Bamba la Uhindi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Bamba la gandunia la Uhindi katika mazingira yake

Bamba la Uhindi ni bamba dogo katika ganda la dunia. Bara Hindi yenye nchi za Uhindi, Pakistan, Bangla Desh, Nepal pamoja na nchi visiwa za Sri Lanka na Maledivi iko juu ya bamba hilo.

Mipaka na mabamba jirani[hariri | hariri chanzo]

Bamba la Uhindi limepakana na bamba la Ulaya-Asia, Bamba la Australia, Bamba la Afrika na bamba la Uarabuni.

Lilisogea chini ya bamba la Ulaya-Asia takriban miaka milioni 10 iliyopita na kusababisha kujikunja kwa ganda la dunia na kutokea kwa milima ya Himalaya na Karakoram.

Bamba la Uhindi limepimwa kuwa na mwendo wa kuelekea kaskazini wa sentimita 5 kwa mwaka. Linaendelea kusogea chini ya bamba la Ulaya-Asia na kulikunja zaidi.

Chini ya Bahari Hindi linakutana na Bamba la Afrika kwenye mgongo kati wa Bahari Hindi.

Matetemeko ya Ardhi[hariri | hariri chanzo]

Mwendo huo na msuguano kati ya mabamba husababisha mishtuko inayojitokeza kama tetemeko la ardhi. Kati ya matetemeko makubwa kulikuwa na:

Tetemeko chini ya Bahari Hindi ya Krismasi 2004[hariri | hariri chanzo]

Tarehe 26 Desemba 2004 lilitokea tetemeko kubwa la ardhi chini ya Bahari Hindi kwenye mstari ambako bamba la Uhindi linasogea chini ya bamba dogo la Burma. Siku ile km 1,200 za pembizo la bamba la Uhindi zilisogea mbele katika muda wa dakika chache kwa urefu wa takriban m 15 chini ya bamba la Burma. Bamba la juu lilisukumwa na kupaa juu takriban mita 30. Mshtuko huo ulianzisha wimbi kubwa chini ya bahari lililotokea juu kwa umbo la tsunami lililoua takriban watu 275,000.

Tetemeko la Kashmir 2005[hariri | hariri chanzo]

Tarehe 8 Oktoba 2005 mwendo wa bamba la Uhindi chini ya Himalaya ulisababisha tetemeko la ardhi lililoua takriban watu 60,000 na kuharibu nyumba za watu milioni 2.5. Kitovu cha mshtuko kilikuwako karibu na Muzaffarabad katika eneo la Azad Kashmir upande wa Pakistani wa Kashmir.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hiyo kuhusu "Bamba la Uhindi" inatumia neno ambalo si kawaida na matumizi yake ni jaribio kwa jambo linalotajwa.
Wasomaji wanaombwa kuchangia mawazo yao.

Kamusi za Kiswahili ama zinatofautiana kuhusu matumizi ya neno hili au hazieleweki au hazina neno kwa jambo linalojadiliwa.