Dola la Ujerumani

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Dola la Ujerumani 1871-1918
Dola la Ujerumani 1919-1937
Dola la Ujerumani Kubwa 1942

Dola la Ujerumani (Kijer.: Deutsches Reich) lilikuwa jina la Ujerumani kati ya 18 Januari 1871 hadi 1949 (wengine husema: 1945).

Dola hili lilikuwa na vipindi vitatu:

Dola la Kaisari[hariri | hariri chanzo]

1871 nchi mbalimbali katika Ujerumani ziliungana chini ya uongozi wa Prussia baada ya ushindi katika vita dhidi ya Ufaransa wa 1870/71. Mfalme Wilhelm I wa Prussia alitangazwa kuwa Kaisari wa Kijerumani 18 Januari 1871 mjini Versailles katika Ufaransa.

Dola lilikuwa na katiba, serikali na bunge. Chansella wa kwanza alikuwa Otto von Bismarck.

Kipindi hiki kilikwisha katika mapinduzi ya Kijerumani ya Novemba 1918 mwishoni wa vita kuu ya kwanza ya dunia. Kaisari Wilhelm II akajiuzulu na kuondoka nchini.

Jamhuri ya Weimar[hariri | hariri chanzo]

Dola la Ujerumani lilitangazwa kuwa jamhuri. Mkutano wa katiba ulikaa mjini Weimar hivyo katiba mpya iliitwa "Katiba ya Weimar" na hivyo kipindi kilichofuata huitwa Jamhuri ya Weimar. Ujerumani ilikuwa nchi ya kidemokrasia iliyojenga upya uhusiano mwema na nchi jirani.

Utaratibu wa kisiasa iliporomoka katika matatanisho ya kiuchumi baada ya 1930. Vyama vya kikomunisti na kifashisti vilianza kupata kura nyingi.

Dola la Hitler[hariri | hariri chanzo]

30 Januari 1933 Adolf Hitler alikuwa chansella wa Dola la Ujerumani akaanza mara moja kujenga udikteta wake wa Dola la Tatu. Sehemu ya siasa yake ilikuwa kujenga uwezo wa kijeshi wa Ujerumani.

Tangu 1938 Hitler alipanusha eneo la Dola kwa kutwaa Austria na Uceki na kuingiza maeneo haya ndani ya Dola la Ujerumani.

Utawala wake ulilenga kwa vita kuu ya pili ya dunia iliyoanza 1 Septemba 1939. Katika miaka ya kwanza ya vita hii Ujerumani ilitawala sehemu kubwa ya Ulaya. 1942 jina lilibadilishwa kuwa "Dola la Ujerumani Kubwa" (Kijer.: Grossdeutsches Reich) na maeneo mengi ya Poland na Ulaya ya Mashariki yalitangazwa kuwa shemu za Dola.

Mwisho wa Dola la Ujerumani[hariri | hariri chanzo]

Ujerumani ilishindwa na tangu 8 Mei 1945 mataifa washindi walichukua mamlaka ya serikali katika Ujerumani. Marekani, Urusi, Uingereza na Ufaransa ziligawa nchi katika kanda za utawala. Maeneo yote yaliyotwaliwa na Hitler yalitengwa tena. Sehemu kubwa ya Ujerumani katika mashariki -takriban robo ya eneo lake hadi ya 1937- iliondolewa na kuwa sehemu ya Poland ilhali wakazi Wajerumani zaidi ya milioni 10 walifukuzwa.

1949 Wajerumani walianza tena kujitawala katika nchi mbili. Kanda za Marekani, Uingereza na Ufaransa ziliungana kwa jina la Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani. Kanda la Kirusi lilikuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kijerumani.

Hali halisi kipindi cha Dola la Ujerumani kilikwisha hata kama sehemu zote mbili zilidai kuendeleza urithi wake na hakuna tangazo rasmi la kumaliza dola hili.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Dola la Ujerumani kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.