Ezana

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sarafu za Ezana wa Aksum zimepatikana hadi Bara Hindi zikionyesha umuhimu wa himaya yake.

Ezana wa Axum (pia inatamkwa Aezana au Aizan) alikuwa mfalme wa Ufalme wa Aksum (320 hivi – 360 hivi) uliokuwepo katika sehemu ambayo inajulikana siku hizi kama Tigray, kaskazini mwa Ethiopia na Eritrea, lakini pia Yemen. Mwenyewe alijiita mfalme wa Saba, Salhen, Himyar na Dhu-Raydan."[1], miji ya zamani ambayo Ezana alimrithi baba yake Ella Amida (Ousanas) tangu alipokuwa mdogo, mama yake Sofya akiwa kama msaidizi wake.

Imani[hariri | hariri chanzo]

Yeye ndiye alikuwa mfalme wa kwanza wa Axum kupenda dini ya Ukristo, na mmoja baada ya Zoskales kutajwa na wanahistoria maarufu, hali iliyopelekea S.C. Munro kusema kuwa, Ezana "ndiye mfalme maarufu zaidi kuwahi kuongoza ufalme wa Axum."[2]

Yeye alimchagua Frumensyo, mlezi wake wa utotoni kutoka Lebanoni, kuwa mkuu wa Kanisa la Ethiopia. Ni kwamba mwaka 316 hivi, wakati alipotawala Kaisari Konstantino Mkuu kule Roma, meli moja ilikuwa safarini kutoka Shamu kwenda Bara Hindi ikaharibika kwenye pwani ya Ethiopia. Vijana wawili waliokolewa wakapelekwa mbele ya mfalme kule Aksum.

Mmojawao, Frumensyo, alipata haraka sifa za kuwa mwenye elimu na hekima. Akapanda ngazi kuwa mshauri wa mfalme na mwalimu wa wana wake Ezana na Saizana. Frumensyo aliweza kupanda mbegu za imani moyoni mwa vijana hao. Baada ya kuwa mfalme, Ezana akaendelea kumtumia Frumensyo kama mshauri wake.

Siku moja Frumensyo aliomba ruhusa ya mfalme aende nyumbani kuangalia kama wazazi wake bado wanaishi. Mfalme akamruhusu akamwomba atafute kule walimu wanaoweza kufundisha elimu aliyokuwa nayo Frumensyo pamoja na imani ya Kikristo. Frumensyo akamwendea Askofu Mkuu wa Misri aliyemweka wakfu kuwa askofu kwa ajili ya Waethiopia. Hivyo Kanisa lilianza katika nyanda za juu za Ethiopia. Mfalme Ezana akabatizwa akifuatwa na watu wengi wa makao makuu.

Kuna barua ya Kaisari Mwario wa Roma Constantius II kwa Ezana na ndugu yake Se'azana, iliyoomba Frumensyo apelekwe Aleksandria achunguzwe kuhusu imani yake; inawezekana kwamba Ezana alikataa au kupuuzia ombi hilo.[3]

Vita[hariri | hariri chanzo]

Jiwe la Ezana (330-350 hivi) linaeleza kwa Kigiriki, Kisabei na Kigeez ushindi wake juu ya mataifa ya jirani.

Ezana pia alianzisha kampeni mbalimbali za kijeshi, ambazo pia zimo katika maandishi yake. Baadhi ya maandishi yake kwa lugha ya Ge'ez yamepatikana katika eneo la Meroe ambayo yalikuja kuelewa kuwa ni ushahidi wa kampeni mbalimbali zilizofanyika katika karne ya 4, Inawezekana kampeni hizi zilifanywa katika kipindi kati ya ‘Ezana’ au aliyekuja kumrithi Ousanas. Wakati wanahistoria wengine wanadhani kuwa maandishi hayo yanathibitisha kuwa ufalme wa Axum uliangusha ufalme wa Kush, wengine wanadhani kuwa ushahidi huo wa kihistoria unaonyesha kuanguka kwa nguvu za kiuchumi na za kisiasa za utawala wa Meroe kati ya miaka 300.[4]

Kumbukumbu[hariri | hariri chanzo]

Baadhi ya sarafu nchini humo zimepigwa chapa ya moto wake, katika lugha ya Kigiriki “TOYTOAPECHTHXWPA’’ ikimaanisha kuwa, naomba hii iwaridhishe watu hawa. Munro-Hay anagusia suala hili na kusema kuwa maandishi hayo yalikuwa kwa ajili ya kuwapa wananchi mwamko na kuwafanya wawe na mapendo na waaminifu katika taifa lao [5] [6] [7] Lakini mabadiliko makubwa ya sarafu hiyo ni kutoka hali ya Upagani hadi kuweka alama ya msalaba yenye kuonyesha ishara ya Ukristo na pia picha ya minara ya mawe.

Ijapokuwa sarafu za nchi hiyo zimeandika jina lake, Ezana haijulikani katika orodha ya wafalme. Kwa mujibu wa tamaduni mbalimbali za nchini humo, wafalme kama vile 'Abreha na 'Asbeha ndio walioongoza Ethiopia wakati dini ya Kikristo ilipoingizwa, inawezekana ndiyo majina waliyoitwa hawa wafalme kama vile Ezana na ndugu yake. Pengine hayo ndiyo majina yao ya ubatizo.[8]

Ezana na Se'azana, wanachukuliwa kama watakatifu nchini Ethiopia na kukumbukwa tarehe 1 Oktoba[9][10].

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. S. C. Munro-Hay, Aksum: An African Civilization of Late Antiquity (Edinburgh: University Press, 1991), p. 81. ISBN 0-7486-0106-6
  2. Munro-Hay, Aksum, p. 77
  3. Munro-Hay, Aksum, pp. 78ff
  4. Munro-Hay, Aksum, pp. 79, 224.
  5. Munro-Hay, Aksum, p. 192.
  6. A number of coins minted bearing his name were found in the late 1990s at archeological sites in India, indicating trade contacts in that country.
  7. Details in Paul B. Henze, Layers of Time: A History of Ethiopia (New York: Palgrave, 2000), p. 31 n.18.
  8. See "'Ezana" article on Dictionary of African Christian Biography (http://www.dacb.org) Web site at http://www.dacb.org/stories/ethiopia/_ezana.html Archived 5 Mei 2017 at the Wayback Machine.
  9. Holweck, F. G., A Biographical Dictionary of the Saints. St. Louis, MO: B. Herder Book Co. 1924
  10. https://catholicsaints.info/saint-aizan-of-abyssinia/

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Yuri M. Kobishchanov. Axum (Joseph W. Michels, editor; Lorraine T. Kapitanoff, translator). University Park, Pennsylvania: University of Pennsylvania, 1979. ISBN 0-271-00531-9
  • Sergew Hable Sellassie. Ancient and Medieval Ethiopian History to 1270 (Addis Ababa: United Printers, 1972).
  • African Zion, the Sacred Art of Ethiopia, (New Haven: Yale University Press, 1993).
  • Stuart Munro-Hay, Aksum: An African Civilisation of Late Antiquity http://users.vnet.net/alight/aksum/mhak1.html

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]