André-Marie Ampère

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

'

André-Marie Ampère
Andre Ampere mwaka 1825
Amezaliwa(1775-01-20)20 Januari 1775
Lyon, Ufaransa
Amefariki10 Juni 1836 (umri 61)
Marseille, Ufaransa
Kazi yakeMwanafizikia


André-Marie Ampère (20 Januari 177510 Juni 1836)[1] alikuwa mtaalamu wa fizikia na hisabati kutoka Ufaransa.

Ana umaarufu kama mtu aliyeweka misingi muhimu kwa sayansi ya usumakuumeme. Katika mfumo wa vipimo sanifu vya kimataifa kipimo cha mkondo wa umeme kimepewa jina lake na kwa Kiswahili kinaandikwa ampea.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa nchini Ufaransa wakati wa Zama za Mwangaza. Baba yake aliyekuwa mfanyabiashara tajiri hakumtuma shule bali alimpa nafasi ya kujisomea nyumbani.

Mwaka 1799 alipata ajira ya kwanza kama mwalimu wa hisabati na mwaka 1802 aliitwa kuwa mwalimu wa fizikia na kemia mjini Bourg-en-Bresse.

Baada ya kifo cha mke wake mwaka 1803 alihamia kufundisha kwenye chuo cha École Polytechnique mjini Paris. Huko alipewa nafasi ya profesa mwaka 1809 ingawa hakuwahi kusoma shuleni wala chuoni wala kuwa na digrii yoyote.

Mwaka 1820 Ampere alijifunza kuhusu kazi ya Mdenmark Hans Christian Ørsted aliyegundua ya kwamba sindano ya dira inaathiriwa na mkondo wa umeme unaopita karibu nayo. Hapo Ampère alianza uchunguzi kwa lengo la kuelewa uhusiano baina ya usumaku na umeme.

Alijumlisha matokeo yake mwaka 1827 katika kitabu Mémoire sur la théorie mathématique des phénomènes électrodynamiques uniquement déduite de l’experience (Kumbukumbu ya nadharia ya kihisabati kuhusu matukio ya dainamia umeme, iliyofikiwa hitimisho kwa njia ya maarifa na majaribio). Kitabu hiki kiliweka msingi kwa jina la sayansi mpya kuwa "dainamia umeme" (electrodynamics).

Mwaka 1827 Ampère aliheshimiwa kwa kuchaguliwa mwanachama mgeni wa Royal Society wa Uingereza na mwaka 1828 kama mwanachama wa Akademia ya Sayansi ya Uswidi.[2]

Kwa heshima ya kazi yake kipimo cha mkondo wa umeme kiliitwa "ampea", pamoja na coulomb, volti, ohm na watt. Vipimo hivi viliitwa kwa heshima ya wataalamu waliofanya kazi pamoja na Ampère na hao walikuwa Charles-Augustin de Coulomb wa Ufaransa, Alessandro Volta wa Italia, Georg Ohm wa Ujerumani na James Watt wa Uskoti.

Jina la Ampere liko kati ya majina 72 yaliyoandikwa kwenye Mnara wa Eiffel mjini Paris.

Katika miaka yake kwenye vyuo mbalimbali alifundisha hisabati, fizikia, falsafa na astronomia.

Alikuwa Mkristo Mkatoliki tena Mfransisko aliyechukua muda kujisomea katika Biblia hasa wakati wa matatizo maishani.[3]

Kabla ya kufa mwaka 1836, Ampère aliagiza kauli ifuatayo iandikwe kwenye jiwe la kaburi lake: "Tandem Felix" (kwa Kilatini: "Hatimaye mwenye heri").

Maandishi[hariri | hariri chanzo]

  • Considerations sur la théorie mathématique du jeu, Perisse, Lyon Paris 1802, [1]
  • Tafsiri ya Kiingereza ya baadhi ya mandishi yake:
    • Magie, W.M. (1963). A Source Book in Physics. Harvard: Cambridge MA. pp. 446–460.
    • Lisa M. Dolling, Arthur F. Gianelli, Glenn N. Statile, ed. (2003). The tests of time : readings in the developement of physical theory. Princeton: Princeton University Press. pp. 157–162. ISBN 978-0691090856. .

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Dictionary of Scientific Biography. United States of America: Charles Scribner's Sons. 1970. 
  2. Library and Archive Catalogue. Royal Society. Iliwekwa mnamo 13 March 2012.
  3. Catholic Encyclopedia. Iliwekwa mnamo 29 December 2007.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

      .
  • Hofmann, James R. (1995). André-Marie Ampère. Oxford: Blackwell. ISBN 063117849X. 

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Wikiquote ina mkusanyiko wa dondoo kuhusu: