Bombomu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Bunduki bombomu)
Bunduki ya Gatling ilikuwa bombomu ya kwanza
Vickers machine gun calibre .303 ilikuwa modeli iliyopendwa kabla ya Vita Kuu I
Bombomu M2 na maganda matupu ya ramia
Askari wa Uganda na bombomu
Bombomu nzito kwenye manowari
Hii ni PKM Machine Gun.

Bombomu (au: bunduki ya mtombo; bunduki ya rashasha; kwa Kiingereza Machine gun) ni silaha ya moto kubwa kiasi inayofyatulia haraka risasi nyingi za mfululizo kutoka kwenye mkanda wa risasi muda wote kiwashio cha silaha inashikwa hadi akiba ya ramia imekwisha, kwa kawaida kwa kiwango cha raundi 300 kwa dakika au zaidi.

Akiba ya ramia imo ama katika chemba yake au ramia zimepangwa katika ukanda unaopita kwenye bombomu. Bombomu ndogu hubebwa na askari mmoja lakini modeli nzito kiasi huhitaji watu wawili hadi watatu.

Bombomu ndogo zaidi huitwa bunduki ya nusu mtombo, hutumiwa kama silaha ya kawaida ya askari, lakini hutumia ramia za bastola. Ni nyepesi, hailengi mbali sana na kusudi lake ni pigano dhidi ya adui aliye karibu.

Bombomu kubwa zaidi hubebwa tena wa watu, hufungwa juu ya gari au magurudumu huitwa mzinga wa bombomu. Hutumiwa pia kwenye manowari na boti za kijeshi, halafu kwenye ndege za kijeshi.

Tofauti na hizo, bunduki za shambulio, silaha za risasi, bastola au vidogo vinaweza kuwa na uwezo wa moto wa moja kwa moja, lakini si kwa ajili ya moto unaoendelea.

Kama darasa la bunduki za haraka za kijeshi, bunduki za silaha ni silaha za moja kwa moja zilizopangwa kutumiwa kama silaha za usaidizi na zinazotumiwa kwa ujumla wakati zilizounganishwa na mlima-au kufukuzwa kutoka chini kwenye bipod au safari.

Modeli za kwanza[hariri | hariri chanzo]

Mitrailleuse na Gatling[hariri | hariri chanzo]

Mtangulizi wa bombomu ya kwanza ilikuwa "Mitrailleuse" iliyobuniwa huko Ubelgiji mnamo 1850. Ilikuwa na kasiba nyingi na kuzungukwa kwa mkono.

"Gatling" ya Marekani ilikuwa bombomu ya kwanza: ilikuwa na kasiba sita na kuzungukuwa pia kwa kombo ya mkono. Wakati wa kuzunguka kasiba ya juu ilifyatulia risasi na mtambo ulijaza kasiba nyingine. Muundo huu uliachwa baadaye kwa sababu haikulenga vizuri. Lakini umerudi tena kwa bombomu zinazotumiwa katika ndege za kivita kwa sababu kasiba nyingi zinaruhusu kufyatulia risasi nyingi bila silaha kushika joto mno kwa sababu kila kasiba inapata nafasi ya kupoa tena.

Maxim[hariri | hariri chanzo]

Bombomu nyingi zilifuata muundo wa Maxim iliyopatikana tangu 1885 na iliyotumia nishati ya marejeo nyuma baada ya kila pigo kuondoa ganda la ramia na kuweka ramia mpya katika silaha. Ilikuwa na kasiba moja tu. Ramia zilipangwa kwa ukanda uliopita katika silaha. Silaha ya Maxim ilikuwa bombomu ya kwanza iliyofaulu kijeshi ikawa chombo muhimu katika upanuzi wa ukoloni wa mataifa ya Ulaya huko Afrika na Asia pasipokuwa na teknolojia hiyo. Wakati wa vita ya Matebele nchini Zimbabwe (1893-1894) kikosi cha Waingereza 50 kilishinda askari 5,000 Wamatabele kwa kutumia bombomu za Maxim 4. Mshairi Mwingereza Hilaire Belloc alitunga shairi kuhusu vita za kikoloni akisema:

"Whatever happens, we have got
The Maxim gun, and they have not"

Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia[hariri | hariri chanzo]

Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia iliona majeshi makubwa yaliyzopigana yakitumia bombomu kila upande. Kuwepo kwa silaha hizi kulilazimisha mabadiliko katika mbinu za vita. Hadi wakati ule mashambulio yalitekelezwa na askari wengi walioshambulia maadui kwa mbio moja kwa moja. Mbinu hii ilisababisha vifo vingi kwa sababu bombomu zilipungua mno idadi ya washambuliaji kabla hawajafikia mahali walipoelekea. Kwa hiyo vita hii iliona mbinu mpya askari wakiambiwa kuchimba mifereji na kusubiri hadi risasi za mizinga ziliponda kwa mifereji ya maadui kwa siku na wiki mfululizo hadi kujaribu shambulio mpya.

Hata kubuniwa kwa vifaru ilikuwa tokeo moja la hatari la bombomu kwa sababu Waingereza walitafuta njia ya kushambulia mifereji ya Wajerumani kwa kumaliza bombomu kwanza bila kupoteza askari wengi mno.

Vita Kuu ya Pili ya Dunia[hariri | hariri chanzo]

Vita hii iliona bombomu nyepesi zaidi zilizohitaji askari wawili, mmoja wa kulenga na kupiga, mwenzake wa kushughulikia ramia. Iliona pia modeli za kwanza za bunduki ya nusu mtombo.

Vilevile modeli nzito zilipatikana kwa wingi katika ndege za kijeshi kwa kushambulia ndege za adui na pia watu ardhini.

Tatizo la silaha hizi ni joto linalojitokeza wakati wa kufyatulia risasi nyingi katika muda mdogo. Palikuwa na modeli zilizotumia mtambo wa maji ya kupoza kasiba lakini hii iliongeza uzito tena.

Mitambo ya kisasa[hariri | hariri chanzo]

Teknolojia imeendelea na kuunda bombomu nyepesi zinazobebwa na askari mmoja tu zikiwa na uwezo wa kufyatulia risasi nyingi kushinda zamani bila kukwama.

Katika matumizi ya kijeshi bunduki za askari wa kawaida zimepokea sifa za bombomu yaani uwezo wa kufyatulia mfululizo.

Modeli kubwa zinazohesabiwa kati ya mizinga iko kwa matumizi juu ya vifaru, kwenye manowari na ndege.

Teknolojia ya vita ya wakati ujao utaona mabadiliko zaidi. Mitambo kama miwani ya kuona usiku inaonyesha bombomu haraka kutokana na joto la kasiba. Hadi sasa ni nchi chache zinazotumia mitambo hii lakini kadiri inavyosambaa silaha inayong'aa kwenye mitambo hii itakuwa hasara.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.