Bethlehemu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mandhari ya Bethlehemu.
Kanisa la Kuzaliwa kwa Yesu mjini Bethlehemu

Betlehemu (kwa Kiarabu "بيت لحم", Beit Lahm) maana yake ni "Nyumba ya mkate" (kutoka Kiebrania בית לחם, ambapo "בית" = nyumba na "לחם" = "mkate") ni mji wa Palestina, maarufu hasa kama mahali alipozaliwa Yesu Kristo kadiri ya Injili ya Mathayo[1] na Luka[2].

Kadiri ya Mathayo, ndivyo ulivyotimia utabiri wa kitabu cha Mika 5:1.

Mapokeo yanataja mahali hapo katika Kanisa la Kuzaliwa lililojengwa mnamo mwaka 330 kwa amri ya Kaizari Konstantino.

Bethlehemu iko kilometa 10 hivi kusini kwa Yerusalemu, mita 765 juu ya usawa wa bahari. Kwa sasa ina wakazi zaidi ya 25,000 ambao wanategemea hasa utalii.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Inakadiriwa kuwa Bethlehemu ilianzishwa miaka 1,400 KK.

Kadiri ya Biblia, Bethlehemu ndio mji asili wa Daudi, mfalme wa pili wa Israeli na babu wa Yesu katika mfululizo wa vizazi vingi.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. 2:1 Yesu alizaliwa mjini Bethlehemu, mkoani Yudea, wakati Herode alipokuwa mfalme. Punde tu baada ya kuzaliwa kwake, wataalamu wa nyota kutoka mashariki walifika Yerusalemu, 2 wakauliza, "Yuko wapi mtoto, Mfalme wa Wayahudi, aliyezaliwa? Tumeiona nyota yake ilipotokea mashariki, tukaja kumwabudu." 3 Mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, yeye pamoja na wakazi wote wa Yerusalemu. 4 Basi akawaita pamoja makuhani wakuu wote na walimu wa Sheria, akawauliza, "Kristo atazaliwa wapi?" 5 Nao wakamjibu, "Mjini Bethlehemu, mkoani Yudea. Ndivyo nabii alivyoandika: 6 `Ewe Bethlehemu katika nchi ya Yuda, kwa vyovyote wewe si mdogo kabisa kati ya viongozi wa Yuda; maana kwako atatokea kiongozi atakayewaongoza watu wangu, Israeli."` 7 Hapo, Herode aliwaita faraghani hao wataalamu wa nyota, akawauliza wakati hasa ile nyota ilipowatokea. 8 Kisha akawatuma Bethlehemu akisema, "Nendeni mkachunguze kwa makini habari za mtoto huyo. Mkisha mpata nileteeni habari ili nami niende nikamwabudu." 9 Baada ya kumsikiliza mfalme, hao wataalamu wa nyota wakaenda. Kumbe ile nyota waliyokuwa wameiona upande wa mashariki iliwatangulia hata ikaenda kusimama juu ya mahali pale alipokuwa mtoto. 10 Walipoiona hiyo nyota, walifurahi mno. 11 Basi, wakaingia nyumbani, wakamwona yule mtoto pamoja na Maria mama yake; wakapiga magoti, wakamsujudia. Kisha wakafungua hazina zao, wakampa zawadi: dhahabu, ubani na manemane. 12 Mungu aliwaonya katika ndoto wasimrudie Herode; hivyo wakarudi makwao kwa njia nyingine.
  2. 2:1 Siku zile, tangazo rasmi lilitolewa na Kaisari Augusto kuwataka watu wote chini ya utawala wake wajiandikishe. 2 Kuandikishwa huku kulikuwa mara ya kwanza, wakati Kirenio alipokuwa mkuu wa mkoa wa Siria. 3 Basi, wote waliohusika walikwenda kujiandikisha, kila mtu katika mji wake. 4 Yosefu pia alifanya safari kutoka mjini Nazareti mkoani Galilaya. Kwa kuwa alikuwa wa jamaa na ukoo wa Daudi alikwenda mjini Bethlehemu mkoani Yuda alikozaliwa Mfalme Daudi. 5 Alikwenda kujiandikisha pamoja na mchumba wake Maria ambaye alikuwa mja mzito. 6 Walipokuwa huko, siku yake ya kujifungua ikawadia, 7 akajifungua mtoto wake wa kwanza wa kiume, akamvika nguo za kitoto, akamlaza horini kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni. 8 Katika sehemu hizo, walikuwako wachungaji wakikesha usiku mbugani kulinda mifugo yao. 9 Malaika wa Bwana akawatokea ghafla, na utukufu wa Bwana ukawaangazia pande zote. Wakaogopa sana. 10 Malaika akawaambia, "Msiogope! Nimewaleteeni habari njema ya furaha kuu kwa watu wote. 11 Kwa maana, leo hii katika mji wa Daudi, amezaliwa Mwokozi kwa ajili yenu, ndiye Kristo Bwana. 12 Na hiki kitakuwa kitambulisho kwenu: mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelazwa horini." 13 Mara kundi kubwa la jeshi la mbinguni likajiunga na huyo malaika, wakamsifu Mungu wakisema: 14 "Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao!" 15 Baada ya hao malaika kuondoka na kurudi mbinguni, wachungaji wakaambiana: "Twendeni moja kwa moja mpaka Bethlehemu tukalione tukio hili Bwana alilotujulisha." 16 Basi, wakaenda mbio, wakamkuta Maria na Yosefu na yule mtoto mchanga amelazwa horini. 17 Hao wachungaji walipomwona mtoto huyo wakawajulisha wote habari waliyokuwa wamesikia juu yake. 18 Wote waliosikia hayo walishangaa juu ya habari walizoambiwa na wachungaji. 19 Lakini Maria aliyaweka na kuyatafakari mambo hayo yote moyoni mwake. 20 Wale wachungaji walirudi makwao huku wakimtukuza na kumsifu Mungu kwa yote waliyokuwa wamesikia na kuona; yote yalikuwa kama walivyokuwa wameambiwa. 21 Siku nane baadaye, wakati wa kumtahiri mtoto ulipofika, walimpa jina Yesu, jina ambalo alikuwa amepewa na malaika kabla hajachukuliwa mimba.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu maeneo ya Asia bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Bethlehemu kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.