butler and Paul Burns, 2005, Butler's Lives of the Saints, Burns and Oats ISBN 0860123839 page 251
  2. Martyrologium Romanum
  3. s. M. Elżbieta Siepak, ZMBM, Dar Boga dla naszych czasów, [on-line]. faustyna.pl.
  4. Franciszek Cegiełka, Siostra Faustyna Szafarka Miłosierdzia Bożego, Londyn-Warszawa, Michalineum, 2003, pp. 15-18. ISBN 83-7019-245-9
  5. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 8., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  6. Franciszek Cegiełka, Siostra Faustyna Szafarka Miłosierdzia Bożego, Londyn-Warszawa,Michalineum, 2003, pp. 23-29. ISBN 83-7019-245-9
  7. Franciszek Cegiełka, Siostra Faustyna Szafarka Miłosierdzia Bożego., Londyn-Warszawa, Michalineum, 2003, pp. 37-43. ISBN 83-7019-245-9
  8. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 113., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  9. M. Elżbieta Siepak ZMBM , Dar Boga dla naszych czasów. [on-line]. www.faustyna.pl.(Kipolandi)
  10. Franciszek Cegiełka, Siostra Faustyna Szafarka Miłosierdzia Bożego., Londyn-Warszawa, Michalineum, 2003, pp. 229-235. ISBN 83-7019-245-9
  11. Kalendarium. www.faustina.pl (Kipolandi)
  12. Kalendarium. www.faustyna.pl. (Kipolandi)
  13. Kalendarium. www.faustyna.pl. (Kipolandi)
  14. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 37., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  15. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 37., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  16. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 125., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  17. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 161., ISBN 83-7502-0 12-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  18. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 162., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  19. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 375., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  20. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 322., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul)
  21. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 122., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul
  22. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 160., ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul
  23. Faustyna Kowalska,Dzienniczek. Miłosierdzie Boże w duszy mojej., Warszawa, 2001, p. 156, ISBN 83-7502-012-5 (Diary.Divine Mercy in My Soul

Viungo vya nje