Cape Town
Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Cape Town ( "Mji wa rasi"- Kiafrikaans: Kaapstad; Kixhosa: iKapa) ni mji mkubwa wa tatu wa Afrika Kusini na mmoja kati ya miji mikuu mitatu ya nchi ikiwa ni makao ya Bunge. Pia ni mji mkuu wa jimbo la Rasi Magharibi (Western Cape / Wes-Kaap). Ni sehemu ya Jiji la Cape Town. Eneo lake ni 1,644 km² lenye wakazi 2,375,910 (mwaka 2005).
Jina la mji limetokana na Rasi ya Tumaini Jema iliyoko karibu upande wa kusini.
Ni mji wa kwanza katika eneo la Afrika Kusini hivyo huitwa mara nyingi "mji Mama" wa nchi. Kihistoria mji ulianzishwa kama kituo cha mapumziko kwenye njia ya safri kwa meli kati ya Uholanzi na koloni zake huko Asia hasa Indonesia ya leo. Kampuni ya Kiholanzi ya India ya Mashariki ilimtuma Jan van Riebeeck kwenye rasi kusudi aanzishe kijiji ambako vyakula vitalimwa kwa ajili ya mabaharia njiani. Walowezi Waholanzi pamoja na Wajerumani na Wafaransa walifuata. Wakaona wenyeji Khoikhoi wakikataa kuwafanyia kazi walileta watumwa kutoka visiwa vya Indonesia. Hapo ndipo mwanzo wa jumuiya muhimu ya Waislamu wa Cape Town. Tangu mwaka 1814 rasi ilikuwa koloni ya Uingereza.
Cape Town ulikuwa mji mkubwa wa Afrika Kusini hadi kupatikana kwa dhahabu katika eneo la Johannesburg kuanzia 1887.
Cape Town ina uwanja wa ndege wa kimataifa mkubwa wa pili nchini. Ni mji wa Afrika Kusini unaotembelewa na watalii kushinda miji yote mingine. Wengi wanaona iko kati ya miji inayopendeza hasa kote duniani.
Kisiwa cha Robben Island ilikuwa mahali pa gereza alikofungwa Nelson Mandela; leo ni makumbusho yanayotembelewa na maelfu wa watalii kila mwaka.
Ishara ya mji ni Mlima wa Meza unaotazama hori ya Cape Town ukitenganisha kitovu cha mji na makazi ya Cape Flats.
[hariri] Viungo vya Nje
- Government
- Habari
- Mengine

